MKURUGENZI wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Joseph
Mafuru ameridhishwa na maandalizi na utayari wa wanafunzi kuelekea kufanya
mtihani wa taifa wa kidato cha Nne na kusema kuwa halmashauri yake inategemea
matokeo bora zaidi ya msimu uliopita.
Mkurugenzi Mafuru aliseme hayo alipofany ziara ya kutembelea
na kukagua maadalizi ya wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani yao ya taifa ya
kidato cha Nne katika shule ya sekondari Miyuji iliyopo jijini Dodoma.
Mafuru alisema “leo nimetembelea shule ya sekondari Miyuji.
Nimekuja kukagua maandalizi ya wanafunzi wa kidato cha Nne na program maalum ya
kuwapa wanafunzi muda wa kutosha wa kusoma ili kujiandaa na mtihani wa taifa.
Nimejionea kuwa wanafunzi wanajiamini na wapo tayari kuanza mitihani wiki
ijayo. Sisi halmashauri tuliamua kuwatengenezea mazingira mazuri ya kusoma. Tukasema
kwa miezi miwili hii tukae na wanafunzi hapa shuleni ili wapate muda wa kutosha
moja musoma na mbili kupumzika”.
Mkurugenzi wa Jiji alisema kuwa taarifa ya awali wanafunzi
hao walikuwa na uwezo wa chini sana. Kutokana na program hiyo maalum wanafunzi wanauwezo
mzuri. “Nimejionea, nimeenda nimekutana na wanafunzi wana ari kubwa ya ufaulu. Kwa
kweli nimshukuru Afisa Elimu Sekondari, Madam Upendo Rweyemamu ambae kimsingi
ndiye aliyeleta hii program kwa Jiji la Dodoma. Iliwasilishwa katika Baraza la
Madiwani wakaridhia na tumeona kujiamini kwa watoto, ogopa mtoto anayekwambia
lete mtihani hata leo, maana yake wapo tayari. Matarajio ya Jiji ni matokeo
bora zaidi ya msimu uliopita” alisema Mafuru.
Aidha, alimshukuru Mkuu wa Shule ya sekondari Miyuji,
Mwalimu Greyson Maige kwa kusimamia program hiyo maalum katika shule yake. “Mwalimu
Maige anajiamini kwamba wanafunzi watafaulu vizuri. Na walimu wake ambao
wamesimamia program hii wanahakikisha kuwa wanafunzi wapo tayari kuanza
mitihani wiki ijayo wakiwa katika mazingira rafiki ukilinganisha na miaka ya
nyuma” alisema Mkurugenzi Mafuru.
Kwa upande wa Afisa Elimu Sekondari Jiji la Dodoma, Mwalimu
Upendo Rweyemamu alisema kuwa maandalizi ya mtihani wa taifa wa kidato cha Nne
yamekamilika. Watahiniwa wote wapo tayari kwa ajili ya mtihani. “Tutakuwa na
jumla ya watahiniwa 6,647 ambao watafanya mtihani. Kati yao wavulana ni 3,019
na wasichana ni 3,628. Tulianza kuwaandaa wanafunzi hawa muda mrefu. Tumekuwa na
program mbalimbali kama program za shule kwa shule na program za ndani ya
wilaya.
Mwl Upendo Rweyemamu akiwajengea ujasiri wanafunzi katika shule ya sekondari Miyuji |
Akiongelea program maalum kwa wanafunzi walioonekana
kuwa ufaulu hafifu alisema kuwa wamefundishwa kupitia program maalum ili waweze
kuongeza ufaulu wao. “Tunaprogram maalum kwa wanafunzi walioonekana wana ufaulu
hafifu. Tuliwatengenezea mazingira ya kuwaweka pamoja na kikosi kazi cha walimu
56 wamekuwa nao kwa zaidi ya miezi miwili. Hivi karibuni tuliwapa mtihani wa jaribio
na wanafunzi wengi walipata daraja A na B katika masomo yao. Wanafunzi hawa tumewaandaa
vizuri na hata kisaikolojia wapo tayari kukabiliana na mtihani” alisema Mwalimu
Rweyemamu.
Akiongelea matarajio ya ufaulu kwa ngazi ya
halmashauri, alisema kuwa matarajio ni kuongeza ufaulu zaidi. “Unapowekeza mahali
unategemea kupata mabadiliko ama mavuno mazuri. Mwaka jana tulikuwa na daraja
la I (652) kati ya wanafunzi 55,326. II (524), III (1,012) IV (2,735) na O (403).
Tulipata ufaulu wa asilimia 93 na GPA ya 3.1. Kwa mikakati tuliyoweka na program
tunazofanya tutapunguza sana Daraja 0. Lakini daraja la I-III litaongezeka sana”
alisema Mwalimu Rweyemamu.
Afisa Elimu huyo alilishukuru Baraza la Madiwani kwa
kuwa msaada kwa idara yake. “Matunda haya ninayopata siyo kwamba napigana
mwenyewe nina nguvu kubwa ya viongozi wangu wakiwemo madiwani, Mstahiki Meya, Mwenyekiti
wa Kamati ya Elimu, Uchumi na Afya, maafisa elimu kata na wakuu wa shule. Shukrani
za kipekee kwa Mkurgenzi wa Jiji kwa ‘support’ kubwa aliyoifanya kwenye idara
yangu. Kama Mkuu wa Idara unaweza kuwa na mawazo mazuri ya jinsi ya kuboresha
taaluma kama usipopata ‘support’ yake huwezi kutoboa” alisema Mwalimu Rweyemamu.
Halmashauri ya Jiji la Dodoma lina vituo 54
vitakavyofanya mtihani wa taifa wa kidato cha Nne mwaka 2022.
MWISHO
Comments
Post a Comment