Na Mwandishi wetu-Dodoma
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu ) Mhe.
Ummy Nderiananga amepokea vifaa vya mawasiliano vitakavyotumika katika
kukabiliana na maafa mbalimbali hapa nchini ambavyo ni Ndege zisizo na
Rubani (Drones) vyenye thamani ya shilingi Milioni 102,741,400
vilivyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani
(WFP).
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo yaliyofanyika katika
Ukumbi wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma Mhe. Ummy alisema vifaa hivyo
vitawezesha Ofisi ya waziri mkuu kutekeleza shughuli za uratibu na
udhibiti wa maafa mbalimbali hasa katika kuchukua taarifa
katika picha ili kupata majanga na madhara pindi yanapotokea katika
nyanja za sekta na taasisi za serikali.
Mhe. Ummy alieleza kwamba vifaa hivyo ni muhimu kwa kuzingatia
jukumu kuu la Ofisi ya Waziri Mkuu ambalo ni Uratibu wa shughuli za Serikali
na uratibu wa shughuli za maafa na taasisi zisizo za kiserikali kwa njia
ya mtandao.
“Kwa niaba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tunaishukuru WFP
binafsi na shirika la WFP kwa kutupatia vifaa hivi muhimu kwa ajili ya
kuimarisha mawasiliano kwa njia ya mtandao, kufanya operesheni za utafutaji na
uokoaji, kupata ramani za hatari zilizopo, uwezekano wa kuathiriwa na janga na
uwezo wa jamii husika,”Alisema Mhe. Ummy.
Aidha aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe.
Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kushirikiana na Mashirika mbalimbali ya
Umoja wa Mataifa ambayo yamekuwa yakiiunga mkono Serikali katika miradi ya
maendeleo kwa manufaa ya wananchi na Taifa.
Awali akimkaribisha Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu
(Sera, Bunge na Uratibu ) Mhe. Ummy Nderiananga, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Dkt.
John Jingu alibainisha kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu iko tayari
kushirikiana na (WFP) kwa kila eneo ambalo watahitaji ushirikiano huku
akiahidi vifaa hivyo kutumika kama ilivyokusudiwa.
“Tunakumbana na maafa mengi na huwa inachukuwa mda mrefu
kwa waokozi au upataji wa taarifa unachelewa hivyo,kwaajili ya hizi drone
naamini ufanyaji kazi na upatikanaji wa uhalisia wa tukio utapatikana kwa
uraisi”.
Aidha Mkurugenzi Mkazi Shirika la Mpango wa Chakula
Duniani (WFP) Bi. Sarah Gibson alifafanua kuwa mradi huo ni endelevu kwa
miaka mitano kuanzia Julai 2022 hadi Juni 2027 na kwamba Shirika litafanya kazi
zake kulingana na viupembeel vya serikali na kuwekeza katika kilimo, elimu,
maafa pamoja na wakimbizi.
Comments
Post a Comment