Na: Mwandishi
wetu - Kilimanjaro
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce
Ndalichako amepongeza uwekezaji kati ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi
wa Umma (PSSSF) pamoja na Jeshi la Magereza Tanzania kwa hatua nzuri ya
ukamilishaji wa kiwanda cha uzalishaji bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro
(Kilimanjaro International Leather Industries Co. Ltd).
Waziri Ndalichako ametoa pongezi
hizo Februari 26, 2022 baada ya kupokea taarifa ya maendeleo ya utekelezaji wa
mradi wa ujenzi wa kiwanda cha bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro wakati
alipotembelea kiwanda hicho kwa lengo la kukagua maendeleo ya kiwanda na
kuangalia namna ya uzalishaji wa bidhaa.
Alisema kuwa, amefurahishwa na
uwekezaji katika kiwanda hicho ambacho kitatoa ajira nyingi kwa vijana pamoja
na kuchangia ukuaji wa pato la Taifa kupitia bidhaa zitakazo kuwa zinazalishwa
na kiwanda hicho.
“Kiwanda kimefikia hatua nzuri na
Mashine zote zimeshafika, hatua inayoendela ni kuziunganisha mashine hizo ili
uzalishaji uendelee kufanyika wanatengeneza. Viatu vinavyotengenezwa hapa ni
vizuri na wanatengeneza viatu vyenye mitindo ya aina mbalimbali,” aliema Prof.
Ndalichako.
Aliongeza kuwa, uwepo wa Kiwanda
cha bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro kitachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza
tatizo la ajira nchini mara tu baada ya kukamilika kwa kiwanda hicho.
“Kiwanda kinauwezo wa kuajiri watu
zaidi ya 10,000 ambapo ajira za moja kwa moja ni 3,000 pamoja na ajira zaidi
kwa watanzania kutokana na fursa mbalimbali zitakazo kuwepo kiwanda hapo,”
alisema
Aidha, Waziri Ndalichako aliwasihi
watendaji wa kiwanda hicho kuhakikisha malengo ya uzalishaji katika kiwanda
yanazingatiwa ili fedha zilizowekezwa zitumike kwa matokeo
yaliyokusudiwa.
Sambamba na hayo amewapongeza
Uongozi wa Chuo cha VETA pamoja na Taasisi ya Teknolojia Dar es salaam (DIT)
kwa kutoa mafunzo bora kwa vijana ya utengenezaji wa bidhaa za Ngozi, huku
akibainisha kuwa vijana wanaotoka katika vyuo hivyo wamekuwa watengenezaji
wazuri wa viatu. Hivyo alitoa wito vijana kuchangamkia sekta ya Ngozi kwa kuwa
serikali imeanza kuwekeza katika kiwanda cha Ngozi na kutakuwa na uhitaji wa
rasilimali watu.
Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa
Kiwanda cha bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro, Mhandisi. Masud Omary ameeleza
kuwa menejimenti ya kiwanda hicho imejipanga kuendelea kukuza masoko ya bidhaa
zinazozalishwa kiwandani hapo ili kuhamasisha wananchi kununua bidhaa hizo. Pia
alieleza juhudi zinazofanywa na kiwanda katika kukuza soko la bidhaa nje ya
nchi.
MWISHO
Comments
Post a Comment