MKURUGENZI MKUU REA ASISITIZA UCHAPAKAZI KWA WATUMISHI

 

Na Veronica Simba  - REA

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amewataka wafanyakazi wote wa Taasisi hiyo kufanya kazi kwa weledi na kujituma ili kufikia malengo yake ya kuboresha maisha ya wananchi vijijini kwa kuwezesha upatikanaji wa nishati bora na zenye gharama nafuu.

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (katikati), akizungumza na Wafanyakazi wa Wakala hiyo (hawapo pichani) katika kikao maalumu kilichofanyika jijini Dodoma Julai 29, 2022. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu, Adrophine Tutuba na kulia ni Mwenyekiti wa TUGHE, Tawi la REA, Swalehe Kibwana


Aliyasema hayo mwishoni mwa juma, Julai 29, 2022 wakati wa kikao maalum baina yake na wafanyakazi wa REA kilicholenga kujadili utendaji kazi, kusikiliza changamoto za watumishi na kuzitolea majibu.

Mhandisi Saidy aliwataka wafanyakazi wote kushirikiana na kuweka nguvu ya pamoja katika utekelezaji wa vipaumbele vya Wakala kwa sasa, ambavyo alivibainisha kuwa ni pamoja na kupeleka umeme vitongojini, programu ya kusaidia upatikanaji wa petroli vijijini, mradi wa kuwezesha upatikanaji wa nishati bora ya kupikia vijijini pamoja na kupeleka umeme katika visiwa.

Kuhusu usambazaji umeme vitongojini, alieleza kuwa ni mradi unaolenga kuvipelekea umeme vitongoji vyote ambavyo havijafikiwa na nishati hiyo, baada ya kila kijiji sasa kufikiwa na mradi wa umeme.

Alifafanua kuwa gharama ya mradi inakadiriwa kuwa shilingi trilioni 6.5 na kwamba katika mwaka huu wa fedha, shilingi bilioni 140 zimetengwa kwa ajili ya utambuzi wa wigo wa mradi pamoja na kuanza kazi ya utekelezaji wa mradi awamu kwa awamu.

Vilevile, aliuelezea mradi wa kuwezesha ujenzi wa vituo vidogo vya kusambaza bidhaa za petroli vijijini, ambapo alibainisha kuwa Serikali imeubuni ikilenga kuwezesha na kuendeleza vituo hivyo kwa maeneo ya vijijini ambayo hayana vituo vya mafuta kwa njia ya mkopo nafuu.

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (Meza Kuu-aliyesimama), akizungumza na Wafanyakazi wa Wakala hiyo katika kikao maalumu kilichofanyika jijini Dodoma


Alisema kuwa mradi huo ni wa majaribio ambao ni sehemu ya jitihada za kutafuta mbinu bora zaidi za kusambaza nishati ya mafuta salama na kwa bei nafuu vijijini.

Pia, Mkurugenzi Mkuu alifafanua kuwa katika mwaka huu wa fedha, Serikali imetenga shilingi milioni 500 ili kufanya kampeni ya kuhamasisha matumizi ya nishati bora ya kupikia pamoja na kuwezesha kufanyika kwa tafiti za kubaini nishati, mfumo sahihi na vivutio vya kusambaza nishati hiyo kwa maeneo ya vijijini.

Aliongeza kuwa, katika mwaka wa fedha 2022/23, shilingi bilioni 10 zitatumika kutekeleza mradi wa majaribio wa kupeleka na kusambaza gesi asilia katika makazi ya wananchi wanaopitiwa na mkuza wa bomba kuu la gesi katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani.

Aidha, kuhusu kipaumbele cha nne kinachohusisha upelekaji umeme visiwani na maeneo yaliyo mbali na Gridi ya Taifa, Mhandisi Saidy alieleza kuwa mradi unahusisha ujenzi wa miradi midogo midogo ili kuzalisha na kusambaza umeme kutokana na vyanzo vya nishati jadidifu kama vile jua, upepo, maporomoko madogo ya maji pamoja na tungamotaka.

Alitaja gharama ya mradi kuwa ni takribani shilingi bilioni 54 na kwamba katika mwaka huu wa fedha, shilingi bilioni 20 zimetengwa kutoka Serikali ya Tanzania.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Mkuu aliwahakikishia wafanyakazi wa REA kuwa changamoto mbalimbali zinazowakabili, zitaendelea kufanyiwa kazi ili kuzitatua na kuwawezesha kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza kwa niaba ya Wafanyakazi, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE), Tawi la REA, Swalehe Kibwana alimshukuru Mkurugenzi Mkuu kutenga muda wa kukutana na wafanyakazi ili kuzungumza nao na kupokea changamoto zao.

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.