Kwa mara ya kwanza JKCI yafanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa kufungua tundu dogo kwenye kifua (Minimal Invasive Surgery)
Na: Genofeva Matemu – Dar es Salaam
26/08/2022 Kwa mara ya kwanza Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na madaktari kutoka Hospitali ya
King Faisal Specialist iliyopo nchini Saud Arabia chini ya Taasisi ya Muslim
World League wamefanya upasuaji maalum wa kufungua tundo dogo (minimal invasive
surgery) kwenye kifua na kufanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa wagonjwa watatu
katika kambi maalum ya matibabu ya siku sita.
Akizungumza na waandishi wa habari
kuhusu kambi hiyo iliyomalizika mwishoni wa wiki Mkurugenzi wa Kurugenzi ya
Upasuaji wa Moyo wa JKCI Dkt. Angela Muhozya alisema kuwa katika upasuaji huo
wanawake wanafanyiwa upasuaji chini ya ziwa na kwa wanaume upasuaji unafanyika
pembeni karibu na kwapa.
“Kwetu sisi wataalam wa JKCI huu ni
upasuaji wetu wa kwanza tumefanya wa kufungua tundu dogo kwenye kifua (minimal
invasive surgery) na moja ya malengo yetu ni kuongeza utaalam kila baada ya
muda, tumekusudia mwaka huu tuanze kufanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa kufungua
kifua kwa sehemu ndogo kwasababu ndio upasuaji wa viwango vya juu kwa sasa
duniani”,
“Tumejifunza hatua za awali, tumejua
vifaa gani vinahitajika, maandalizi ya aina gani ya ziada yafanyike kwa
wagonjwa na pia baada ya upasuaji tumejifunza ni jinsi gani tunapaswa
kuwahudumia wagonjwa hao, upasuaji wa moyo siyo lazima uwe na mshono mkubwa,
unakuwa na mshono kidogo, maumivu kidogo na unapona haraka”, alisema Dkt.
Angela
Akizungumzia idadi ya wagonjwa
waliofanyiwa upasuaji katika kambi hiyo Dkt. Angela alisema kuwa jumla ya wagonjwa
15 ambao walihitaji kubadilishiwa milango ya moyo, kupandikiza mishipa na
kubadilisha mshipa mkubwa wa moyo (aneurysm repair) wamefanyiwa upasuaji.
“Wagonjwa 8 walifanyiwa upasuaj wa
kubadilishiwa milango ya moyo ambapo kati yao wagonjwa 3 walifanyiwa upasuaji
mkubwa wa moyo kwa kufungua kifua sehemu ndogo chini ya ziwa ambapo wagonjwa
hao walitoka chumba cha uangalizi maalumu ICU baada ya siku moja na kwenda
wodini wakiwa na kidonda kidogo sana”, alisema Dkt. Angela.
Dkt. Angela alisema wagonjwa wengine 5
walifanyiwa upasuaji wa kupandikiza mishipa (bypass surgery) zaidi ya mitatu kwa
njia ya kawaida kutokana na matatizo yao kuwa makubwa hivyo kukosa nafasi ya
kufunguliwa tundu dogo ambapo wagonjwa 3 walifanyiwa upasuaji bila ya
kuusimamisha moyo na wawili walifanyiwa upasuaji kwa kuusimamisha moyo.
“Wagonjwa wawili wamefanyiwa upasuaji
mkubwa wa moyo wa kubadilisha mshipa mkubwa wa moyo (aneurysm repair) na hadi
sasa wagonjwa wote wanaendelea vizuri na wengine wameshatoka katika chumba cha
uangalizi maalum (ICU) wamerudishwa wodini”, aliasema Dkt. Angela
Aidha Dkt. Angela amewataka wananchi
kujiwekea utaratibu wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili wanapokuwa
na tatizo la moyo liweze kugundulika
mapema kwani tatizo linapojulikana mapema matibabu huwa rahisi kufanyika kwa
wakati hivyo kuwezesha kupata matokeo
mazuri zaidi na maisha bora baada ya
upasuaji .
Kwa upande wake Daktari bingwa wa
upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka Hospitali ya King Faisal Specialist iliyopo
Nchini Saud Arabia chini ya Taasisi ya Muslim World League Ali Haneef alisema
kuwa madaktari wa Saud Arabia wamekua wakishirikiana na madaktari wa JKCI mara kwa
mara ambapo katika kambi hiyo wamekuja na mbinu mpya ya upasuaji wa moyo wa
kufungua tundu dogo katika upasuaji mkubwa wa moyo.
“Tunaendeleza lengo letu la
kuwasaidia wagonjwa wa moyo lakini pia kubadilishana uzoefu na wataalam wenzetu
wa hapa JKCI ambapo katika kambi hii tumewafundisha mbinu mpya ya upasuaji wa
moyo kwa kufungua sehemu ndogo ya kifua na kufanya upasuaji mkubwa mbinu ambayo
inarahishisha matibabu na mgonjwa anapona haraka”,
“Wataalam wa JKCI wanaendelea kupanda
viwango kwani hapo awali ilitulazimu kuja kundi kubwa la wataalam wa maeneo
yote kuanzia madaktari wa usingizi, wauguzi wa chumba cha upasuaji na ICU na
madaktari wa upasuaji lakini katika kambi hii tumekuja wataalam wachache
kwasababu uzoefu tuliobadilishana nao umeleta matokeo chanya sasa tunafanya kwa
pamoja”, alisema Dkt. Ali
Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Muslim
World League nchini Tanzania Hassan Katungunya ameishukuru Serikali ya Tanzania
kwa ushirikiano ambao wanautoa kufanikisha ujio wa wataalam hao kutoka nchini
Saud Arabia kwa ajili ya kutoa ujuzi na matibabu kwa watanzania.
“Naishukuru Serikali ya Tanzania kwa
ushirikiano mliotupatia, lakini pia nawashukuru wataalam wa afya waliotoka Saud
Arabia kwa kufanikisha zoezi la kuwasaidia watanzania wenye uhitaji wa
kufanyiwa upasuaji wa moyo lakini pia kuwaongezea wataalamu wetu ujuzi” alisema
Hassan
Comments
Post a Comment