Kwa mara ya kwanza JKCI yafanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa kufungua tundu dogo kwenye kifua (Minimal Invasive Surgery)

Na: Genofeva Matemu – Dar es Salaam

26/08/2022 Kwa mara ya kwanza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na madaktari kutoka Hospitali ya King Faisal Specialist iliyopo nchini Saud Arabia chini ya Taasisi ya Muslim World League wamefanya upasuaji maalum wa kufungua tundo dogo (minimal invasive surgery) kwenye kifua na kufanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa wagonjwa watatu katika kambi maalum ya matibabu ya siku sita.

Madaktari bingwa wa upasuaji mkubwa wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya King Faisal Specialist iliyopo nchini Saud Arabia kumfanyia upasuaji wa kupandikiza mishipa ya damu (Bypass Surgery) mgonjwa wakati wa kambi maalum ya siku 6 ya matibabu ya moyo iliyofanyika katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini Dar es Salaam


Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kambi hiyo iliyomalizika mwishoni wa wiki Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Upasuaji wa Moyo wa JKCI Dkt. Angela Muhozya alisema kuwa katika upasuaji huo wanawake wanafanyiwa upasuaji chini ya ziwa na kwa wanaume upasuaji unafanyika pembeni karibu na kwapa.

“Kwetu sisi wataalam wa JKCI huu ni upasuaji wetu wa kwanza tumefanya wa kufungua tundu dogo kwenye kifua (minimal invasive surgery) na moja ya malengo yetu ni kuongeza utaalam kila baada ya muda, tumekusudia mwaka huu tuanze kufanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa kufungua kifua kwa sehemu ndogo kwasababu ndio upasuaji wa viwango vya juu kwa sasa duniani”,

“Tumejifunza hatua za awali, tumejua vifaa gani vinahitajika, maandalizi ya aina gani ya ziada yafanyike kwa wagonjwa na pia baada ya upasuaji tumejifunza ni jinsi gani tunapaswa kuwahudumia wagonjwa hao, upasuaji wa moyo siyo lazima uwe na mshono mkubwa, unakuwa na mshono kidogo, maumivu kidogo na unapona haraka”, alisema Dkt. Angela

Akizungumzia idadi ya wagonjwa waliofanyiwa upasuaji katika kambi hiyo Dkt. Angela alisema kuwa jumla ya wagonjwa 15 ambao walihitaji kubadilishiwa milango ya moyo, kupandikiza mishipa na kubadilisha mshipa mkubwa wa moyo (aneurysm repair) wamefanyiwa upasuaji.

“Wagonjwa 8 walifanyiwa upasuaj wa kubadilishiwa milango ya moyo ambapo kati yao wagonjwa 3 walifanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo kwa kufungua kifua sehemu ndogo chini ya ziwa ambapo wagonjwa hao walitoka chumba cha uangalizi maalumu ICU baada ya siku moja na kwenda wodini wakiwa na kidonda kidogo sana”, alisema Dkt. Angela.

Madaktari bingwa wa upasuaji mkubwa wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya King Faisal Specialist iliyopo nchini Saud Arabia kumfanyia upasuaji wa kubadilisha mshipa mkubwa wa moyo (aneurysm repair) mgonjwa wakati wa kambi maalum ya siku 6 ya matibabu ya moyo iliyofanyika katika Taasisi hiyo iliyopo Jijini Dar es Salaam


Dkt. Angela alisema wagonjwa wengine 5 walifanyiwa upasuaji wa kupandikiza mishipa (bypass surgery) zaidi ya mitatu kwa njia ya kawaida kutokana na matatizo yao kuwa makubwa hivyo kukosa nafasi ya kufunguliwa tundu dogo ambapo wagonjwa 3 walifanyiwa upasuaji bila ya kuusimamisha moyo na wawili walifanyiwa upasuaji kwa kuusimamisha moyo.

“Wagonjwa wawili wamefanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo wa kubadilisha mshipa mkubwa wa moyo (aneurysm repair) na hadi sasa wagonjwa wote wanaendelea vizuri na wengine wameshatoka katika chumba cha uangalizi maalum (ICU) wamerudishwa wodini”, aliasema Dkt. Angela

Aidha Dkt. Angela amewataka wananchi kujiwekea utaratibu wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili wanapokuwa na tatizo la moyo liweze  kugundulika mapema kwani tatizo linapojulikana mapema matibabu huwa rahisi kufanyika kwa wakati hivyo kuwezesha  kupata matokeo mazuri zaidi  na maisha bora baada ya upasuaji .

Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka Hospitali ya King Faisal Specialist iliyopo Nchini Saud Arabia chini ya Taasisi ya Muslim World League Ali Haneef alisema kuwa madaktari wa Saud Arabia wamekua wakishirikiana na madaktari wa JKCI mara kwa mara ambapo katika kambi hiyo wamekuja na mbinu mpya ya upasuaji wa moyo wa kufungua tundu dogo katika upasuaji mkubwa wa moyo.

“Tunaendeleza lengo letu la kuwasaidia wagonjwa wa moyo lakini pia kubadilishana uzoefu na wataalam wenzetu wa hapa JKCI ambapo katika kambi hii tumewafundisha mbinu mpya ya upasuaji wa moyo kwa kufungua sehemu ndogo ya kifua na kufanya upasuaji mkubwa mbinu ambayo inarahishisha matibabu na mgonjwa anapona haraka”,

“Wataalam wa JKCI wanaendelea kupanda viwango kwani hapo awali ilitulazimu kuja kundi kubwa la wataalam wa maeneo yote kuanzia madaktari wa usingizi, wauguzi wa chumba cha upasuaji na ICU na madaktari wa upasuaji lakini katika kambi hii tumekuja wataalam wachache kwasababu uzoefu tuliobadilishana nao umeleta matokeo chanya sasa tunafanya kwa pamoja”, alisema Dkt. Ali

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Muslim World League nchini Tanzania Hassan Katungunya ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano ambao wanautoa kufanikisha ujio wa wataalam hao kutoka nchini Saud Arabia kwa ajili ya kutoa ujuzi na matibabu kwa watanzania.

“Naishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano mliotupatia, lakini pia nawashukuru wataalam wa afya waliotoka Saud Arabia kwa kufanikisha zoezi la kuwasaidia watanzania wenye uhitaji wa kufanyiwa upasuaji wa moyo lakini pia kuwaongezea wataalamu wetu ujuzi” alisema Hassan

 

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.