Na: Mwandishi Wetu - MWANZA
Waziri wa
Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Prof.
Joyce Ndalichako amewataka wamiliki wa viwanda nchini kutekeleza ipasavyo
sheria za kazi ikiwemo kuwapa mikataba ya kazi wafanyakazi wanaowaajiri ili
kuepukana na migogoro mahali pa kazi.
Akiongea
baada ya kufanya ziara ya kukagua utekelezaji wa sheria za kazi na Waajiri
katika maeneo ya kazi ya viwandani jijini Mwanza, Waziri Ndalichako amefafanua
kuwa suala kubwa alilobaini katika ziara hiyo kuwa wapo wafanyakazi ambao hawana
mikataba kabisa ya kazi aidha ya kudumu au ya muda mfupi.
“Wafanyakazi
wengine wameajiriwa kwa zaidi ya miaka kumi na tano lakini wanakuwa wanapewa
mkataba wa mwezi mmoja mmoja, sheria za mikataba ya wafanyakazi zinaweka wazi
juu ya aina ya kazi ambazo mfanyakazi anaweza kupewa mkataba wa kudumu au wa
muda mfupi, Mikataba mingine huandaliwa tu kwa ajili ya kutuonesha watendaji wa
serikali lakini wafanyakazi hawana nakala hizo na hata wakati wa kusaini
wafanyakazi hawajui kilichomo ndani ya hiyo mikataba,” alisema Waziri
Ndalichako
Aidha, amesisitiza kuwa suala la Usalama na Afya mahala pa kazi bado ni
changamoto katika viwanda vingi hususan katika kuwapatia vifaa kinga
wafanyakazi wakati wa shughuli za uzalishaji viwandani, hivyo amefafanua kuwa
Ofisi hiyo kupitia OSHA itaendelea kutoa elimu ili kuhakikisha sheria ya
Usalama na Afya mahala pa kazi inatekelezwa.
Mhe. Ndalichako amefafanua kuwa utekelezaji wa sheria za kazi katika viwanda
hivyo umeongezeka kwa kulinganisha na kaguzi zilizopita japokuwa bado kuna
mapungufu hususan katika kulipa michango ya wafanyakazi kwenye mifuko ya
Hifadhi ya Jamii.
“Ni wasihi
waajiri wahakikishe wanakuwa na takwimu sahihi za michango wanayowasilisha
katika mifuko ya hifadhi ya jamii, kwani idadi ya wafanyakazi wanaochangiwa
katika mfuko wa NSSF tumekuta inakuwa tofauti sambamba na michango ya mfuko wa
WCF, ikiwa idadi ya wafanyakazi walio ajiriwa ipo hivyo, mnapaswa kuhakikisha
takwimu hiyo inaoana na waliochangiwa katika mifuko ya Hifadhi ya jamii”
alieleza
Aliongeza
kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imeendelea kuvutia wawekezaji nchini
kwa lengo la kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.
Kwa upande
wake Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi akizungumza kwa niaba ya
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, amemuhakikishia Mhe. Waziri kuwa watahakikisha
wanashirikiana na watendaji wanao husika na masuala ya kusimamia sheria za kazi
mkoani humo kwa lengo la kutekeleza maagizo yake kwa wakati.
Katika hatua
nyingine, Menejimenti za Viwanda vilivyotembelewa zimeshukuru kwa ushirikiano
wanaoupata kutoka katika Taasisi za serikali hususan katika utekelezaji wa
sheria za kazi, suala ambalo huwasaidia katika uzalishaji wao kuwa wa tija.
Aidha, wameahidi kutelekeleza maagizo waliyopewa kikamilifu ili kuepukana na
migogoro katika viwanda vyao.
MWISHO
Comments
Post a Comment