Na Veronica
Simba - REA
Mkurugenzi
Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amewataka
wafanyakazi wote wa Taasisi hiyo kufanya kazi kwa weledi na kujituma ili
kufikia malengo yake ya kuboresha maisha ya wananchi vijijini kwa kuwezesha
upatikanaji wa nishati bora na zenye gharama nafuu.
Aliyasema
hayo mwishoni mwa juma, Julai 29, 2022 wakati wa kikao maalum baina yake na
wafanyakazi wa REA kilicholenga kujadili utendaji kazi, kusikiliza changamoto
za watumishi na kuzitolea majibu.
Mhandisi
Saidy aliwataka wafanyakazi wote kushirikiana na kuweka nguvu ya pamoja katika
utekelezaji wa vipaumbele vya Wakala kwa sasa, ambavyo alivibainisha kuwa ni
pamoja na kupeleka umeme vitongojini, programu ya kusaidia upatikanaji wa
petroli vijijini, mradi wa kuwezesha upatikanaji wa nishati bora ya kupikia
vijijini pamoja na kupeleka umeme katika visiwa.
Kuhusu
usambazaji umeme vitongojini, alieleza kuwa ni mradi unaolenga kuvipelekea
umeme vitongoji vyote ambavyo havijafikiwa na nishati hiyo, baada ya kila
kijiji sasa kufikiwa na mradi wa umeme.
Alifafanua
kuwa gharama ya mradi inakadiriwa kuwa shilingi trilioni 6.5 na kwamba katika
mwaka huu wa fedha, shilingi bilioni 140 zimetengwa kwa ajili ya utambuzi wa
wigo wa mradi pamoja na kuanza kazi ya utekelezaji wa mradi awamu kwa awamu.
Vilevile,
aliuelezea mradi wa kuwezesha ujenzi wa vituo vidogo vya kusambaza bidhaa za
petroli vijijini, ambapo alibainisha kuwa Serikali imeubuni ikilenga kuwezesha
na kuendeleza vituo hivyo kwa maeneo ya vijijini ambayo hayana vituo vya mafuta
kwa njia ya mkopo nafuu.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (Meza Kuu-aliyesimama), akizungumza na Wafanyakazi wa Wakala hiyo katika kikao maalumu kilichofanyika jijini Dodoma |
Alisema kuwa
mradi huo ni wa majaribio ambao ni sehemu ya jitihada za kutafuta mbinu bora
zaidi za kusambaza nishati ya mafuta salama na kwa bei nafuu vijijini.
Pia,
Mkurugenzi Mkuu alifafanua kuwa katika mwaka huu wa fedha, Serikali imetenga
shilingi milioni 500 ili kufanya kampeni ya kuhamasisha matumizi ya nishati
bora ya kupikia pamoja na kuwezesha kufanyika kwa tafiti za kubaini nishati,
mfumo sahihi na vivutio vya kusambaza nishati hiyo kwa maeneo ya vijijini.
Aliongeza
kuwa, katika mwaka wa fedha 2022/23, shilingi bilioni 10 zitatumika kutekeleza
mradi wa majaribio wa kupeleka na kusambaza gesi asilia katika makazi ya
wananchi wanaopitiwa na mkuza wa bomba kuu la gesi katika mikoa ya Mtwara,
Lindi na Pwani.
Aidha, kuhusu
kipaumbele cha nne kinachohusisha upelekaji umeme visiwani na maeneo yaliyo
mbali na Gridi ya Taifa, Mhandisi Saidy alieleza kuwa mradi unahusisha ujenzi
wa miradi midogo midogo ili kuzalisha na kusambaza umeme kutokana na vyanzo vya
nishati jadidifu kama vile jua, upepo, maporomoko madogo ya maji pamoja na
tungamotaka.
Alitaja
gharama ya mradi kuwa ni takribani shilingi bilioni 54 na kwamba katika mwaka
huu wa fedha, shilingi bilioni 20 zimetengwa kutoka Serikali ya Tanzania.
Katika hatua
nyingine, Mkurugenzi Mkuu aliwahakikishia wafanyakazi wa REA kuwa changamoto
mbalimbali zinazowakabili, zitaendelea kufanyiwa kazi ili kuzitatua na
kuwawezesha kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.
Akizungumza
kwa niaba ya Wafanyakazi, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na
Afya Tanzania (TUGHE), Tawi la REA, Swalehe Kibwana alimshukuru Mkurugenzi Mkuu
kutenga muda wa kukutana na wafanyakazi ili kuzungumza nao na kupokea
changamoto zao.
Comments
Post a Comment