Na. OMM Rukwa
Mkuu
wa Mkoa, Queen Sendiga akemea kikundi cha matapeli kilichoibuka mkoani humo
maarufu kama rambaramba ambao wanasababisha taharuki kwenye jamii wakisaka
washirikina.
Ametoa
onyo hilo leo (Alhamisi, Novemba 03,2022) wakati wa mkutano wa hadhara na
wananchi wa kijiji cha King’ombe kata ya Kala wilaya ya Nkasi ambapo kwa siku
za hivi karibuni matapeli hao wamekuwa wakichangisha fedha ili waondoshe
ushirikina.
Sendiga
ametoa agizo hilo kufuatia hivi karibuni kutokea kikundi cha watu wanaofanya utapeli
kwa kupita kwenye makazi ya watu na kusaka wachawi hatua inayopelekea taharuki
kwenye wilaya za Nkasi, Kalambo na Sumbawanga.
“Mnaharibu
sifa nzuri ya mkoa wetu, watu wanakimbia nyumba zao kwa kuogopa rambaramba
kufika kusaka wachawi. Kata hii inaongoza kwa kufanya vikao vya kusaka wachawi.
” alisema Sendiga.
Katika
mkutano huo, Sendiga ametoa agizo kwa Jeshi la Polisi kuendesha msako na
kuchukua hatua za kuwafikisha mahakamani watu wanaoendeleza vitendo vya kusaka
wachawi kwenye makazi ya watu.
Naye
Mkuu wa Wilaya ya Nkasi Peter Lijualikali amemhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa
ataongoza kampeni maalum ya kuwasaka watu wanaofanya utapeli kwa kigezo cha
kusaka wachawi kwenye makazi ya watu na kukusanya fedha kwa watu.
Katika
hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amefanya ukaguzi wa vituo vya afya Kate na
Kala ambavyo vimepokea kila kimoja shilingi Milioni Mia Tano (500,000,000)
zilizotokana na tozo ambapo ameagiza Halmashauri kuhakikisha vituo hivyo
vinakamilika kabla ya mwaka 2022 kuisha.
Mwisho.
Comments
Post a Comment