Wakuu wa Mikoa Kusimamia Usajili wa wakulima utoaji mbolea ya ruzuku


Na Fred Kibano, Dodoma

Serikali imewaagiza wakuu wa mikoa kote nchini kusimamia kwa ukamilifu zoezi la kuwasajili wakulima kwa ajili ya zoezi la mfumo wa utoaji wa mbolea ya ruzuku kwa msimu wa mwaka 2022/20223.

Waziri Innocent Bashungwa


Hayo yalisemwa na Innocent Bashungwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI wakati akitoa salamu kwenye kikao maalum kati ya Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wizara ya Kilimo kilichowahusisha wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa katika ukumbi wa St. Gaspar jijini Dodoma jana.

Lipo suala la wakulima, waheshimiwa wakuu wa mikoa na makatibu tawala wa mikoa, ili tuweze kupeleka huduma kwa mkulima, kuna suala la kusajili wakulima wetu, Wizara ya Kilimo inatutegemea sisi ili kuhakikisha suala la kuwasajili wakulima linafanikiwa kwa kiasi kikubwa” alisema Bashungwa.

Bashungwa amesema pia lengo la kikao hicho ni sehemu ya kujipanga katika kuhakikisha utekelezaji wa dira na maelekezo ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha yanatokea mapinduzi chanya kwa wakulima kote nchini.

Akitoa hotuba katika kikao hicho, Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe amesema wizara yake inazingatia teuzi za Bodi za Kilimo kuwa na mkuu wa mkoa kama mjumbe kwasababu wao pamoja na wakuu wa wilaya, makatibu tawala wa mikoa ndio kama mikono ya Wizara ya Kilimo na lazima wahusishwe kwenye masuala yote ya kilimo kwenye maeneo yao.

Bashe amesema katika mwaka huu wa fedha Wizara ya Kilimo itaajiri Wahandisi wa umwagiliaji ambao watapelekwa katika kila halmashauri zoezi ambalo litakwenda sambamba na kuwapatia magari kwa ajili ya ufuatiliaji wa kazi zao.

Pia wizara hiyo inaendelea kugawa pikipiki kwa Maafisa Ugani ambazo idadi yake itafikia 7,000 kwa ajili ya maafisa hao ngazi ya halmashauri Tanzania Bara kuweza kuwahudumia wakulima kwa kuongeza uzalishaji na kupunguza gharama za kilimo.

Aidha, amesema mfumo mpya wa ruzuku ya utoaji wa mbolea unatumia kanzi-data kuanzia ngazi ya kitongoji, kijiji hadi ngazi ya juu na mpaka sasa jumla ya wakulima halali 1,297,240 wamekwishasajiliwa.

Katika hatua nyingine Waziri Bashe amesema wizara yake inatarajia kujenga maghala 62 mapya kwa ajili ya kuhidhia mazao ambapo mkoa wa Ruvuma utakuwa na maghala 31sawa na asilimia 80 ya maghala yote.  

Kwa upande wake Mkurugeni wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea nchini (TFRA), Dkt. Stephan Ngailo amesema jumla ya shilingi Bilioni 150 zimetolewa na Serikali katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kutekeleza Mpango wa utoaji wa mbolea ya ruzuku kwa wakulima nchini ili kuongeza uzalishaji wa mazao, kupunguza gharama ya mbolea, kulinda usalama wa chakula, kuongeza upatikanaji wa bidhaa za viwanda, kuongeza fedha za kigeni na kuimarisha upatikanaji wa ajira nchini.

Akiongea kwa niaba ya wakuu wa mikoa mwenyekiti wa wakuu wa mikoa ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongela amesema kuwa suala la wakulima ni sehemu ya jukumu lao na hivyo watalitekeleza kama ilivyoagizwa.

Sisi kama unavyotuona hii ni sehemu ya wajibu wetu, kwa niaba ya wenzangu nikuhakikishie hatuwezi kurudi nyuma tunaunga mkono hii kazi na tunaenda kuitekeleza kama inavyotakiwa” alisema Mhe. Mongela.

Kikao kazi hicho cha siku moja kilikuwa na lengo la kuwakutanisha Viongozi hao na wizara mbili ili kuona namna ya kumsaidia mkulima nchini na kukuza ustawi wa uchumi wa mazao kwa ujumla.

 

Chanzo: www.tamisemi.go.tz

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.