Na. Dennis Gondwe, DODOMA
WATENDAJI
wa kata katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kuhakikisha utaratibu
wa chakula kwa wanafunzi unafanikiwa kwa kiasi kikubwa ili kuwasaidia watoto
kuondokana udumavu na kupandisha kiwango cha usikivu utakaowapelekea kufaulu
vizuri wanapokuwa shuleni.
Mkurugenzi wa Jiji, Joseph Mafuru akiagiza kutolewa chakula katika shule zote jijini Dodoma |
Agizo
hilo lilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Joseph Mafuru
alipokuwa akisaini Mkataba wa utendaji kazi ya usimamizi wa shughuli za lishe na
maafisa watendaji kata 41 wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika ukumbi wa mikutano
wa halmashauri ya jiji hilo.
Mkurugenzi
Mafuru alisema kuwa lengo la mikataba hiyo ni kuboresha suala la hali ya lishe
na kupunguza athari za utapiamlo katika jamii. “Lazima twende kwa kina zaidi
ili chakula kipatikane kwa wanafunzi. Watendaji wote mtambue majukumu yenu na
muongeze nguvu kwasababu mtoto akiwa na njaa hawezi kusoma wala kuelewa kile
kinachofundishwa darasani. Kuna umuhimu hata wazazi kuelimishwa juu ya watoto
wao hata kupata kifungua kinywa kabla hawajaenda shuleni ili apate nguvu,
lakini kuna baadhi ya shule zimefanikiwa katika jambo hili. Kwahiyo, wale ambao
hawajafanikiwa mnatakiwa kujifunza kwa wenzenu ni njia gani wamezitumia,”
alisema Mafuru.
Akiongelea
mtakata wa utendaji kazi ya usimamizi wa shughuli za lishe, Afisa Lishe wa
Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Semeni Eva Juma alisema kuwa unalenga kutatua
changamoto ya lishe katika Jiji la Dodoma. “Mkataba huu unaosainiwa ni wa miaka
minane hivyo, watendaji wa kata mnatakiwa kuhamasisha jamii kushiriki katika
mpango wa utoaji wa chakula kwa wanafunzi shuleni na kuwatambua wadau wa lishe
wote waliopo kwenye kata na kuhakikisha wanawasilisha taarifa zao kwenye Kamati
ya Maendeleo ya Kata,” alisema Juma.
Afisa Lishe Jiji la Dodoma, Semeni Eva Juma akielezea vipengele katika Mkataba wa Lishe |
Kiongelea
nafasi ya madiwani katika utekelezaji wa masuala ya lishe, alisema kuwa madiwani
wote wanatakiwa kuhakikisha wananchi wanatambua umuhumu wa kushiriki katika
siku ya afya na lishe. Alisema kuwa siku hiyo inalenga kutoa elimu zaidi juu
lishe bora kwa watoto kwasababu wanafunzi wengi wamekuwa wakishindwa kufanya
vizuri katika masomo yao kutokana na kukosa lishe.
Kwa
upande wake Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe katika
Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Andrew Method alisema kuwa maafisa
watendaji wa kata wanapokwenda kuwasainisha maafisa watendaji wa mitaa ni vizuri
kualika na viongozi wengine katika tukio hilo. Uwepo wa viongozi wengine katika
mitaa utawasaidia kuwa mashahidi na kurahisisha utekelezaji wa masuala ya lishe
katika mitaa na kutoa matokeo yaliyokusudiwa, alisema.
MWISHO
Comments
Post a Comment