WATUMISHI WA SERIKALI WAMSHUKURU RAIS SAMIA KUBORESHA MASLAHI YAO

Na. Moses Mpunga, DODOMA

Watumishi wa serikali mkoani Dodoma wamemshukuru na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha maslahi ya watumishi wa Umma kwa kupandisha mishahara kwa asilimia 23.3 pamoja na posho mbalimbali.



Shukrani hizo zilitolewa na Mtunza Kumbukumbu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Imelda Matofali katika hafla fupi ya kumshukuru na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuboresha maslahi ya watumishi katika ukumbi wa mikutano wa PSSSF jijini hapa.

Matofali akizungumza kwa niaba ya watunza kumbukumbu kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, alimshukuru Rais kwa kuwakumbuka watumishi wa kada za chini. Alisema kuwa Rais amewakumbuka kwa kuwaongezea mishahara pamoja na posho jambo ambalo halikuwahi kufanyika kwa muda mrefu. "Kama mnavyojua Rais wetu ni mama na sifa kubwa ya mama ni kuwakumbuka watoto wake. Hivyo, tunamshukuru sana mama kwa kutukumbuka na sisi tunamuahidi kuchapa kazi kwa nguvu zetu zote" alisema Matofali.

Akiwawakilisha Watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Afisa Mtendaji Kata ya Uhuru, Christina Mpete alimuhakikishia Rais Samia Suluhu Hassan kuwa watumishi wataongeza juhudi katika kufanya kazi na kuwa atembee kifua mbele wao wapo nyuma yake na hawatamuangusha. Alisema kuwa ongezeko hilo la mishahara na posho limeongeza morali ndani ya watumishi wa Halmashauri hiyo.

"Mama yetu tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu akulinde na akupe afya njema ili uendelee kuchapa kazi na kutuhudumia watanzania" aliongeza Mpete.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Walimu Mkoa wa Dodoma, Mwl. Samweli Malechela alisema licha ya kuongeza mishahara na posho, Rais amelipa malimbikizo mengi ya mishahara kwa watumishi ndani ya mwezi uliopita. Katika Mkoa wa Dodoma, walimu zaidi ya 2,300 walipandishwa madaraja.

Mwl. Malechela aliongeza kuwa kupanda kwa mishahara na posho kutaimarisha na kuboresha uchumi wa watumishi pamoja na watanzania kwa ujumla. Mzunguko wa fedha utakua ni mkubwa jambo litakalopelekea uchumi wa Taifa kukua pia, aliongeza.

"Licha ya mambo yote ya kuboresha maslahi ya watumishi anayoyafanya Mama Rais wetu mpendwa lakini bado miradi mikubwa inaendelea kwa kasi ileile. Kwahiyo, ni dhahiri kabisa kuwa mama anaupiga mwingi. Hivyo, ni jukumu letu kumuunga mkono kwa kufanya kazi kwa juhudi kubwa ili kuendena na kauli ya kazi iendelee" alimalizia Mwl. Malechela.

 

MWISHO

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.