MKURUGENZI MAFURU ARIDHISHWA MAANDALIZI MTIHANI WA TAIFA WA KIDATO CHA NNE

 Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Joseph Mafuru ameridhishwa na maandalizi na utayari wa wanafunzi kuelekea kufanya mtihani wa taifa wa kidato cha Nne na kusema kuwa halmashauri yake inategemea matokeo bora zaidi ya msimu uliopita.

Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Joseph Mafuru alimsaidia mwanafunzi Sara Mchiwa somo la Jiografia alipotembelea shule ya sekondari Miyuji kukagua maandalizi ya mtihani wa taifa wa kidato cha Nne na kuzungumza na wanafunzi


Mkurugenzi Mafuru aliseme hayo alipofany ziara ya kutembelea na kukagua maadalizi ya wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani yao ya taifa ya kidato cha Nne katika shule ya sekondari Miyuji iliyopo jijini Dodoma.

Mafuru alisema “leo nimetembelea shule ya sekondari Miyuji. Nimekuja kukagua maandalizi ya wanafunzi wa kidato cha Nne na program maalum ya kuwapa wanafunzi muda wa kutosha wa kusoma ili kujiandaa na mtihani wa taifa. Nimejionea kuwa wanafunzi wanajiamini na wapo tayari kuanza mitihani wiki ijayo. Sisi halmashauri tuliamua kuwatengenezea mazingira mazuri ya kusoma. Tukasema kwa miezi miwili hii tukae na wanafunzi hapa shuleni ili wapate muda wa kutosha moja musoma na mbili kupumzika”.

Mkurugenzi wa Jiji alisema kuwa taarifa ya awali wanafunzi hao walikuwa na uwezo wa chini sana. Kutokana na program hiyo maalum wanafunzi wanauwezo mzuri. “Nimejionea, nimeenda nimekutana na wanafunzi wana ari kubwa ya ufaulu. Kwa kweli nimshukuru Afisa Elimu Sekondari, Madam Upendo Rweyemamu ambae kimsingi ndiye aliyeleta hii program kwa Jiji la Dodoma. Iliwasilishwa katika Baraza la Madiwani wakaridhia na tumeona kujiamini kwa watoto, ogopa mtoto anayekwambia lete mtihani hata leo, maana yake wapo tayari. Matarajio ya Jiji ni matokeo bora zaidi ya msimu uliopita” alisema Mafuru.

Aidha, alimshukuru Mkuu wa Shule ya sekondari Miyuji, Mwalimu Greyson Maige kwa kusimamia program hiyo maalum katika shule yake. “Mwalimu Maige anajiamini kwamba wanafunzi watafaulu vizuri. Na walimu wake ambao wamesimamia program hii wanahakikisha kuwa wanafunzi wapo tayari kuanza mitihani wiki ijayo wakiwa katika mazingira rafiki ukilinganisha na miaka ya nyuma” alisema Mkurugenzi Mafuru.

Kwa upande wa Afisa Elimu Sekondari Jiji la Dodoma, Mwalimu Upendo Rweyemamu alisema kuwa maandalizi ya mtihani wa taifa wa kidato cha Nne yamekamilika. Watahiniwa wote wapo tayari kwa ajili ya mtihani. “Tutakuwa na jumla ya watahiniwa 6,647 ambao watafanya mtihani. Kati yao wavulana ni 3,019 na wasichana ni 3,628. Tulianza kuwaandaa wanafunzi hawa muda mrefu. Tumekuwa na program mbalimbali kama program za shule kwa shule na program za ndani ya wilaya.

Mwl Upendo Rweyemamu akiwajengea ujasiri wanafunzi katika shule ya sekondari Miyuji


Akiongelea program maalum kwa wanafunzi walioonekana kuwa ufaulu hafifu alisema kuwa wamefundishwa kupitia program maalum ili waweze kuongeza ufaulu wao. “Tunaprogram maalum kwa wanafunzi walioonekana wana ufaulu hafifu. Tuliwatengenezea mazingira ya kuwaweka pamoja na kikosi kazi cha walimu 56 wamekuwa nao kwa zaidi ya miezi miwili. Hivi karibuni tuliwapa mtihani wa jaribio na wanafunzi wengi walipata daraja A na B katika masomo yao. Wanafunzi hawa tumewaandaa vizuri na hata kisaikolojia wapo tayari kukabiliana na mtihani” alisema Mwalimu Rweyemamu.

Akiongelea matarajio ya ufaulu kwa ngazi ya halmashauri, alisema kuwa matarajio ni kuongeza ufaulu zaidi. “Unapowekeza mahali unategemea kupata mabadiliko ama mavuno mazuri. Mwaka jana tulikuwa na daraja la I (652) kati ya wanafunzi 55,326. II (524), III (1,012) IV (2,735) na O (403). Tulipata ufaulu wa asilimia 93 na GPA ya 3.1. Kwa mikakati tuliyoweka na program tunazofanya tutapunguza sana Daraja 0. Lakini daraja la I-III litaongezeka sana” alisema Mwalimu Rweyemamu.

Afisa Elimu huyo alilishukuru Baraza la Madiwani kwa kuwa msaada kwa idara yake. “Matunda haya ninayopata siyo kwamba napigana mwenyewe nina nguvu kubwa ya viongozi wangu wakiwemo madiwani, Mstahiki Meya, Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu, Uchumi na Afya, maafisa elimu kata na wakuu wa shule. Shukrani za kipekee kwa Mkurgenzi wa Jiji kwa ‘support’ kubwa aliyoifanya kwenye idara yangu. Kama Mkuu wa Idara unaweza kuwa na mawazo mazuri ya jinsi ya kuboresha taaluma kama usipopata ‘support’ yake huwezi kutoboa” alisema Mwalimu Rweyemamu.

Halmashauri ya Jiji la Dodoma lina vituo 54 vitakavyofanya mtihani wa taifa wa kidato cha Nne mwaka 2022.

 



MWISHO


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.