Na Munir Shemweta, WANMM
NJOMBE
Waziri wa Ardhi Nyumba na
Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ametaka maeneo ya yanayomegwa kwa ajili
ya kupatiwa wananchi waliovamia hifadhi yapangiwe mpango wa matumizi ya ardhi
na kutolewa hati kwa wamiliki wake.
Dkt mabula alitoa kauli hiyo
oktoba 27, 2022 katika kijiji cha Mpanga kilichopo wilaya ya Wanging'ombe
wakati timu ya mawaziri nane wa wizara za kisekta inayoshughulikia migogoro ya
matumizi ya ardhi katika vijiji 975 ilipotembelea mkoa wa Njombe ikiwa ni
mfululizo wa ziara zake kawenye mikoa ya Tanzania Bara.
Kijiji cha Mpanga ni moja ya
vijiji 11 vilivyopo wilaya ya Wanging'ombe na Makete mkoani Njombe ambavyo
vimemegewa eneo kutoka hifadhi ya Pori la Akiba la Mpanga Kipengele.
Dkt Mabula alisema, serikali ya
awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeridhia baadhi ya vijiji
kwenye mkoa wa Njombe kubaki maeneo ya hifadhi za Mapori ya Akiba ingawa
wananchi wake waliingia bila ridhaa ya serikali.
Kwa mujibu wa Dkt Mabula, ili
kuondokana na migogoro ya ardhi vijiji vilivyomegewa maeneo
vitapimwa na kumilikishwa ili wamiliki kujua mipaka sambamba na kuweza kutumia
hati kukopa fedha benki na fedha kutumika kuboresha shamba au mifugo.
"Kinachofanyika hapa siyo
tu kutoa maeneo, eneo linatolewa lakini liwekewe mpango mzuri na endelevu ili
kuona jinsi gani mnaweza kutumia ardhi mliyopewa kwa faida na kwa sababu
tunaongezeka basi mpango uwe mzuri na endelevu" alisema Dkt Mabula.
Amebainisha kuwa, ni lazima
maeneo yanayopangwa yaanishwe matumizi yake kama vile maeneo ya akiba, hifadhi,
makazi na uwekezaji na kutaka wakati wa utekelezaji wataalamu wazingatie mpango
wa matumizi katika maeneo hayo.
Timu ya Mawaziri Nane wa Wizara
za Kisekta ambayo inashughulikia migogoro ya matumizi ya ardhi kwenye vijiji
975 imemaliza ziara yake katika mkoa wa Njombe ukiwa ni mkoa wa 22 kati ya 26
ya Tanzania Bara na inaendelea na ziara yake katika mkoa wa Ruvuma.
MWISHO
Comments
Post a Comment