Na. Mwandishi Wetu, MWANZA
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja amesisitiza kuwa
fursa zilizoko kwenye Sekta ya Maliasili na Utalii zikitumika ipasavyo
zitasaidia kukuza pato la Taifa
na uchumi wa mtu mmoja mmoja.
Mhe. Mary Masanja ametoa Kauli hiyo leo jijini Mwanza wakati
wa kikao cha pili cha Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Mwanza kwa Mwaka
2020/2021. Amesema takwimu za watalii wanaoingia hapa nchini kuanzia mwaka 1993
walikuwa 230,000. Aidha, mwaka 2019 idadi hiyo ya watalii
iliongezeka na kufikia milioni 1.5.
"Idadi ya Watanzania kwa sasa ni milioni 60, lakini ukingalia takwimu
hizo watalii wanaoingia kwenye hifadhi zetu kuangalia vivutio ni milioni
1.5, hii inaonesha sisi Watanzania tuna kazi kubwa ya kufanya, kuwa
wazalendo na kupenda vile tulivyo navyo" amesema Mhe. Masanja.
Katika hatua nyingine, Mhe. Mary Masanja amewaeleza viongozi wa mkoa
huo kuwa uwepo wa vivutio vingi vya Utalii katika Kanda ya ziwa ni fursa
pekee ya wananchi kuendelea kunufaika akitoa wito kwa viongozi waliohudhuria
mkutano huo wahamasishe Utalii wa ndani kwa nguvu zote. "Ni
lazima tuongeze nguvu katika kuhamasisha utalii wa ndani bila
kusahau kuhamasisha wageni kutoka nje ya nchi yetu , Utalii wa ndani unatuhusu
sisi wenyewe ,nikiuliza hapa wangapi wamefika kwenye hifadhi zetu na kwenye
vivutio mbalimbali tulivyonavyo tutabaini idadi kidogo sana,
nawaomba sana tuhamasishane ’ amesisitiza Mhe. Mary Masanja.
Ameongeza kuwa janga la
Corona limesababisha kuyumba kwa sekta Utalii duniani kote pia hapa
nchini kwa kuwa watalii waliokua wakitegemewa nchi zao zimeathiriwa
na Corona hivyo ni wajibu wa kila Mtanzania kuwa Balozi wa kutangaza
Utalii na kutembelea vivutio vilivyopo
Comments
Post a Comment