JKCI kushirikiana na Poland kutibu magonjwa ya Moyo

Na: Mwandishi Maalum – Dar es Salaam

09/11/2022 Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imesaini mkataba na chuo Kikuu cha Jagiellonian kilichopo nchini Poland kwa ajili ya kushirikiana katika kubadilishana ujuzi wa kutoa huduma za kibingwa za matibabu na upasuaji wa moyo.



Mkataba huo ambao utaanza kutumika mapema mwakani ulisainiwa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha nchini Poland Prof. Bartlomiej Guzik.

Akizungumza na waandishi wa habari hizi Dkt. Kisenge alisema JKCI imesaini mkataba na chuo hicho ili kuweka ushirikiano ambao   umelenga kuongeza wigo katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo pamoja na upasuaji wa moyo katika Taasisi hiyo.

“Tumesaini makubaliano ambayo yatawawezesha wataalam wetu kwenda nchini Poland kwa ajili ya kujifunza namna wenzetu wanavyotoa huduma za matibabu ya moyo lakini wao pia watakuja hapa kwetu kuona na kujifunza jinsi tunavyotoa huduma za tiba na upasuaji wa moyo”,

“katika ushirikiano huu pia tumekubaliana wenzetu hawa watatuletea wataalam ambao watashirikiana nasi katika kuwahudumia wagonjwa kwa kufanya matibabu ya kibingwa ya upasuaji wa moyo hasa kuzibua mishipa ya damu ambayo imeziba, kubadilisha valvu za moyo bila kupasua kifua upasuaji unaoitwa TAVI procedure ambao kwa hapa nchini kwetu bado haujaanza kufanyika”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema JKCI imeongeza wigo wa kuwa na ushirikiano na mashirika yanayotoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kutoka nchi 18 ikiwemo nchi hiyo ya Poland ambayo itaanza rasmi kubadilishana ujuzi na wataalam wa Taasisi hiyo mapema mwakani.

“Tutaendelea kuongeza ushirikiano huu wa kubadilishana uzoefu na nchi nyingine ambazo tunaamini zinatoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo nia ikiwa ni kuifanya JKCI kutoa matibabu ya kibingwa ya magonjwa ya moyo katika Afrika yote”, alisema Dkt. Kisenge

Naye Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Jagiellonian kilichopo nchini, Poland Prof. Bartlomiej Guzik alisema wamevutiwa kufanya kazi na wataalam wa afya wa JKCI ili kwa pamoja waweze kutoa huduma za kibingwa za matibabu na upasuaji wa moyo kwa wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo.

“Kujenga uhusiano baina yetu na JKCI kutasaidia kuboresha huduma za kibingwa za matibabu na upasuaji wa moyo lakini pia kutaongeza ubobezi kwa wataalam hawa wa afya”, alisema Prof. Bartlomiej.



Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.