WANADODOMA WASHAURIWA KUJALI AFYA YA MBWA NA PAKA

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

WAKAZI wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kujali afya ya mifugo (Mbwa na Paka) kwa kuhakikisha wanapata chanjo na matibabu ili kuepuka vifo na madhara yatokanayo na kichaa cha Mbwa.

Mkuu wa Divisheni ya Kilimo mjini katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Yustina Munishi


Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Divisheni ya Kilimo mjini katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Yustina Munishi alipokuwa akitoa ushauri kwa wakazi wa jiji hili katika maadhimisho ya siku ya kuzuia ugonjwa wa kichaa cha Mbwa duniani.

Munishi alisema kuwa jamii inatakiwa kuchukua tahadhari zote dhidi ya ugonjwa wa kichaa cha Mbwa. “Ni muhimu kuhakikisha afya ya mifugo hasa Mbwa na Paka inazingatiwa katika maeneo yetu kwa sababu ugonjwa wa kichaa cha Mbwa unasababisha madhara na vifo kwa binadamu na Mbwa wenyewe. Mfano uwepo wa Mbwa katika makazi yetu ni faida kwa sababu anatusaidia ulinzi lakini pia ni mnyama rafiki katika jamii kama alivyo Paka. Hivyo, jamii ina wajibu wa kuwatunza kwa kuhakikisha wanapata chanjo zote na matibabu ili wawe na afya njema na tuendelee kunufaika nao” alisema Munishi.

Aidha, aliipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa maadhimisho ya siku ya kuzuia kichaa cha Mbwa duniani.

Siku ya kuzuia kichaa cha Mbwa duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 28 Septemba, kwa lengo la kuhamasisha jamii kutokomeza ugonjwa wa kichaa cha Mbwa kwa kufanya kampeni za chanjo na kutoa elimu kwa umma juu ya ugonjwa huu hatari.

Mwaka huu maadhimisho hayo yameongozwa na kaulimbiu isemayo Afya moja: Bila vifo.

 

MWISHO

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.