Serikali imeombwa kuingiza matibabu
ya magonjwa yasiyoambukiza katika bima ya afya kwa wote ili kupunguza
changamoto zinazowapata watu wanaoishi na magonjwa yasiyoambukiza kwani
tathmini iliyofanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO) inaonesha zaidi ya asilimia
45 ya vifo vinavyotokea duniani hutokana na magonjwa hayo.
Ombi hili limetolewa hivi karibuni
na Katibu wa Shirikisho la Vyama vya magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA)
Prof. Kaushik Ramaiya wakati wa uzinduzi wa mkakati wa utetezi juu ya bima ya afya
kwa watu wote inayojumuisha magonjwa yasiyoambukiza uliofanyika katika Hoteli
ya Protea jijini Dar es Salaam.
Prof. Ramaiya alisema mfuko wa
Taifa wa bima ya afya una bima za aina mbalimbali ambazo zimekuwa zikitoa
huduma za matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza pamoja na magonjwa mengine,
lakini baadhi ya huduma za matibabu hazipatikani katika bima hizo na
hivyo kuwanyima fursa wagonjwa kupata huduma iliyokamilia wanapofika
hospitali kupata matibabu.
“Magonjwa yasiyoambukiza
yanagharama kubwa katika kuyatibu, kupitia mfuko wa Taifa wa bima ya afya
wananchi wamekuwa wakikata bima za afya za aina mbalimbali lakini kadi hizo
zimekuwa zikitoa baadhi ya huduma, na huduma nyingine kama dawa, upasuaji na
vifaa kutokuwepo katika bima hivyo kuwanyima fursa wagonjwa ya kupata matibabu
kamili”,.
“Ninaiomba Serikali iliangalie hili
kwani tathmini iliyofanywa na WHO inaonesha baada ya miaka mitano hadi kumi
ijayo vifo vinavyotokana na magonjwa yasiyoambukiza vinaweza kuongezeka na kuwa
zaidi ya asilimia 55”,
“Magonjwa yasiyoambukiza
yasipotibiwa vizuri hupelekea mtu kupata madhara mengine kama vile kudhuru
figo, mishipa ya damu, macho, kupata kiharusi na madhara mengine mengi ambayo
humsababishia mtu kupoteza uhai wake”, alisema Prof. Ramaiya.
Aidha Prof. Ramaiya aliiomba
Serikali kuratibu upatikanaji wa matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza katika
maeneo yote yenye zahanati na vituo vya afya ili jamii iweze kupata huduma
maeneo ya karibu na kwa wakati hivyo kupunguza madhara yanayoweza kutokea kama
magonjwa hayo hayatatibiwa mapema.
“Kama wagonjwa wenye magonjwa
yasiyoambukiza watapata huduma za matibabu kwa wakati katika vituo vya karibu
vya afya wataweza kuendelea na shughuli zao za kiuchumi hivyo kukuza vipato
vyao na pato la taifa”,.
“Jamii inapaswa kujikinga na magonjwa
haya yasiyoambukiza kwani utafiti uliofanywa na WHO unaonesha kila dola moja
unayoiweka katika kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza unapata nafuu ya dola
7 hadi 12 kwa kila dola uliyotumia kuwekeza katika kinga”, alisema Prof.
Ramaiya
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la
Mbozi Mkoa wa Songwe Mhe. George Mwenisongole alisema suala la bima ya afya kwa
wote likawe ajenda ya kitaifa ili kutoa fursa kwa kila mtanzania kuwa na
matumaini ya kupata matibabu pale wanapougua magonjwa mbalimbali.
“Bima ya afya kwa wote inapaswa
kuwa bima isiyobagua lakini bima inayotoa huduma zote za matibabu ili
watanzania wafaidike na huduma za matibabu hasa wale wenye magonjwa
yasiyoambukiza ambayo yamekuwa yakitibiwa kwa gharama kubwa”,
“Nimepata nafasi ya kushiriki
semina iliyoandaliwa na TANCDA na kujifunza mengi kuhusiana na magonjwa
yasiyoambukiza, wito wangu kwa Serikali ni kuhakikisha tunapata sera ya kitaifa
ya kupambana na magonjwa yasiyoambukiza ambayo itaweza kuzuia uvutaji wa sigara
hadharani ili kuokoa maisha ya watu wanaoathirika na moshi wa sigara”, alisema
Mhe. Mwenisongole
Naye Mhariri wa Makala kutoka
gazeti la Habarileo Gloria Tesha aliiomba Serikali iwekeze katika elimu ya
magonjwa yasiyoambukiza kuanzia ngazi ya shule za msingi ili watoto wanapokuwa
wawe na ufahamu wa kutosha juu ya magonjwa hayo, hii itawasaidia kujikinga na
magonjwa hayo.
“Waandishi wa habari tupo tayari
kutumia kalamu zetu kupaza sauti ili jamii ifahamu athari za magonjwa
yasiyoambukiza na namna ambavyo itaweza kujikinga na magonjwa hayo. Ninaiomba
Serikali pamoja na taasisi zinazojihusisha na mapambano dhidi ya magonjwa
yasiyoambukiza kututumia ili tuweze kuzifikia jamii na kuziokoa”,
“Wadau na Serikali kwa pamoja
tukubaliane kupiga vita magonjwa yasiyoambukiza kwa kuyafanya magonjwa haya
kuwa ajenda ya kitaifa katika kila kikao kinachofanyika kuanzia ngazi za mitaa,
kata, wilaya na mikoa ajenda hiyo ikipewe kipaumbele ninaamini tutaweza
kupunguza ama kuyaondoa kabisa magonjwa haya”, alisema Gloria.
Uzinduzi wa mkakati wa utetezi juu
ya bima ya afya kwa watu wote inayojumuisha magonjwa yasiyoambukiza uliandaliwa
na Shirikisho la Vyama vya magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) na
kushirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wizara ya Afya, wajumbe wa kamati
ya kudumu ya bunge ya masuala ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Dawa za kulevya na
Magonjwa yasiyoambukiza, Kamati ya kudumu ya bunge ya huduma na maendeleo ya
jamii, watu wanaoishi na magonjwa yasiyoambukiza na wahariri wa habari .
Mwisho
Comments
Post a Comment