RAIS SAMIA AAGIZA WALIOTUMIA VIBAYA FEDHA ZA LISHE KUCHUKULIWA HATUA

 

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amemuagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI kuwachukulia hatua wale wote waliotumia vibaya fedha za lishe na kukwamisha malengo ya serikali katika kukabiliana na changamoto za lishe nchini.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali, Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala pamoja na Watumishi wa Serikali mara baada ya kuweka saini Mikataba ya Usimamiaji wa Shughuli za Lishe


Agizo hilo alilitoa alipokuwa akihutubia halfa ya utiaji saini mkataba wa usimamiaji wa shughuli za lishe tukio lililofanyika katika ukumbi wa kisasa wa mikutano wa jengo la kitega uchumi la Halmashauri ya Jiji la Dodoma lililopo Mji wa serikali Mtumba jijini hapa.

Rais Samia alisema “nakuagiza Waziri wa TAMISEMI, wote waliotumia vibaya fedha za lishe au kuzitumia kwa malengo tofauti wachukuliwe hatua na ripoti yake niipate”.

Akiongelea lengo la halfa hiyo, alisema kuwa ni kutatua matatizo ya lishe nchini. “Ndugu zangu, lengo ni kutatua matatizo ya lishe yaliyopo katika maeneo yenu na hasa wanajamii, kuelimisha na kuhamasisha umma kuhusu masuala ya lishe na lishe bora kwa kutumia jumbe mbalimbali na kutoa ushauri kwa wananchi na hasa makundi yanayolengwa” alisema Rais Samia. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali, Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala pamoja na Watumishi wa Serikali mara baada ya kuweka saini Mikataba ya Usimamiaji wa Shughuli za Lishe


Kuhusu umuhimu wa lishe bora, alisema kuwa ni muhimu kwa jamii hasa wajawazito, watoto na wanawake walio katika umri wa uzazi, wazee, na vijana katika rika ya balehe. “Sasa ukitizama tunaanza na wajawazito kuwapa lishe bora ili watoe watoto wenye afya. Lakini mtoto mwenye afya akisha kuzaliwa tunahitaji kumtunza mtoto huyo nae akifika umri, akiitwa balehe anahitaji kutunzwa pia. Anahitaji kutunzwa ili kama ni mwanamke au mwanaume waje wazae pia watoto wenye afya. Sasa tuangalie ulimwengu wetu sasa hivi. Mama mjamzito tunahangaika nae, watoto wakishazaliwa hawawezi kujisaidia, inaeleweka lazima tuwatunze, watoto balehe. Hebu tufanye utafiti tunakosea wapi? Kwa nini wanakuwa na lishe mbovu?

Kwa nini kunakuwa na changamoto ya lishe, je ni mitindo ya maisha nataka niwe ‘sixpacks’, nataka sijui niwe ‘slim’, nisizidi kilo ngapi…wakifika wakati wa kuwajibika kuja kuzaa kuongeza ‘society’ wanahangaika. Mara supu ya pweza…Tunatatizo na mnalijua mnalificha. Watafiti fanyeni utafiti. Tunatatizo na tatizo hili kwa sababu halisemwi ni siri linaumiza zaidi vijana wetu, mara ndo udongo wa kongo…tatizo kubwa liko kwenye lishe” alisisitiza Rais Samia.

Akiongelea ukubwa wa tatizo la lishe, Rais Samia alisema kuwa matokeo yake ni kuwa na taifa goigoi. “Nasema haya kwa sababu nilishasema kwamba tukiacha hali hii tunaenda kuwa na taifa goigoi. Tunaenda kuwa na taifa lenye watu na si rasilimali watu, ni watu ambao ni mzigo kwa taifa siyo watu ambao watazalisha kwa ajili ya taifa. Kuzalisha mali, kusimamia uchumi, lakini pia kuzalisha watu ili taifa hili liendelee, tutafika pahali hapa hatumjui mke nani mume nani” alisema Rais Samia kwa masikitiko.

Akimkaribisha Rais Samia kuhutubia, waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Innocent Bashungwa alianza kwa kuipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa ujenzi wa ukumbi bora na wa kisasa kwa hadhi ya makao makuu. “Ukumbi huu ni bora na unapendeza na tupo hapa ‘very confortable’. Tuwapongeze sana wenzetu upande wa Jiji la Dodoma” alisema Bashungwa.

Akiongelea shughuli ya tathmini ya 6 ya utekelezaji wa mkataba wa lishe alisema kuwa mkataba huo ni utekelezaji wa agizo la Rais. “Utekelezaji huu uliuasisi mwenyewe mwaka 2017/2018 na ulielekeza usimamizi na utekelezaji wa shughuli za mkataba wa lishe ufanywe na waheshimiwa wakuu wa mikoa” alisema Bashungwa.

 


MWISHO

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.