JIJI LA DODOMA KINARA MICHANGO YA ALAT

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

JUMUIYA ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) imeipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa umakini wake katika kuwasilisha michango kwa wakati jambo linaloonesha nia njema na uwajibikaji unaolenga kuifanikisha taasisi hiyo.

Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Murshid Ngeze


Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Murshid Ngeze alipokuwa akiongea katika Mkutano wa mwaka wa ALAT tawi la Mkoa wa Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma mwishoni mwa wiki.

Ngeze alisema “niishukuru Halmashauri ya Jiji la Dodoma, katika michango ya ALAT Taifa. Halmashauri hii ndiyo inaongoza ulipaji wa michango kwa wakati. Nilipokutana na Waziri wa TAMISEMI nilimshauri kumuacha Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma ili aendelee kutekeleza mipango mizuri aliyonayo kwa Jiji la Dodoma na miradi ya maendeleo”.

Aidha, aliipongeza ALAT tawi la Mkoa wa Dodoma kwa kazi nzuri. “Sasa umefika wakati ALAT Mkoa wa Dodoma kufikiria kuanzisha miradi ya kiuchumi ili tuache alama. Tufikirie miradi itakayoisaidia ALAT kuwa na mapato ya uhakika na kuachana na kutegemea mapato ya kuombaomba” alisema Ngeze.

Mwenyekiti huyo alielezea masikitiko yake kwenye halmashauri zenye migogoro na kusema kuwa inakwamisha maendeleo ya wananchi. “Mheshimiwa Rais anaona na kusikitishwa na migogoro katika halmashauri. Ameiagiza ALAT kuondoa migogoro hiyo na kuhakikisha halmashauri zinachapa kazi. Hadi sasa kuna halmashauri zipo kwenye migogoro ya kumuondoa Meya na mwenyekiti wa halmashauri, jambo linalochelewesha maendeleo ya wananchi” alisema Ngeze.

Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Mwenyekiti wa ALAT mkoa wa Dodoma, Zuberi White alisema kuwa ALAT Mkoa wa Dodoma ni wamoja na wanafanya kazi kwa ushirikiano.

Mkutano wa mwaka wa ALAT Mkoa wa Dodoma ulifanyika katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma ukitanguliwa na ziara ya siku moja ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa jijini hapo.

 



MWISHO

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.