MKURUGENZI MAFURU AMSHUKURU RAIS SAMIA KWA SHILINGI 580,000,000 UJENZI WA MADARASA 29 YA SEKONDARI DODOMA
Na. Dennis Gondwe, DODOMA
HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imemshukuru Rais Samia Suluhu
Hassan kwa kuipatia fedha shilingi 580,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa
29 ya shule za sekondari kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi kusoma kwa nafasi
na katika mazingira bora.
Mkurugenzi wa Jiji, Joseph Mafuru akimshukuru Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kwa kulipatia Jiji la Dodoma shilingi 580,000,000 fedha za ujenzi wa madarasa 29 ya shule za sekondari
Mafuru alisema “kwa mara nyingine tena tunamshukuru
sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kwa hili
alilotufanyia Jiji la Dodoma, ametufanyia mara ya pili mfululizo kwa elimu ya
sekondari. Katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma hatutarajii watoto watakaofaulu
Darasa la saba watapa shida kujiunga na kidato cha kwanza Watakuta madarasa
yote yapo kamili. Kwa hiyo, mwezi Januari ni kuingia darasani na kusoma”.
Alisema kuwa Rais Samia Suluhu Hassan aliipatia
Halmashauri ya Jiji la Dodoma shilingi 580,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa
madarasa 29 ya shule za sekondari. “Nimezunguka baadhi ya shule kukagua hali ya
ujenzi wa madarasa unavyoendelea. Ndugu wanahabari, mmejionea katika shule hii
ya sekondari Miyuji wapo kwenye ‘roofing stage’. Sisi Halmashauri ya Jiji la
Dodoma, ofisi ya Mkuu wa Mkoa ilitupatia muda wa mwisho kumaliza ujenzi wa
madarasa haya tarehe 15 Disemba, 2022 kuwa tumekamilisha ujenzi wa madarasa yote
29. “Sisi tuliporudi ofisini tukasema hebu tutengeneze programu yetu ya ndani
ili tuwe na muda wa kutosha kufanya marekebisho pale yatakapohitajika.
Nimeongea na Mwalimu Maige na mafundi hapa tunakabidhiwa madarasa haya tarehe
15 Novemba, 2022” alisema Mafuru.
Akiongelea kasi ya ujenzi huo kwa shule nyingine
zinazotekeleza ujenzi wa madarasa hayo alisema kuwa inaenda vizuri. “Nimeongea
na Afisa Elimu Sekondari, Madam Upendo Rweyemamu na kunihakikishia kuwa maeneo
yote kasi inalingana. Hivyo, tupo asilimia 90 ya ujenzi kwenye madarasa haya. Bahati
nzuri Afisa Elimu alishatoa maelekezo kwamba wakati tunaendelea na ujenzi huu
waanze kutengeneza meza na viti. Nimekuta tayari shule ya sekondari Miyuji
wameshaanza na kuandaa viti na meza 100 na tarehe 15 tunakabidhiwa madarasa,
viti na meza” alisema Mafuru.
Akitoa maelezo ya mradi wa ujenzi wa madarasa mawili
katika shule ya sekondari Miyuji, Mkuu wa shule hiyo, Mwalimu Greyson Maige alisema kuwa shule yake ilipokea
shilingi 40,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa mawili na ofisi moja.
“Baada ya kupokea fedha hizo tulipokea maelekezo toka Ofisi ya Mkurgenzi juu ya
matumizi ya ‘force account’. Tuliunda kamati tatu. Kamati ya ujenzi, manunuzi
na mapokezi ya vifaa. Baada ya hapo tukafanya taratibu za kumpata fundi,
tukafanya taratibu za kupata wazabuni walio bora. Mpaka sasa mradi umefikia
hatua nzuri. Ofisi ya Mkurugenzi imetusaidia sana na kamati za shule
zimetusaidia sana. Wanakamati wamefanya kazi kwa weledi bila kuchoka” alisema
Maige.
Mwalimu Greyson Maige |
Akiongelea faida za mradi huo, alizitaja kuwa ni wanafunzi
kuwa na madarasa bora kwa ajili ya kujifunzia na kupunguza mrundikano
madarasani na walimu kuweza kufundisha vizuri na kuongeza ufaulu wa wanafunzi.
Awali akitoa maelezo ya utangulizi kwa Mkurugenzi wa
Jiji, Afisa Elimu Sekondari wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma alisema kuwa jiji
hilo lilipokea fedha shilingi 580,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 29,
na shule ya sekondari Miyuji ni moja ya shule zinazotekeleza ujenzi wa madarasa
hayo ikiwa inajenga madarasa mawili.
MWISHO
Comments
Post a Comment