WATAALAM WA ANUANI ZA MAKAZI KUELEKEA KATA YA MBABALA KUHAMASISHA


NA. Dennis Gondwe, DODOMA

HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma kupeleka timu ya hamasa na elimu juu ya Anuani za Makazi Kata ya Mbabala ili kufanikisha zoezi hilo.

Mkurugenzi wa Jiji, Joseph Mafuru


Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Joseph Mafuru alipokuwa akijibu swali la Diwani wa Kata ya Mbabala, Paskazia Mayala aliyetaka kujua lini kata yake itapata uhamasishaji na wakazi wa kata hiyo kupata namba za makazi katika nyumba zao jana katika mkutano wa Baraza la Madiwani lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Mkurugenzi Mafuru alisema kuwa elimu ya Anuani za Makazi ilitolewa kwenye ngazi zote katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Tulipeleka waratibu kwenda kujifunza Morogoro. Waliporudi tukatoa elimu katika ngazi ya jiji, watendaji na wenyeviti wa mitaa. Lengo lilikuwa kujua nani anaendesha zoezi hilo na taratibu zake zilivyo ili kuwa na uelewa wa pamoja” alisema Mafuru.

Diwani wa Mbabala, Paskazia Mayala


Akiongelea wataalam kwenda tena Kata ya Mbabala, alisema kuwa watakwenda kesho (leo). “Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie kuwa kesho wataalam wa Anuani za Makazi watafika Kata ya Mbabala na kufanya uhamasishaji. Sasa hivi wanarudia kuhakikisha maeneo ambayo hawakufanya vizuri. Mimi naangalia taarifa za kila siku za mwenendo wa zoezi hili. Kesho watakuwepo Mbabala na kazi itafanyika kwa kiwango cha juu” alisema Mafuru kwa kujiamini.

Zoezi la uandikishaji Anuani za Makazi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma limefikia asilimia 82.3.

 

MWISHO

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.