Naibu
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) amewaasa wadau wa misitu
kote nchini washiriki kikamilifu katika usimamizi na utunzaji wa maeneo ya
misitu ya vijiji ili kudhibiti mabadiliko ya tabia ya nchi.
Ameyasema hayo leo Novemba 15,
2022 wakati wa ufunguzi wa warsha ya 22 ya Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa
Misitu Tanzania (MJUMITA)mkoani Morogoro.
"Kasimamieni misitu vizuri
msigawe maeneo hovyo, mkaweke mpango wa matumizi bora ya ardhi ili kuzuia uvamizi
kwenye maeneo ya hifadhi" Mhe. Masanja amesisitiza.
Aidha, amewataka viongozi wa
MJUMITA wawaelimishe wananchi juu ya usimamizi wa misitu na umuhimu wa
uhifadhi.
Katika hatua nyingine Mhe. Mary
Masanja amewataka viongozi hao wakemee mila potofu ambazo zinamkandamiza
mwanamke na kumnyima fursa za kushiriki kwenye uhifadhi wa misitu .
'Tuchukue hatua mara moja
kuhakikisha jinsia inazingatiwa ili kulinda misitu yetu na kuhakikisha jamii
inanufaika na uwepo wa Misitu hiyo" ameongeza.
Aidha, amesisitiza kuwa misitu
ikisimamiwa vizuri ina uwezo mkubwa wa kudhibiti mabadiliko ya tabia ya nchi,
kutunza vyanzo vya maji, kuwa makazi ya wanyama hai na chanzo cha mapato kwa
jamii hasa kwa kutekeleza shughuli za ufugaji nyuki.
Lengo la warsha hiyo ni kujenga
uelewa wa pamoja wa dhana za ujumuishi wa wanawake na vijana katika uhifadhi na
kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi, kubadilishana uzoefu wa namna ya
kutekeleza dhana ya ushiriki wa jinsia kwenye uhifadhi wa misitu, kujadiliana
kuhusu fursa na changamoto zinazowakabili wanawake na vijana katika uhifadhi na
ushiriki katika mnyororo wa thamani ya mazao ya misitu.
Comments
Post a Comment