Na Mary Gwera, Mahakama
Mahakama ya Tanzania inaendelea na jitihada mbalimbali za
kuhakikisha kuwa inatekeleza ipasavyo jukumu lake la msingi la utoaji haki
sambamba na kufikia kwa vitendo Dira yake ya Utoaji Haki Sawa kwa
wote na kwa wakati.
Jitihada hizi zinadhihirishwa na kasi ya uondoshaji wa mashauri
katika ngazi mbalimbali za Mahakama nchini ikiwemo Divisheni za Mahakama Kuu ya
Tanzania mojawapo ikiwa ni Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi.
Katika kikao cha Watumishi wa Divisheni hiyo kilichofanyika hivi
karibuni katika ukumbi wa Shule ya Sheria ‘Law School’ jijini Dar es Salaam,
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Mhe. Agnes Mgeyekwa
amewapongeza watumishi wa Divisheni hiyo kwa kufanya kazi kwa bidii na
ushirikiano ulioiwezesha Mahakama hiyo kuondosha jumla ya mashauri 2249 kwa
kipindi cha mwezi Februari 2022 hadi Oktoba mwaka huu.
Akizungumza na Watumishi wa Divisheni hiyo, Mhe. Mgeyekwa alisema
kuwa idadi hiyo inajumuisha jumla ya mashauri ya mlundikano 167 yaliyovuka
mwaka 2021.
“Kila mtumishi amekuwa na mchango mkubwa sana kwa sababu kazi ya
kuondosha mashauri sio kwa Majaji peke yao, bali kila mtumishi. Hivyo, pongezi
za takwimu nzuri za uondoshaji mashauri zinakwenda kwa kila mtumishi wa
Divisheni hii,’ alisema.
Anaeleza kuwa, katika kipindi hicho cha Februari hadi Oktoba mwaka
huu mashauri yaliyofunguliwa yalikuwa 1684, yaliyoamuliwa 2249 na yanayoendelea
(pending) ni 1014.
Aidha; Mhe. Mgeyekwa anabainisha kuwa, hadi kufikia tarehe 04
Novemba, 2022 mashauri ya mlundikano yaliyosalia katika Divisheni hiyo ni 46 pekee
huku 12 kati ya hayo yapo nje ya uwezo wa Mahakama hiyo kwa sababu kuna
mashauri ya rufaa yanaendelea Mahakama ya Rufani na sababu nyingine ni kutolewa
kwa amri za kutoendelea kuyasikiliza kutoka Mahakama ya Rufani. Ameongeza kuwa,
“mkakati uliopo ni kumaliza mashauri 34 kabla ya mwisho wa mwaka huu.”
Jaji Mfawidhi huyo anaongeza kwamba, Divisheni ya Ardhi imefanya
jitihada mbalimbali zenye lengo la kuondosha mashauri mojawapo ikiwa ni pamoja
na kutumia vikao maalum vya kuendesha mashauri ‘sessions’ ambapo mashauri 59
yalipangiwa mbele ya Majaji watano (5) kutoka nje ya Kituo, kati ya hayo
mashauri 51 yalimalizika, saba (7) yanaendelea kusikilizwa na shauri moja (1)
linasubiri hukumu.
“Divisheni imeweka kipaumbele cha kibajeti kwenye kuondosha
mashauri hasa ya mlundikano ili kufikia malengo iliyojiwekea ambapo
walilazimika kualika Majaji na Naibu Wasajili kutoka vituo vingine ili kuongeza
nguvu zaidi ya kuondosha mashauri hayo,” anasisitiza Jaji Mfawidhi.
“Mbinu hii yenye matokeo chanya huongeza matumizi ya bajeti, kwa
kuwa mashauri ndiyo jukumu la msingi la Mahakama, Menejimenti imeona ni busara
kujikita kwenye matumizi hayo, ambapo tulialika Majaji na Naibu Wasajili
walioendesha vikao vya Mahakama ‘session’ na kuiwezesha Divisheni kung’ara na
hivyo watumishi wote mnastahili kujipongeza na kuona fahari,” alisisitiza Mhe.
Mgeyekwa.
Katika kikao hicho kilichohudhuriwa na Majaji na Watumishi wote wa
Divisheni hiyo, mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo Mpango Mkakati wa
Mahakama wa 2020/2021 hadi 2024/2025. Katika mada hii watumishi watatu (3) wa
Divisheni hii Bw. Ukani, Mlinzi, Bi. Carolina Mambo, Msaidizi wa Kumbukumbu na
Bi. Radhia Mpinga, Mwandishi Mwendesha Ofisi walifanya mawasilisho kwa umahiri
mkubwa na kuonesha namna ambavyo Mpango Mkakati umeeleweka kwa watumishi wa
kada zote.
Aidha, Mtaalam Mwezeshaji wa mada hii alikuwa Bw. Kisingi Mhando,
Mchumi kutoka Makao Makuu ya Mahakama ambaye alitoa ufafanuzi wa kina kuhusu
vipengele muhimu vya Mpango Mkakati huo na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji
wake.
Mada nyingine iliyowasilishwa na Mwezeshaji, Bi. Betty Jones
almaarufu kama ‘BJ’ ilihusu Mbinu za Kukabiliana na Msongo wa Mawazo (Stress
Management) katika maisha ya kila siku nje na mahali pa kazi ili kuwajengea
watumishi uwezo na mbinu za kumudu msongo ‘stress’ na kutimiza malengo ya
Taasisi.
Kadhalika, Mada nyingine iliyowasilishwa ilihusu Mpango wa Bajeti
ya Divisheni, Usimamizi na Matumizi yake kwa Mwaka 2022/23 iliwasilishwa na Bw.
Peter Mbaguli, Afisa Tawala akishirikiana na Bibi. Hawa Wanguvu, Afisa Hesabu
Mwandamizi.
Katika majadiliano ya pamoja watumishi walitoa hoja zilizolenga
kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa kuongeza idadi ya watumishi, vitendea
kazi, vikao vya watumishi wote pamoja na kuboresha masilahi ya watumishi ili
kuwapunguzia ukali wa maisha.
Katika ufafanuzi wa hoja hizo, Mtendaji wa Mahakama Kuu-Divisheni
ya Ardhi, Bw. Anatory Kagaruki alisema kuwa masuala yote yanazingatiwa
kikamilifu huku na kuongeza kuwa, uwezo na mipango ya kibajeti katika ngazi ya
Taasisi na Divisheni ndiyo unaotoa dira ya namna ya kutimiza mahitaji hayo.
Alifafanua kuwa ipo mipango na mikakati ya kimenejimenti ya ndani ya Divisheni
na ile ya kitaasisi ya kuboresha mazingira ya kazi. Alitoa mfano wa Programu ya
Kuboresha Maslahi ya Watumishi wa Mahakama inayotekelezwa na Viongozi wa
Mahakama ya Tanzania wakiongozwa na Mtendaji Mkuu.
Pamoja na kuwapongeza watumishi kwa kuchapa kazi kwa bidii, Bw.
Kagaruki pia aliwasihi watumishi hao kuendelea kuwa wavumilivu, kufanya kazi
kwa juhudi na maarifa ili kutoa huduma kwa kiwango kinachotarajiwa na wananchi,
Serikali na Viongozi wa Mahakama.
"Nichukue nafasi hii kuwapongeza Watumishi wenzangu kwa
kuchapa kazi, hata hivyo tusisahau vipaumbele vyetu ambavyo ni kuendelea na
matumizi ya TEHAMA, kuimarisha ushirikiano na wadau na nidhamu kwa
watumishi," alisema Bw. Kagaruki.
Kikao hicho kilichosheheni matukio mbalimbali kilihitimishwa kwa
kuwapongeza na kuwakaribisha Majaji wageni walioteuliwa Mwezi Agosti 2022 na
kupangiwa Divisheni ya Ardhi. Katika tukio, Jaji mpya wa Divisheni hiyo, Mhe.
Kevin Mhina alizungumza kwa niaba ya Jaji mwenzake Mhe. Jaji Hemed Lusungu kuwa
wanaahidi kufanya kazi kwa ushirikiano na kuahidi kwamba wanaungana na Timu ya
Divisheni ya Ardhi kutimiza malengo yaliyopo.
Zoezi lingine lililofanyika lilikuwa ni la utoaji wa zawadi kwa
mfanyakazi bora wa Divisheni hiyo Bw. Nkotya Muro, Mlinzi ambaye alipongezwa na
Jaji Mfawidhi kwa kuchaguliwa na wafanyakazi na kuwasihi watumishi wengine hasa
vijana kuiga mfano huo.
Akitoa neno la kufunga kikao kwa niaba ya Jaji Mfawidhi, Jaji wa
Mahakama Kuu-Divisheni ya Ardhi, Mhe. Isaya Arufani alipongeza uongozi wa
Divisheni hiyo kwa kuandaa kikao hicho na matukio yote ambayo yamewaunganisha
pamoja. Akiongeza kwamba, tukio hilo limesisimua ari na morali ya watumishi
wote na kwamba ufanisi na tija ya kazi itaongezeka maradufu.
Watumishi walionesha kufurahishwa na kikao hicho na kushauri vikao
na matukio ya aina hiyo yafanyike mara kwa mara kwa sababu yanaimarisha umoja
na upendo miongoni mwa watumishi. Mtumishi mmoja alisema kuwa kukaa pamoja na
Majaji ambao ni viongozi adimu kukutana nao tena nje ya mazingira ya ofisi ni
suala la kupongeza na kuendelezwa kwa kuwa inafanya watumishi kuwafahamu zaidi
viongozi wao na hata kujifunza mambo mengi kutoka kwao.
Katika kuhakikisha kwamba, azma ya Mahakama ya kuongeza kasi ya
usikilizaji wa Mashauri na kuondoa mlundikano, Mahakama iliweka idadi ya
mashauri yanayopaswa kumalizwa na Maafisa wa Mahakama (Majaji na Mahakimu)
ambapo Hakimu wa Mahakama za Mwanzo anapaswa kumaliza mashauri 260 kwa mwaka,
mashauri 250 kwa Mahakama za Hakimu Mkazi na mashauri 220 kwa ngazi ya Mahakama
Kuu.
Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi wakifuatilia kwa makini yanayojiri katika kikao kilichofanyika hivi karibuni |
Watumishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi wakiwa katika kikao kilichofanyika hivi karibuni katika Ukumbi ya Shule ya Sheria 'Law School of Tanzania) jijini Dar es Salaam |
Comments
Post a Comment