WENYEVITI WA HALMASHAURI NCHINI WATAKIWA KUITEREMSHA BAJETI KWA WANANCHI


Na. Dennis Gondwe, DODOMA

WENYEVITI na wakurugenzi wa halmashauri nchini wametakiwa kuichambua bajeti iliyopitishwa na serikali ili wananchi katika ngazi za chini wawe na uelewa na kunufaika nayo.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), Murshid Ngeze


Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), Murshid Ngeze alipokuwa akiongea katika Mkutano wa mwaka wa ALAT tawi la Mkoa wa Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma mwishoni mwa wiki.

Ngeze alisema kuwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imepitisha bajeti ya kihistoria na ya mfano. “Ndugu zangu, bajeti hiyo imejaa fursa mbalimbali zenye manufaa kwa halmashauri zetu na wananchi wetu. Wenyeviti wote na wakurugenzi wa halmashauri ni wajibu wenu kuichambua bajeti hiyo na kuwaeleza wananchi ili fedha zitakapokuja kwenye halmashauri zetu ziweze kuwanufaisha na sisi kuzisimamia ipasavyo” alisema Ngeze.

Aidha, aliwataarifu wajumbe kuwa Mkoa wa Kagera umepata shilingi bilioni 70 kwa ajili ya kuanzisha ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba. Alishauri kuwa Mkoa wa Dodoma kujipanga kwa ufugaji huo kutokana na kutokuwa na bahari wala ziwa. Ufugaji huo ni wa kawaida na hauhitaji uwekezaji mkubwa, aliongeza.

Mwenyekiti wa ALAT Mkoa wa Dodoma, Zuberi White


Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Mwenyekiti wa ALAT Mkoa wa Dodoma, Zuberi White alisema kuwa ALAT Mkoa wa Dodoma ni wamoja na wanafanya kazi kwa ushirikiano.

Mkutano wa mwaka wa ALAT Mkoa wa Dodoma ulifanyika katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma ukitanguliwa na ziara ya siku moja ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa jijini hapo.

 

MWISHO

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.