WATUMISHI WA MAHAKAMA YA TANZANIA WAFURAHIA UJENZI WA MAKAO MAKUU

Na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma

Jumla ya Watumishi 120 wa Mahakama ya Tanzania kutoka Makao Makuu Dar es Salaam wamefanya ziara ya kutembelea na kujionea Mradi wa Ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama unaojengwa katika eneo la Tambuka Reli jijini Dodoma ambapo wameonyesha kufurahishwa na ujenzi wa majengo hayo yanayotarajiwa kukamilika mwisho wa mwaka huu.

Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Solanus Nyimbi aliyesimama mstari wa mbele kulia mwenye shati la 'Light blue'  akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Kada za Wasaidizi wa Kumbukumbu, Wasaidizi wa Ofisi, Wasaidizi wa Maktaba, Makatibu Mahsusi, Walinzi, Madereva wakiongozwa na Maafisa Utumishi waliotembelea Mradi wa Ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania mkoani Dodoma


Akizungumza na Watumishi hao waliotembelea Mradi huo tarehe 29 Januari, 2022, Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Solanus Nyimbi aliwaambia Watumishi hao kujiandaa kisaikolojia kwakuwa wapo mbioni kuhamia Dodoma.

“Ifikapo mwezi wa 12 mwaka huu ninyi wote mtakuwa mmehamia katika jengo hili, kwahiyo ni vizuri mkajiandaa kisaikolojia na kufanya maandalizi mengine ya msingi, kwa mfano najua wengine wana Watoto ambao wanaenda shule, wengine wana wenza wa kuwaweka sawa kisaikolojia, lakini la msingi la Mtendaji Mkuu kuwapa fursa kuja kuona ni ili mpate picha ya sehemu mtakayokuja kufanya kazi,” alisema Bw. Nyimbi.

Aliongeza kuwa Watumishi wote wa Makao Makuu, Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu Masjala kuu wote wanatakiwa kuhamia katika jengo la Makao Makuu ya Mahakama-Dodoma ifikapo mwezi Desemba mwaka huu.

Akizungumza kwa niaba ya Watumishi, Afisa Utumishi wa Mahakama, Bw. Nkrumah Katagira ameshukuru Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole kwa kuwapa fursa ya kutembelea jengo hilo la Makao Makuu na kuongeza kuwa wamefurahi sana kupewa nafasi hiyo.

“Kwa niaba ya Watumishi wenzangu, nimshukuru sana Mtendaji wa Mahakama ya Rufani kwa niaba ya Mtendaji Mkuu, Watumishi kwakweli wamefurahi sana kwa hii safari, kwa sababu ni sehemu ya kujiandaa kisaikolojia kujua wapi tutakuja kukaa na hii imepunguza wasiwasi kwetu baada ya kuona sehemu ambayo tutakuja kufanyia kazi,” alisema Bw. Katagira.

Pamoja na kutembelea Mradi wa ujenzi wa Makao Makuu, Watumishi hao pia walitembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-Dodoma (IJC) na kutembelea Maonesho ya Wiki ya Sheria katika Viwanja vya Nyerere ‘square’ Dodoma.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama kutoka Dar es Salaam wakipata maelezo kuhusu uboreshaji wa huduma mbalimbali za Mahakama zenye lengo la kurahisisha huduma ya utoaji haki kwa wananchi. Watumishi hapo walipata pia fursa ya kutembelea Maonesho ya Wiki ya Sheria katika Viwanja vya Nyerere 'Square' Dodoma


Safari hii imejumuisha Watumishi wa Kada za Wasaidizi wa Kumbukumbu, Wasaidizi wa Ofisi, Wasaidizi wa Maktaba, Makatibu Mahsusi, Walinzi, Madereva wakiongozwa na Maafisa Utumishi.

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.