SAKATA LA FAMILIA YA MAREHEMU RICHARD BUKOMBE LACHUKUA SURA MPYA

Na Rhoda Simba, Dodoma

 

SAKATA la ndugu wa marehemu Richard Bukombe mkazi wa Miyuji jijini Dodoma aliyefariki dunia kwa kile kinachodaiwa kugongwa na gari mali ya jeshi la Magereza limechukua sura mpya baada ya wanafamilia kumtaka Mkuu wa Jeshi la Magereza, kutowakingia kifua waliohusika.

 


 

Aidha, wameiomba Tume ya Haki za Binadamu pamoja na Kituo cha Haki za Binadamu na Msaada wa Kisheria (LHRC) kuingilia kati sakata hilo ili kifo cha ndugu yao kipatiwe haki.

 

Akizungumza na waandishi wa habari  jijini hapa kwa niaba ya familia mdogo wa marehemu Bukombe Bulole, alisema pamoja na kuzika mwili wa ndugu yao bado hawata kata tamaa ya kupata haki ya ndugu yao.

 

Amesema baada ya kuuzika mwili wa marehemu walifuatilia katika hospitali ya rufaani ya mkoa wa Dodoma ambapo ilibainika kuwa mwili wa ndugu yao uliletwa na kutelekezwa katika chumba cha kuhifadhia maiti na askari wa Jeshi la Magereza.

 

“Kamishna anapaswa kulifanyia kazi hili kwani lipo mikononi mwake asiwape kazi viongozi wake wa juu kwa ajili ya kuwalinda wahahusika, tunamuomba sana atusaidie hakuna haja sisi kumfuata waziri mkuu au Rais Samia Suluhu Hassan afanye kitu ambacho ni jukumu la mteule wake”amesema Bukombe

 

Amesema kuendelea kukaa kimya kwa jeshi la Magereza kunazidi kuwapa hofu kuwa ndugu yao alipogongwa na gari hakuwa amekufa bali wao ndiyo waliomalizia ili kuondoa ushahidi.

 

“Ndugu wanahabari sheria ya usalama barabarani kifungu cha 57 ii b kinamtaka mtu yeyote atakaye sababisha ajali aripoti kituo cha polisi ndani ya saa 12 ila sheria itamsamehe akichelewa endapo kutokana na ajali hiyo atakuwa hawezi kutimiza takwa la sheria hiyo.

 

“Lakini pia kifungu cha 40 sura ya168 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 inasema kwamba mtu yeyote atakayesababisha majeruhi au kifo kwa mujibu wa sheria ya usalama barabarani atakuwa ametenda kosa la jinai”amesema

 

Amesema kwakuwa askari Magereza ni miongoni mwa vyombo vinavyohakikisha sheria ya nchi haivunjwi na kwa kutoripoti ajali ile kituo cha polisi wamevunja sheria.

 

“Hivyo askari Magereza ambao ni wasimamizi wa sheria za nchi wametenda kosa la jinai na tunawaomba viongozi wao wawafikishe mahakamani mara moja bila kusumbua vyombo vingine vya usalama kuchunguza jambo hilo”amesisitiza Bukombe

 

Vilevile, alisema familia inamuomba Kamishna wa Magereza aige mfano wa Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu Sera,Bunge na Uratibu George Simbachawene alivyoruhusu sheria ifuate mkondo wake kwa mtoto wake ambaye alivunja sheria za nchi.

 

Bukombe, alisema toka ajali imetokea Septemba 13, mwaka huu hadi leo hii ni zaidi ya siku 14, zimepita bila kuona chochote kilichofanywa na Magereza zaidi ya danadana za kivuta muda ili wasahau na kuacha kufuatilia jambo hilo.   

 

Marehemu Richard Bukombe, maarufu kwa jina la Baba Paroko anadaiwa kugongwa na gari mali ya Jeshi la Magereza (Land cruzer pick up) Septemba 13, mwaka huu jirani na eneo la Twiga hotel Msalato jijini hapa.

 

Kwa mujibu wa ndugu zake wanadai aligongwa na gari hilo mali ya Magereza majira ya saa 12:30 jioni ambapo baadhi ya askari wa jeshi hilo walimchukua na kuondoka naye na baadaye mwili wake kukutwa umetelekezwa mochwari.

 

Mkuu wa Jeshi la Magereza mkoa wa Dodoma Kenneth Mwambije, alipoulizwa kuhusu tukio hilo alikiri kuwa analifahamu kama ambavyo watu wengine wanavyolisikia lakini akasisitiza kuwa watu wa kulitolea ufafanuzi ni makao makuu ya Jeshi hilo.

 

Wiki iliyopita Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Yussuf Hamad Masauni, alipoulizwa kuhusu tukio hilo alisema anaomba kwanza kukutana na wanafamilia hao ili kusikiliza malalamiko yao.

 

Mwisho

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.