Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Hesabu za Serikali (PAC) imeeleza kuwa, kazi ya uletaji wa mafuta kwa pamoja
nchini inayosimamiwa na Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja
(PBPA) ina tija kwa Taifa kutokana na sababu mbalimbali ikwemo ya nchi
kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta ikiwemo dizeli na petroli.
Hayo yamesemwa na Wajumbe wa
Kamati hiyo baada ya kukagua miundombinu ya kushusha na kupima mafuta
katika Bandari ya Dar es Salaam pamoja na hifadhi kubwa ya mafuta ya kampuni ya
TIPER ambayo Serikali ni mbia kwa umiliki wa hisa asilimia 50.
Ziara hiyo iliyoongozwa na
Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato pamoja na Naibu Katibu Mkuu,
Kheri Mahimbali ambaye alimwakilisha Katibu Mkuu, Wizara ya Nishati,
Eng.Felchesmi Mramba, ilifanyika tarehe 14 Novemba, 2022, ambapo Makamu
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Japhet Hasunga alisema kuwa, lengo la ziara
lilikuwa ni kuona uwezo wa miundombinu hiyo katika kushusha na kuhifadhi
mafuta.
Mhe. Hasunga alieleza kuwa,
baada ya ukaguzi huo Kamati hiyo imejihakikishia kwamba miundombinu iliyopo ya
ushushaji na uhifadhi mafuta ina uwezo wa kukidhi mahitaj ya nchi
hivyo Kamati hiyo imefurahishwa na uwepo wa miundombinu hiyo.
Hata hivyo, Kamati hiyo ilitoa
wito kwa TIPER kujenga miundombinu ya kuhifadhi mafuta katika maeneo mengine ya
nchi ili kuongeza uwezo wa kampuni na nchi katika kuhifadhi mafuta na
pia kuleta urahisi katika usafirishaji wa mafuta hayo ndani na nje
ya nchi.
Awali, kabla ya kufanyika kwa
ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa PBPA, Erasto Mulokozi, aliieleza Kamati
hiyo kuwa, kutoka Wakala huo uanzishwe mwaka 2015 umekuwa na mafanikio
mbalimbali ikiwemo kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta yanayotosheleza
mahitaji na yenye viwango vya ubora unaohitajika.
Manufaa mengine ni Serikali
kuweza kupanga ukusanyaji wa mapato kwa kuzingatia takwimu sahihi, kuweza
kupanga bei elekezi ya mafuta pamoja na kupata unafuu wa gharama za uletaji wa
mafuta nchini kutokana na uagizaji wa mafuta kwa pamoja kwa wastani wa zaidi ya
Dola za Marekani milioni 200 Sawa na shilingi bilioni 462 huokolewa kwa mwaka.
Aidha alisema kuwa, kutokana na
mfumo huo kuleta ufanisi, nchi za jirani pia zinatumia mfumo huo kuagiza mafuta
kupitia Tanzania hivyo kuipatia Serikali mapato kutokana na kuongezeka kwa
matumizi ya bandari.
Aliongeza kuwa, mfumo huo
umesaidia kupunguza upotevu wa mafuta wakati wa kupakua mafuta kutoka melini
ambapo wastani wa Tani 1100 ( lita 1,300,000) huokolewa kila mwezi sawa na
shilingi bilioni 4.3.
Comments
Post a Comment