Na. OMM Rukwa
Mkuu
wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Mkirikiti amezionya halmashauri za mkoa huo kwa
kutokutoa fedha za utekelezaji wa afua za lishe katika kipindi cha Oktoba hadi
Desemba 2021.
Ametoa
onyo hilo jana (25.02.2022) wakati akiongoza kikao cha tathmini ya mkataba wa
shughuli za lishe kipindi cha Julai hadi Desemba 2012 kilichofanyika mjini
Sumbawanga ambapo halmashauri zote nne ziliripotiwa kutoa fedha za lishe asilimia
17.5 tu hatua inayokwamisha shughuli za lishe.
“Leo
ndio siku ya mwisho nisisikie kuwa Afisa Lishe anasema hajapewa fedha za
kutekeleza shughuli wakati mkoa bado una tatizo la udumavu na utapiamlo. Wakurugenzi
nendeni mkabadilike. Suala la lishe ni agenda muhimu kwa uhai wa watu wetu”
alisisitiza Mkirikiti.
Kwa
mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa ambaye pia ni Mganga
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Dkt. Bonoface Kasululu ilionyesha kuwa halmashauri za
Sumbawanga Manispaa, Sumbawanga Vijijini, Nkasi na Kalambo zimetoa asilimia 17
na kupelekea mkoa uwe kwenye rangi nyekundu.
Dkt.
Kasululu aliongeza kusema matokeo ya ujumla yanaonesha kuwa mkoa wa Rukwa una
wastani wa alama asilimia 87 ambapo kiasi hicho kimechangiwa na kutokutolewa
kwa fedha za afua za lishe kwa upande wa halmashauri.
Sehemu ya Maafisa Lishe wa Halmashauri wakiwa kwenye kikao cha tathmini ambapo walieleza kutopata fedha kutekeleza afua za lishe kutoka halmashauri kipindi cha Julai hadi Desemba 2021 |
“Asilimia
ya bajeti ya halmashauri iliyotumika kutekeleza shughuli za lishe kati ya
iliyotengwa rangi nyekundu ni asilimia 17.5 kiashiria hiki kinaendelea kufanya
vibaya zaidi ikilinganishwa na matokeo ya asilimia 54 kipidi cha mwaka
2020/2021” alieleza Dkt. Kasululu.
Taarifa
ya tathmini kwa kiashiria cha asilimia ya fedha zilizotumika kwa shughuli za
lishe katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2021 kwenye halmashauri na asilimia
zake kwenye mabano Manispaa ya Sumbawanga (0.0), Sumbawanga DC (18.9), Nkasi DC
(0.0) na Kalambo DC (47.7) hatua inayofanya mkoa kuwa na jumla ya asilimia 17.5
Mmoja
wa Maafisa Lishe toka Halmashauri ambaye hatuka jina litajwe alisema “tumekuwa
tukiandika madokezo kuomba fedha za shughuli za lishe lakini hatupatiwi bila
kupewa sababu. Oktoba –Desemba, 2021 niliomba shilingi 800,000 lakini hadi leo
sijajibiwa na kazi zimesimama” alisema mtaalam huyo.
Kwa
upande wake Mwakilishi wa Shirika la Jukwaa la Lishe Tanzania (PANITA) Aron
Isaack alisema licha ya mkoa wa Rukwa kushika nafasi ya 13 kati 26 mwaka 2020/21
bado kuna changamoto kubwa ya shughuli za lishe kutopewa kipaumbele hatua
inayosababisha utapiamlo na udumavu kuendelea.
Isaack
aliongeza kuwa kunahitajika utashi wa kisiasa ili kutekelezwa kwa mkataba wa lishe
miongoni mwa viongozi na watendaji wa serikali wakiwemo Waganga Wakuu wa Wilaya
za Rukwa.
“Tunaishukuru
serikali kwa kusimamia suala la lishe hasa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM
ya mwaka 2020 iliyotamka suala la lishe kupewa kipaumbele “alisema Isaack.
Kwa
mujibu wa taarifa ya lishe iliyotolewa na Wizara ya Kilimo Desemba 2020
ilionesha kuwa mikoa inayoongoza kwa uzalishaji mazao ya chakula ndio ina
kiwango kikubwa cha udumavu unaotokana na utapiamlo ikiwemo Rukwa (47.9),
Njombe (53.6) na Iringa (47.1).
Mwisho.
Comments
Post a Comment