Na. Mwandishi Wetu,
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt.
Selemani Jafo ametoa rai kwa watekelezaji na wasimamizi wa Mradi wa Kuhimili
Mabadiliko ya tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (Ecosystem Based
Adaptation for Rural Resilience – EBARR in Tanzania) unaotekelezwa Kaskazini A
- Unguja kuongeza kasi ya uchimbaji wa visima katika eneo la Matembwe ili
wakazi wa maeneo hayo waweze kunufaika na maji safi na salama.
Dkt. Jafo
ametoa rai hiyo mara baada ya kufanya ziara ya kikazi
katika eneo la Matembwe na kuzungumza na watendaji na wasimamizi wa mradi
huo na
kuwaagiza kusimamia kazi zote zilizopangwa kutekelezwa na kuhakikisha
zinakamilika kwa wakati bila kuomba muda wa nyongeza.
Amesema
agenda ya mazingira ni suala linaloigusa dunia kwa sasa na kuainisha kuwa
athari za mabadiliko ya tabianchi ni dhahiri na ni mjadala wa kidunia hivyo
Ofisi yake itahakikisha inashirikiana na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais
(Zanzibar) katika kuibua miradi yenye manufaa kwa pande zote mbili za muungano.
“Ndugu
zangu sote ni mashahidi wa athari hizi za mabadiliko ya tabianchi ikiwa ni
pamoja na kuongezeka kwa ukame na hapa Zanzibar visima viko hatarini kutoweka
kutokana na ongezeko la kina cha bahari” Jafo alisisitiza.
Kwa upande
wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dkt. Saada Mkuya
ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutekeleza miradi
ya maendeleo pande zote mbili za Muungano na kusisitiza kuwa atahakikisha
shughuli zilizopangwa kutekelezwa na mradi huo ikiwa ni pamoja na ununuzi wa
boti, uchimbaji wa visima na utengenezaji wa majiko banifu unakamilika kwa muda
uliopangwa bila kuomba muda wa ziada.
Mradi wa
Kuhimili Mabadiliko ya tabianchi kwa kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini ni wa
kipindi cha miaka mitano na ulianza utekelezaji wake 2018 na unatekelezwa
katika wilaya za Kishapu, Mvomero, Mpwapwa, na Simanjiro kwa upande wa Tanzania
Bara. Kwa Zanzibar mradi unatekelezwa katika Wilaya ya Kaskazini A, Mkoa wa
Kaskazini Unguja - Kijiji cha Matemwe, Mbuyutende na Matemwe Jugakuu.
Lengo la
mradi huu ni kuongeza uwezo wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi
katika jamii za vijijini kwa kuimarisha mifumo ikolojia na kuwezesha njia
mbadala za kujiongezea kipato. Mradi huu unaratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais
kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Kwa upande
wa Zanzibar Mradi unatekelezwa kwa kushirikiana na Idara ya Mazingira (Ofisi ya
Makamu wa Kwanza wa Rais).
Jumla ya
shilingi 1,100,112,000 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za Mradi
upande wa Kaskazini A, na kazi zilizotekelezwa ni pamoja na kuendesha mafunzo
na kuviwezesha vikundi katika maeneo ya mradi kutengeneza majiko sanifu na
banifu kwa lengo la kupunguza matumizi makubwa ya kuni na mkaa na hivyo
kupunguza uharibifu wa misitu.
Pia,
kuandaa Mipango ya Usimamizi wa Matumizi ya ardhi ili kuwezesha jamii husika
kupanga matumizi ya ardhi kwa ajili ya Makazi, Kilimo, Ufugaji, Hifadhi ya
Misitu/mikoko na uoto wa asili, hifadhi ya vyanzo vya maji ili kuepusha
migogoro katika matumizi ya ardhi.
Kupitia
mradi huu utafanyika ununuzi wa boti sita za uvuvi, Uchimbaji wa Visima Virefu
sita (6) katika Shehia tatu za Kijini, Mbuyutende na Jugakuu na mpaka sasa
jumla ya majiko sanifu 90 yametengenezwa katika kaya ya Matemwe Kijini, Matemwe
Mbuyutende na Matemwe Jugakuu.
Comments
Post a Comment