Serikali imesema itaongeza vitendea kazi yakiwemo magari na pikipiki katika Kanda zenye changamoto za wanyamapori wakali na waharibifu kwa ajili ya kuwezesha kazi ya udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu kunusuru maisha na mali za wananchi wanaoathirika na wanyamapori hao.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja
Hayo yalisemwa Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary
Masanja kwa niaba ya Waziri wa Maliasili alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa
Manyoni Magharibi, Yahaya Massare aliyetaka kujua mikakati ya Serikali ya
kudhibiti Tembo wanaovamia vijiji vya Doroto, Kitaraka, Kamenaga, Gurugu, Muhanga na
Njirii.
Ameongeza kuwa Serikali imekuwa ikitekeleza mkakati wa kudhibiti
wanyamapori wakali na waharibifu kwa kuimarisha vituo vya Askari wa Wanyamapori
nchini ikiwemo kituo cha askari wanyamapori kilichopo katika kijiji cha Doroto
Wilayani Manyoni.
“Wizara imeagiza jumla ya magari 35 na pikipiki 50 ambapo Kanda ya
Manyoni itapatiwa gari moja na pikipiki mbili ili kuwezesha udhibiti wa
wanyamapori wakali na waharibifu” alisema Masanja.
Aidha, amefafanua kuwa katika kipindi cha mwaka 2021/22 jumla ya doria
960 zimefanywa na Askari wa Jeshi la Uhifadhi kudhibiti wanyamapori wakali na
waharibifu hususan tembo na kuongeza kuwa Serikali inaendelea kutoa elimu kwa
wananchi juu ya mbinu rafiki za kudhibiti wanyamapori hao ambapo Askari
Wanyamapori wa Vijiji wa wilaya watapatiwa mafunzo maalum katika Chuo cha
Uhifadhi wa Maliasili kwa Jamii - Likuyu Sekamaganga Mkoani Ruvuma.
Mary Masanja alisisitiza kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii itaendelea kutekeleza mpango wa
kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo mengine yenye
changamoto nchini kwa kadri fedha zinavyopatikana.
Comments
Post a Comment