Simbachawene: Makundi ya watu wenye ulemavu yashirikishwe katika mchakato mzima wa Sensa ya Watu na Makazi




Na Mwandishi Wetu, Dodoma. 

Serikali imesema itaendelea kuyashirikisha makundi ya watu wenye ulemavu  katika hatua mbalimbali za maandalizi na utekelezaji wa zoezi la Sensa ya Watu na Makazi linalo tarajiwa kufanyika Agosti 23,2022.

Hayo yamesemwa Juni 29,2022 jijini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu  Sera, Bunge na Uratibu George Simbachawene katika kongamano la kuwajengea uelewa watu wenye ulemavu kuhusu Sensa ya Watu na Makazi .

‘’Ushirikishwaji wa kundi la Watu Wenye Ulemavu katika mchakato mzima wa Sensa umesaidia sana katika kuimarisha maswali ya hali ya ulemavu katika Sensa, hivyo matarajio ya Serikali ni kupata takwimu bora za hali ya ulemavu katika kaya zetu ili hatimae kusaidia utungaji Sera na upangaji wa mipango na programu za maendeleo zinazogusa Watu Wenye Ulemavu kwa uhakika zaidi kuliko ilivyo hivi sasa.’’ amesema Simbachawene

Aidha, Simbachawene amesema kumekuwepo na jitihada mbalimbali za kuimarisha ukusanyaji wa takwimu za Watu Wenye Ulemavu na taasisi mbalimbali zimeonesha nia ya kufanya tafiti za kupata idadi na hali ya Watu Wenye Ulemavu ili kuelewa mahitaji yao halisi kwa lengo la kuboresha hali zao za maisha.

‘’Takwimu za Watu Wenye Ulemavu ni muhimu sana kwa kuwa ni msingi mmojawapo sio tu wa kuhakikisha ustawi wa Watu Wenye Ulemavu nchini bali pia ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya kuleta maendeleo jumuishi nchini.’’ ameongeza Simbachawene 

Wakati huo huo, amesema upatikanaji wa takwimu sahihi za msingi za Watu Wenye Ulemavu zitawezesha kutunga sera wakilishi na kusaidia kupima utekelezaji wa malengo mbalimbali ya kitaifa, kikanda na kimataifa .

‘’Kama vile Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP III) na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG) ambayo yote imeweka mkazo katika kuhakikisha Watu Wenye Ulemavu sio tu wanakuwa sehemu ya mipango ya maendeleo ya nchi bali wanapewa kila fursa za kujiendeleza katika nyanja zote za maendeleo kama wananchi wengine.’’ amesema Simbachawene

Katika hatua nyingine, Simabachawene ameiagiza Ofisi ya Taifa ya Takwimu Tanzania Bara, na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Tanzania Zanzibar kuendelea kuboresha mbinu za ukusanyaji wa taarifa hizi za hali ya ulemavu nchini,kushirikiana na taasisi mbalimbali zinazojihusisha na Watu Wenye Ulemavu kwa lengo la kuwatambua na kuwahudumia.

‘’Sambamba na kuendelea kutoa msaada wa kitaalamu kwa vyama mbalimbali vya Watu Wenye Ulemavu katika kuwajengea uwezo wa kukusanya taarifa za hali ya ulemavu nchini.’’ ameongeza Simbachawene 

Hatahivyo , amesema Ofisi za takwimu ziendelee kujumuisha maswali yanayolenga kupata taarifa za hali ya ulemavu nchini kwenye tafiti mbalimbali zinazofanywa na Ofisi hizo.


Mwisho.


Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.