SERIKALI YAAHIDI KULINDA NA KUSIMAMIA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU

Na. Mwandishi Wetu - Dodoma

Serikali imeahidi kuendelea kusimamia na kulinda haki za Watu wenye Ulemavu nchini ili kuwezesha kundi hilo kuwa na ustawi mzuri katika nyanja mbalimbali. 

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi akizungumza wakati wa kufunga kikao cha Kurekebisha Mpango Kazi wa Taifa kwa Watu Wenye Ualbino kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano Dodoma Hotel


Kauli hiyo imetolewa Februari 25, 2022 na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Patrobas Katambi wakati akifunga Kikao cha Kurekebisha Mpango Kazi wa Taifa kwa Watu Wenye Ualbino 2022/2023 - 2026/2027 (National Action Plan for Persons with Albinisms - NAP) kilichofanyika Dodoma Hotel, Jijini Dodoma.

Naibu Waziri Katambi alieleza kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kushirikiana na wadau wanaotoa huduma kwa Watu wenye Ulemavu ili kuhakikisha utekelezaji wa Sera, Sheria, Miongozo na Mikataba ya Kimataifa ambapo utekelezaji wake utasaidia jamii kutambua haki na wajibu wa Watu wenye Ulemavu.

“Kwa muda mrefu kundi la Watu wenye Ualbino limekuwa katika wakati mgumu wa kufanyiwa vitendo vya kikatili ambavyo vilichangia kuzorota kwa maendeleo yao ya kijamii na kiuchumi, hivyo kuandaliwa kwa mpango huu utasaidia kuweka mikakati endelevu ya utekelezaji wa changamoto zote ambazo wamekuwa wakikabliana nazo,” 

“Mpango Kazi huu wa Taifa kwa Watu wenye Ualbino ni faraja kubwa sana kwetu sisi kama Serikali pamoja na wadau kwa sababu mpango huu umeweka bayana maeneo makuu manne ambayo ni ulinzi, uzuaiji, usawa, ubaguzi na uwajibikaji,” alisema Mhe. Katambi.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi (kulia) akipokea raismu ya Mpango Kazi wa Taifa kwa Watu Wenye Ualbino kutoka kwa Katibu Mkuu wa Chama cha Watu Wenye Ualbino Tanzania (TAS) (kushoto) baada ya kikao hicho  kilichofanyika katika Ukumbi  wa Mikutano Dodoma Hotel


Aliongeza kuwa, Serikali inaendelea kutoa kipaumbele katika huduma za afya kwa Watu wenye Ulemavu, kuboresha miundombinu ili kujenga mazingira fikivu yatakayo wawezesha Watu wenye Ulemavu kufanya shughuli zao katika mazingira rafiki kama watu wengine.

“Serikali inatekeleza miradi mbalimbali na katika ujenzi wa miradi hiyo inazingatia miundo mbinu rafiki kwa Watu wenye Ulemavu ili wawezesha kupata huduma kama watu wengine na wamekuwa wakipewa kipaumbele wanapoenda kupata matibabu au huduma nyingine za kijamii mahali popote,” alieleza 

Vilevile alibainisha kwamba Watu wenye Ulemavu wana haki ya kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo fursa za ajira au fursa mbalimbali zinazojitokeza ili wajikwamue kiuchumi badala ya kuendelea kuwa tegemezi, hivyo alihasa jamii kutambua mchango wa Watu wenye Ulemavu kuanzia ngazi ya familia hadi Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha Watu wenye Ualbino Tanzania (TAS) Bw. Mussa Kabimba alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kwa kushirikiana na chama hicho cha TAS pamoja na wadau katika uaandaji wa mchakato huo hadi kufikia hatua ya kukamilika kwake.

“Tunashukru watalamu wote kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia kitengo cha huduma kwa Watu Wenye Ulemavu na Idara ya Sera na Mipango kwa namna walivyojitoa kushirikiana pamoja na Chama cha Watu wenye Ualbino Tanzania (TAS) katika kurekebisha Mpango kazi huu wa Taifa kwa Watu wenye Ualbino,” alisema

Pamoja na hayo, alitumia fursa hiyo kupongeza mchakato wa Serikali wa ujenzi wa Vyuo vipya vya Ufundi Stadi kwa Watu wenye ulemavu katika mkoa wa Kigoma na Songwe sambamba na maboresha ya vyuo sita vya Ufundi Stadi kwa watu wenye ulemavu ambavyo ni Yombo - Dar es salaam, Mtapika - Mtwara, Sabasaba - Singida, Luanzari - Tabora, Masiwani – Tanga na Milongo kilichopo Jijini Mwanza.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (SHIVYAWATA) Bi. Tungi Mwanjara alihimiza Serikali kushirikiana na wadau wa maendeleo kutoa elimu kuhusu haki za Watu wenye Ulemavu ili kuhakikisha usalama wa kundi hilo. 

MWISHO

 

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.