Na Rhoda Simba Dodoma
WAKALA wa Maendeleo ya
Uongozi wa Elimu ADEM imesema kuwa imejipanga kutoa Mafunzo
ya Uongozi na Usimamizi wa Shule kwa Walimu Wakuu wapatao elfu 17,000,
mafunzo hayo yakiwa ni kutoa mafunzo ya utawala bora kwa wasimamizi wa
elimu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma
na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu
ADEM Dkt Siston Mgullah wakati akizungumza na waandishi wa habari
jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa majukumu ya wakala huo na
vipaumbele vyake kwa mwaka wa 2022/2023.
Amesema Katika kipindi cha mwaka
2021/2022, Wakala umeweza kushirikiana na mashirika mengine katika kutoa
mafunzo ya Uongozi, Usimamizi na Uthibiti Ubora wa Elimu ikiwemo UNICEF,
EQUIP-TZ, World Bank, GPE-LANES, PS3+, Good Neighbors (TZ, Zanzibar Office),
Mwanamke Initiatives Foundation (MIF), Aga Khan University (AKU, IED, EA) na
Shule Bora.
Aidha amesema malengo mengine
ya wakala kwa mwaka 2022/2023 ni pamoja na Kudahili Walimu 2343 katika
Kozi za CELMA, DEMA na DSQA, kuandaa Kiongozi cha Mwalimu Mkuu na kuandaa
Mwongozo wa Utawala Bora kwa viongozi wa Serikali za Mitaa.
“Malengo yetu ni
kuimarisha usimamizi wa utoaji wa elimu bora shuleni kwa kuzingatia sera,
sheria, kanuni na miongozo ya elimu, kuziba ombwe la maarifa na ujuzi ambalo
kiongozi au mtendaji hakupata katika mafunzo ya awali ya Ualimu na kuongeza
idadi ya viongozi wenye maarifa ya uongozi na usimamizi wa elimu,
“Katika kipindi cha mwaka
2020/2021, Wakala umefanya tafiti mbalimbali zikiwemo za tathimini ya matokeo
ya Mafunzo ya KKK kwa Walimu wa Darasa la III na IV yaliyofanyika Tanzania
Bara, utekelezaji wa uthibiti ubora wa shule na utoaji wa mrejesho kwa walimu
ili kuboresha ufundishaji na ujifunzaji katika shule za Msingi”amesema
Dkt Mgullah
Akizungmzia Kuhusu mafunzo kwa
njia ya masafa,amesema kwa sasa wana mradi na Chuo kikuu cha Mzumbe
kilichopo Morogoro kwa ajili ya kuandaa Moduli za kuendeshea mafunzo ya masafa.
Akizungumzia kuhusu Ufuatiliaji
wa utendaji kazi wa Wakuu wa Shule waliopata mafunzo ya Uongozi na Utawala
katika Elimu, ufuatiliaji wa matokeo ya mafunzo ya Stashahada ya uongozi na
usimamizi wa Elimu na tathmini ya athari za kozi ya Astashahda ya Uongozi,
Usimamizi na Utawala wa elimu iliyofanyika katika mikoa minne.
Katika kipindi cha miaka mitano
(2018- 2022), Wakala umetoa machapisho ya Moduli ya wajibu na majukumu ya
Mjumbe wa Kamati na Bodi ya Shule,Wajibu na majukumu ya Mjumbe wa Bodi ya Chuo
cha Ualimu 2022 Moduli ya uthibiti ubora wa Shule wa ndani 2021 na
uandaaji na usimamizi wa Utekelezaji wa Mpango wa Jumla wa Maendeleo ya Shule -
2018
UTEKELEZAJI WA MALENGO
Amesema Wakala umedahili Walimu
1,839 katika mafunzo ya Stashahada ya Uongozi na Usimamizi wa Elimu (DEMA) na
Stashahada ya Uthibiti Ubora wa Shule (DSQA) ili kuwapa ujuzi na maarifa walimu
katika usimamizi, ufuatiliaji na tathimini katika elimu.
“Wakala umetoa mafunzo ya muda
mfupi kuhusu uthibiti ubora wa shule wa ndani, kwa Maafisa 3,860 (REOs, RAOs,
DEOs, WEOs) ili kuwajengea uwezo wa kusimamia ufundishaji na ujifunzaji wenye
kuleta tija katika elimu,
“Wakala umetoa mafunzo ya muda
mfupi kuhusu uthibiti ubora wa shule wa ndani kwa walimu 7,612 ili kuwajengea
uwezo wa kusimamia ufundishaji na ujifunzaji katika shule wanazosimamia Wakala
umeendesha mafunzo ya muda mfupi kwa Walimu Wakuu na Waratibu wa Taaluma 147
kutoka katika Shule za Msingi na Sekondari Zanzibar, chini ya mradi wa Mwanamke
Initiative Foundation (MIF).
Dkt Magullah amesema Wakala
umeendesha mafunzo ya Kamati za Shule kwa Washiriki 126 katika Mkoa wa Songwe
ili kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji katika Shule na umeandaa mtaala wa shahada
ya menejimenti ya uthibiti ubora wa elimu ili kuimarisha usimamizi na utoaji wa
elimu bora katika ngazi zote za elimu.
Amesema Wakala umefanya Tafiti
sita na kuwasilishwa kwa wadau mbalimbali wa elimu ili kubaini mapungufu na
kuandaa mafunzo wezeshi kwa wahusika, wakala umeandaa Moduli 3 katika eneo la
Uongozi na Usimamizi wa Shule ili kuendesha mafunzo ya kuimarisha ufundishaji
na ujifunzaji wa ujenzi wa umahiri kwa walimu wa Shule za Sekondari Zanzibar na
umeandika vitabu vya kujenga umahiri katika utekelezaji wa Mtaala wa Sekondari
ili kuboresha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji wa masomo ya Sayansi, Hisabati
na Kiingereza kwa ajili ya Shule za Zanzibar.
Nae Mkurugenzi Mkuu wa
Idara ya Habari Maelezo na Msemaji Mkuu Wa Serikali Gerson Msigwa amesema
Serikali inaweka fedha nyingi kwenye sekta ya elimu nchi nzima ambapo kwa mwaka
wa fedha 2022/23, sekta ya elimu pekee imetengewa Shilingi trilioni 5.8. Chuo
hiki ni moja ya juhudi za Serikali za kusimamia ubora wa elimu.
“Fedha hizi ni nyingi ambazo
zinahitaji usimamizi wa karibu, hivyo wale viongozi wa kwenye taasisi
zinazosimamia elimu lazima wawe na ujuzi na mbinu nzuri za kusimamia maendeleo
ya elimu ili tuweze kupata thamani ya fedha zilizotolewa na Serikali,
“Viongozi wanaosimamia Taasisi
za Elimu wanatakiwa wakasome katika chuo hiki ili wakapate ujuzi wakasimamie
vizuri taasisi hizo. Natoa wito kwa waajiri kutosita kuwaruhusu viongozi wa
taasisi za elimu kwenda kusoma ADEM”Amesema Msigwa.
Mwisho
Comments
Post a Comment