Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga amewapongeza watendaji wa Wakala ya Usambazaji Maji na Usafi na Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Songwe kwa jitihada zao za kuwafikishia wananchi huduma ya maji.
Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (kushoto) akielekeza jambo alipotembelea ujenzi wa tenki la maji katika mji wa Vwawa
Mhandisi Sanga ametoa pongezi hizo hivi karibuni wakati wa ziara yake ya
kukagua miradi inayotekelezwa na RUWASA mkoani humo.
“Nimejionea kazi kubwa na nzuri inayofanywa na watendaji wetu wa
RUWASA; Meneja wa RUWASA Mkoa wa Songwe na Mameneja wako wa Wilaya mnafanya
kazi nzuri,” alisema Mhandisi Sanga.
Alisema RUWASA ilipokea miradi mingi ambayo ilikuwa haitoa maji ambapo
kwa Tanzania nzima ilikuwa takriban miradi 177 na kwamba kati ya hiyo miradi
karibu 30 ilikuwa kwenye Mkoa wa Songwe na sasa imekamilika isipokuwa mmoja
ambao nao unatarajiwa kuanza kutoa maji hivi karibuni.
“Kama ambavyo tumekuwa tukiongea miaka ya nyuma tulikuwa na miradi mingi
sana ambayo tunaita miradi chechefu takriban miradi 177 na katika mkoa huu peke
yake kulikuwa na miradi chechefu karibu 30 na tunafurahi kuona miradi takriban
yote imekwamuliwa katika mkoa huu wa Songwe umebaki mmoja tu nao unakaribia
kukamilika,” alifafanua Mhandisi Sanga.
Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Anthony
Sanga (mwenye kofia ngumu) akikagua ujenzi wa tenki la maji Kata ya Uwanjani
Wilayani unduma
Alisema ukamilishwaji wa miradi hiyo ni faraja kwa Serikali kwani
inakuwa imetimiza dhamira na ahadi yake ya kumtua mwanamke ndoo kichwani na
aliwasisitiza kuendelea na jitihada za kuwaondolea adha wananchi.
Mhandisi Sanga alisema matarajio ya Serikali ni kuhakikisha vyanzo
toshelevu vya maji vinatumika kote nchini ili kuwaondolea adha wananchi na
kwamba ziara yake mkoani humo ni hatua mojawapo ya kutazama ni vipi suala hilo
linafanikiwa.
Naye Diwani wa Kata ya Uwanjani Wilaya ya Tunduma, Kwintin Kayombo
akizungumza kwa niaba ya wananchi wake alipongeza jitihada za Wizara ya Maji
kwa harakati zote inazoendelea nazo katika kuhakikisha wanapata huduma ya
majisafi na salama.
“Kwa niaba ya wananchi hawa tumepata faraja kubwa sana baada ya kuona
mradi huu wa tenki kwenye kata yetu ambao utahudumia pia na kata zingine tatu
kwenye wilaya yetu; tunashuhudia mambo makubwa yakifanywa na Wizara ya Maji,”
alisema Kayombo.
Comments
Post a Comment