WAZIRI JAFO APONGEZA WAFANYAKAZI OFISI YA MAKAMU WA RAIS KWA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YAO NA UTATUZI WA HOJA 11 ZA MUUNGANO
Waziri wa Nchi Ofisi ya
Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) amewapongeza wafanyakazi wa Ofisi ya
Makamu wa Rais kwa utekelezaji wa majukumu yao ikiwemo utatuzi wa hoja 11 za
Muungano ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.
Ametoa pongezi hizo
wakati akifungua Kikao cha Baraza la Wafanyakazi, Ofisi ya Makamu wa Rais cha
kupitisha Bajeji ya Utekelezaji wa Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha
2022/2023 kilichofanyika leo Machi, 2022 jijini Dodoma
Akizungumza na
wafanyakazi hao Dkt. Jafo aliwataka kuendeleza juhudi hizo ili wananchi wapate
uelewa zaidi kuhusu umuhimu wa Muungano na masuala ya Mazingira.
Pia, Dkt. Jafo alitoa
pongezi kwa wafanyakazi wa Ofisi hiyo kwa kuwajibika ipasavyo katika sekta ya
mazingira ikiwemo kusimamia kampeni mbalimbali zikiwemo ‘Soma na Mti’ ambayo
inahusisha wanafunzi ngazi ya shule za msingi hadi vyuo kupanda miti na hivyo
kuifanya nchi yetu kuwa ya kijani.
“Kikubwa zaidi niwape
moyo watumishi mmefanya kazi nzuri sana, sasa twendeni na spirit (moyo)
tuendeleze upendo tulio nao maana bila upendo hakutakuwa na mafanikio,”
alisisitiza Jafo.
Waziri huyo alisema
vikao vya Baraza la Wafanyakazi ni muhimu katika kujadili masuala mbalimbali ya
wafanyakazi kwa upana kwa kuzingatia haki, weledi ikiwa ni pamoja na
kujadiliana changamoto za kiutendaji na hatua za kukabiliana nazo.
Aliongeza kuwa vikao
hivyo vinalenga kudumisha utamaduni wa kufanya kazi kwa pamoja, bidii na
maarifa ili kuleta ufanisi katika kutekeleza majukumu ya Ofisi na Taifa kwa
ujumla.
Hivyo aliwataka
wafanyakazi kujadili suala la Bajeti kwa kina na ikiwa zipo changamoto
zilizobainishwa mwaka wa fedha uliopita zijadiliwe ili ziweze kutafutiwa
ufumbuzi ili kurahisisha Utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka wa fedha ujao.
“Ninaamini Bajeti hii
imejikita katika kuwezesha, kudumisha Muungano wetu na imezingiatia masuala ya
uhifadhi wa mazingira yetu unaosimiwa na Ofisi hii na pia niwaombe wajumbe
boresheni utendaji kazi ili Ofisi hii iwe mfano wa Taasisi na Wizara zote
katika utekelezaji wa majukumu yetu kwa kuzingatia umuhimu wa Ofisi hii,”
alisisitiza Jafo.
Comments
Post a Comment