Mgawo wa umeme katika vijiji 20 Ludewa wapatiwa ufumbuzi na Makamba

Waziri wa Nishati, Mhe. Januari ametoa ufumbuzi wa changamoto ya miaka mingi ya mgawo wa umeme wa masaa 12 kwa vijiji 20 katika Wilaya ya Ludewa ambavyo vimekuwa vikipata umeme kutoka kampuni ya Madope. 

 

Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba akimsikiliza mmoja wa Wananchi katika Kijiji cha Lugarawa wilayani Ludewa baada ya kufika kijijini hapo kutatua changamoto ya upatikanaji umeme

Kampuni hiyo ya Madope inayoendesha mradi huo mdogo wa umeme wa maji (MW 1.7 inaundwa na wadau mbalimbali wakiwemo Jumuiya ya Watumia Umeme Lugarawa na Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa. 

 

Changamoto hiyo ya mgawo wa umeme imetokana na waya unaotumika kusambaza umeme kuwa mdogo ukilinganisha na mahitaji ya wananchi ambao wanaotumia umeme kwa shughuli za kiuchumi kama vile kuendesha mashine za kukamulia alizeti na kukoboa na kusaga nafaka. 

 

Akizungumza na wananchi katika Kijiji cha Lugarawa wilayani humo, Waziri Makamba amesema kuwa, Serikali kupitia TANESCO imeamua kununua umeme wote unaozalishwa na kampuni hiyo baada ya kufanya mazungumzo na wadau wote wanaohusika na mradi huo pamoja na TANESCO. 

 

Amesema kuwa, kwa TANESCO kununua umeme huo kutawezesha wananchi kupata umeme wa uhakika kwani kwa sasa katika megawati 1.7 zinazozalishwa, umeme unaotumika ni 0.3 na pia kampuni hiyo ya Madope itapata mapato. 

 

Ameongeza kuwa, Wataalam wa TANESCO watafika Lugarawa tarehe 7 Agosti 2022 ili kufanya tathmini ya Miundombinu ya Usafirishaji umeme pamoja na kusaini mikataba  ya makubaliano hayo na inategemewa kuwa ifikapo mwezi wa Pili mwaka 2023 wananchi hao watakuwa wameshaanza kupata umeme wa uhakika. 

 

Mradi huo wenye wateja 3200 kwa sasa umeleta manufaa mbalimbali kwa wananchi wa Kijiji hicho ikiwemo kutoa huduma ya umeme katika vituo vya afya, shule za Sekondari 5, shule za msingi 19 na kituo kimoja cha kulelea watoto yatima. 

 

Utekelezaji wa Mradi wa umeme wa Madope umewezeshwa na wadau mbalimbali ikiwemo Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambao ulitoa shilingi Bilioni 4.5 kuendeleza mradi huo. 

 

Wananchi pamoja na viongozi katika Wilaya hiyo akiwemo Mbunge wa Ludewa,, Mhe. Joseph Kamonga wamemshukuru Waziri wa Nishati kwa kutoa ufumbuzi wa changamoto hiyo ambayo imedumu kwa muda mrefu. 

 

Akiwa wilayani humo Waziri wa Nishati ameendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia ambapo ametoa mitungi ya gesi kwa kinamama ikiwa ni mradi wa majaribio utakaofanyiwa tathmini ili Serikali itengeneze mkakati bora wa kitaifa wa namna bora ya kusambaza nishati hiyo nchini.

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.