Na. James Kapele na Mayanga Someke, Mahakama-Sumbawanga
Jaji Kiongozi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani leo tarehe 27 Mei, 2022 ameongoza jopo
la baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu katika hafla maalum ya kumuaga kitaaluma
Jaji mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. David Mrango aliyestaafu katika
utumishi wa umma tarehe 02 Januari 2021.
Akizungumza katika hafla
hiyo mahsusi ya kuagwa kitaaluma kwa Jaji Mrango, iliyofanyika katika ukumbi wa
Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Jaji Kiongozi, Mhe. Siyani amemshukuru
kwa utumishi wake na kuahidi kuyaenzi yote aliyoyafanya wakati wa utumishi
wake.
Naye, Jaji Mstaafu, Mhe.
David Mrango amemshukuru Mungu kwa kufikia hatua ya kustaafu kwani kazi hii
ilikuwa na ugumu wake, amewashukuru pia watumishi wa Mahakama kwa kumuwezesha
kufanya kazi yake vizuri.
“Katika muda wangu wa kazi
ndani ya Mahakama nimegundua kuwa Wahe. Majaji na Mahakimu hawawezi kufanya
kazi zao kwa ufanisi bila uwepo wa Makarani, Watendaji, Wahudumu wa Ofisi,
Madereva na hata Walinzi,” amesema Mhe. Mrango.
Akiendesha shauri dogo
maalum lililofunguliwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga na kupewa namba
1/2022, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani
alipokea hotuba nne ambazo zimezungumzia safari ya maisha ya kitaaluma ya Jaji
Mstaafu, Mhe. Mrango.
Kwa upande wake, Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu-Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Dunstan Ndunguru amesema
Mhe. Mrango ameacha alama ya kuigwa kwa watumishi wote kwani alihakikisha
malengo katika mpango mkakati wa Mahakama yanatekelezeka ipasavyo.
“Mh. Jaji Mrango alikuwa
mara nyingi akisisitiza usikilizwaji wa mashauri kwa haki na kufuata taratibu
hasa kwa watuhumiwa ambao ni wananchi wa kawaida (laymen) wasiojua sheria na
taratibu za kiufundi,” amesema Jaji Ndunguru.
Awali akiwasilisha hotuba
ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Simon Peres ambaye ni Mwendesha Mashtaka
wa Serikali mkoa wa Rukwa pamoja na mambo mengine amesema Mhe, Jaji Mstaafu
David Mrango ni moja ya Majaji ambao tasnia ya sheria itamkumbuka kwa kuwa
ameacha misingi mizuri katika wigo wa sheria huku akitoa mfano wa shauri moja
ambalo Mhe.Mrango ameacha alama katika wigo wa sheria shauri la ‘Saimon S/O
Maduhu @Buhalo & 4 others, Crim. Appeal No. 10 of 2020.’
Katika shauri hili Mhe,
Mrango alitoa hukumu kwa kusema “It is a principle of law that in any criminal
proceedings it is the charge which lays a foundation of trial. As such the
charge must contain sufficient information to enable the appellant to
understand the nature of charge he faces and what defence to put up”. Ametaja
pia mashauri mengine mengi ambayo Mhe. Mrango ameyatolea uamuzi.
Naye Wakili wa Kujitegemea
aliyesoma hotuba kwa niaba ya Chama Cha Mawakili Tanzania katika Tawi la Mbeya,
Wakili Bartazar Chambi pamoja na mambo mengine ametoa wasifu wa maisha ya
utumishi wa Mhe. Mrango huku akisisitiza kwamba, katika utumishi wake wa umma
Jaji Mrango alikuwa ni mtu wa kujali muda na kusimamia maadili ya watumishi wa
Mahakama kwa ujumla.
Wakili Chambi ameongeza
kuwa, Mhe. Mrango aliilinda kwa dhati taaluma ya sheria kwani hakutaka itumike
vibaya na watu wasio na taaluma hiyo. “Akiwa Sumbawanga alidhibiti vishoka na
mmoja wa vishoka hao ajulikanaye kwa jina la Mwakasege alifungwa gerezani.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na
baadhi ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Watumishi wa Kanda hiyo, Mkuu wa
Wilaya ya Sumbawanga, Mhe. Sebastian Waryuba aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa
Rukwa, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Chama cha
Mawakili wa kujitegemea Tawi la Mbeya na wageni wengine.
Katika hatua nyingine, Jaji
Kiongozi, Mhe. Siyani alipata fursa ya kuzungumza na Watumishi wa Mahakama katika
Kanda hiyo ambapo amesisitiza kuzingatia mambo makuu matatu ambayo ni maadili
na uadilifu katika kazi, Kanda kujiwekea mpango mkakati katika masuala ya
kupunguza mlundikano wa mashauri pamoja na matumizi ya TEHAMA na ushirikiano
katika utendaji wa kazi kwa watumishi wa ngazi zote.
Baada ya kikao hicho,
Watumishi wa hiyo wamempongeza, Mhe. Siyani kwa kuteuliwa kushika wadhifa huo
na kumtakia heri na baraka katika utendaji kazi wake.
Comments
Post a Comment