WAANDISHI WA HABARI WAJENGEWA UWEZO WA KUTAFUTA NA KUCHAKATA HABARI ZITAKAZO CHOCHEA UHURU WA KUJIELEZA
DODOMA.
TAASISI ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika,Tawi la Tanzania
(MISA-TAN) imeendesha mafunzo ya siku (3) ya kuwajengea uwezo wa
kutafuta na kuchakata habari zitakazo chochea Uhuru wa kujieleza kwa Wanahabari
zaidi ya 40 kutoka Mikoa ya Tabora, Dodoma, Shinyanga, Simiyu na wenyeji mkoa
wa Singida.
Mafunzo hayo yameandaliwa na MISA TAN kwa ufadhili wa Ubalozi wa
Kanada nchini Tanzania.
Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo mwishoni mwa wiki,
Andrew Marawiti kutoka Misa-Tan, amesema lengo kuu la mafunzo hayo
ni kuwajengea uwezo waandishi wa habari ili kuzalisha maudhui yenye ubora
yanayohusiana na Uhuru wa Kujieleza.
“MISA TAN inatamani kuona vyombo vya habari vinatoa kipaumbele
kuandaa maudhui yatakayochochea Uhuru wa Kujieleza ili tutengeneze jamii ambayo
sauti ya kila mmoja iwe na uwezo wa kusikika.” Alifafanua.
Kwa upande wake Mwezeshaji wa Mafunzo hayo mwandishi mkongwe
Marko Gideon, amewataka Wanahabari kutumia kalamu zao vyema kuandika
habari za uhuru wa kujieleza katika nyanja mbalimbali ili kupaza sauti za
wananchi ambao kwa kiasi kikubwa wanategemea vyombo vya habari kufikisha vilio
vyao.
Bw.Gideon amesema kwamba Uhuru wa Kujieleza ni moja ya nguzo katika kujenga msingi imara Utawala wa bora kwa vile wananchi wote watashiriki katika kutoa maoni kwa ujenzi wa mambo mbalimbali katika taifa.
“Nchi isiyo na Uhuru wa kujieleza hautakuwepo uwajibikaji kwa
viongozi, hakutakuwa na usawa wa kisheria, hakuna uwazi, uchaguzi hauwezi kuwa
huru na haki, wala kudhibiti matumizi mabaya madaraka kwa viongozi, "
amesema
Nao baadhi ya washiriki wameishukuru MISA TAN kwa kuandaa
mafunzo hayo kwani yamewasidia kupata maarifa yatakayowawezesha kuandaa maudhui
bora katika vyombo vyao vya habari.
“Mafunzo
yamenijengea uwezo na nimepata maarifa kuhusu vile ninavyoweza kubainisha
vyanzo vyangu ili habari yangu iweze kuleta mabadiliko katika jamii.” Amesema
Mwamvita Issa mshiriki kutoka mkoa wa Shinyanga.
Comments
Post a Comment