WATUMISHI WA MAHAKAMA MPYA ZA WILAYA WAENDELEA KUPIGWA MSASA

 Na Mary Gwera, Mahakama-Morogoro

Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18 zilizozinduliwa hivi karibuni wanaendelea kupatiwa mada mbalimbali za kuboresha utendaji kazi wao katika Mafunzo yanayoendelea kutolewa kwenye Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.

Ikiwa ni siku ya pili ya mafunzo hayo, jana tarehe 29 Novemba, 2022 mada zilizotolewa ni pamoja na; Wajibu na Majukumu ya Mahakama za Wilaya, Utunzaji na matumizi sahihi ya Kumbukumbu na matumizi ya ofisi mtandao ‘e-office’, Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama.

Akiwasilisha Mada ya Wajibu na Majukumu ya Mahakama ya Wilaya, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt amewataka Watumishi wa Mahakama hizo kuwathamini wananchi ambao ndio wateja wanaosababisha wao kuwa kazi, hivyo huduma zitakazotolewa ziwe za viwango.

“Nadhani hapa wote mnafahamu majukumu ya Mahakama mnazofanyia kazi, hivyo tuko hapa kwa ajili ya kukumbushana ili kutoa huduma bora zaidi, ni matumaini yangu na Mahakama kwa ujumla kuwa mtaboreshaji utendaji kazi wenu kwa kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza jukumu kuu la Mahakama la kutoa haki,” amesema Mhe. Sarwatt.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu- Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula amewaasa Watumishi hao kuzingatia utunzaji sahihi wa nyaraka mbalimbali za ofisi na kuwaasa kutunza siri za ofisi na za wateja.

Akiwasilisha mada ya Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama, naye Mchumi Mwandamizi kutoka Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Bi. Felister Fatukubonye amewaeleza washiriki wa Mafunzo hayo kuwa Mahakama ya Tanzania inatekeleza Mpango Mkakati wake wa mwaka 2020/2021-2024-2025, ambapo amewaeleza Watumishi hao kuwa Mahakama ya Tanzania bado inaendelea na uboreshaji wa huduma mbalimbali zenye lengo la kuhakikisha kuwa huduma ya utoaji haki inamfikia mwananchi kwa urahisi.

Aidha, Bi. Felister amesema kuwa, ili jitihada za Mahakama, Serikali na Wafadhili ziweze kuzaa matunda kunahitajika ushirikiano wa pamoja ikiwemo watumishi kubadili mtazamo na fikra ili uboreshaji za miundombinu na kadhalika viweze kwenda sambamba na utoaji huduma bora kwa wananchi.

Mafunzo haya ya Huduma kwa mteja yanaendelea kutolewa na Watumishi hao mpaka tarehe 02 Desemba, 2022 na mada nyingine zitatolewa ikiwemo Jinsi ya kukabiliana na msongo (Stress Management) na kadhalika.

Tarehe 25 Novemba, 2022 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alizindua Mahakama ya Wilaya Busega iliyowakilisha Mahakama nyingine mpya za Wilaya mpya 17, Mahakama hizo zilizojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia ni pamoja na; Butiama, Rorya, Songwe, Gairo, Mkinga, Mvomero, Kilombero, Mbogwe, Nyang'hwale, Kyerwa, Itilima, Missenyi, Kaliua, Uvinza, Buhingwe, Kakonko na Tanganyika.

Sehemu ya Mahakimu na Watumishi wengine wa Mahakama mpya za Wilaya 18 wakifuatilia kwa makini mada iliyokuwa ikitolewa na Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (hayupo katika picha) aliyekuwa akitoa mada ya wajibu na Majukumu ya Mahakama ya Wilaya. Mada hiyo ametoa jana tarehe 29
Novemba, 2022 kwenye Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sharmillah Sarwatt (aliyesimama) akiwasilisha Mada ya wajibu na Majukumu ya Mahakama ya Wilaya kwa Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18.

Watumishi wakimsikiliza kwa makini mtoa mada (hayupo katika picha).
Mkurugenzi wa Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu- Mahakama ya Tanzania, Bw. Malimo Manyambula akitoa mada ya Utunzaji na matumizi sahihi ya Kumbukumbu na matumizi ya ofisi mtandao ‘e-office’ kwa Watumishi wa Mahakama mpya za Wilaya 18 zilizozinduliwa hivi karibuni.
Washiriki wakimsikiliza mtoa mada (hayupo katika picha).
Mchumi Mwandamizi kutoka Kitengo cha Maboresho cha Mahakama ya Tanzania, Bi. Felister Fatukubonye akiwasilisha mada ya Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama kwa Washiriki wa Mafunzo ya Huduma kwa Mteja yanayofanyika kwenye Ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro.
Mkurugenzi Msaidizi kutoka Kitengo cha Maboresho-Mahakama ya Tanzania, Bw. Daniel Msangi akichangia mada ya Mradi wa uboreshaji wa huduma za Mahakama iliyotolewa na Bi. Felister.

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.