WATAALAM WA AFYA 60 WAPATIWA MAFUNZO YA MOYO DAR ES SALAAM


Na: Mwandishi Maalum

30/01/2022 Wataalam wa afya 60 wanaofanya kazi katika hospitali za wilaya na hospitali binafsi za Mkoa wa Dar es Salaam wamepatiwa mafunzo ya kutambua moyo unaofanya kazi chini ya asilimia 50.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akitoa elimu ya jinsi ya kutambua moyo unaofanya kazi chini ya asilimia 50 kwa wataalam wa afya kutoka hospitali za wilaya na binafsi za Mkoa wa Dar es Salaam walioshiriki mafunzo maalum ya siku mbili ya jinsi ya kutoa huduma ya dharura kwa wagonjwa yaliyoandaliwa na kituo cha mafunzo cha tiba na huduma za dharura na kufanyika katika ukumbi wa JKCI leo Jijini Dar es Salaam


Elimu hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi wakati wa mafunzo maalum ya siku mbili ya jinsi ya kutoa huduma ya dharura kwa wagonjwa yaliyoandaliwa na kituo cha mafunzo cha tiba na huduma za dharura na kufanyika katika ukumbi wa JKCI leo Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mafunzo hayo Prof. Janabi ambaye pia ni Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo amesema kuwa JKCI iliona ni muhimu kwa wataalamu hao wa afya kupata elimu ya kutambua moyo unaofanya kazi chini ya asilima 50 kwani wengi wao wametoka katika hospitali za wilaya ambazo wagonjwa huanzia huko.

“Tumetoa elimu ya kutambua moyo unaofanya kazi chini ya asilimia 50 kwa wataalam wa afya wanaoshiriki mafunzo ya jinsi ya kutoa huduma ya dharura kwa wagonjwa kwani hawa ndio wataalam wanaokutana na wagonjwa wengi katika ngazi ya kwanza hivyo kupitia elimu niliyoitoa itawasaidia zaidi kutoa huduma bora za matibabu wanapokutana na wagonjwa wa moyo lakini pia kutambua ni kwa wakati gani wanapaswa kuwapa rufaa wagonjwa hao kufika katika taasisi yetu”, alisema Prof. Janabi

Akizungumzia mafunzo ya dharura kwa wagonjwa Prof Janabi amesema kuwa wataalam wa afya wanaopata mafunzo hayo itawasaidia kutoa huduma ya dharura iliyo sahihi kwani hatua ya kwanza kufanyiwa mtu anayehitaji huduma ya dharura ni ya muhimu kama itafanywa kwa usahihi hivyo kuokoa maisha ya mgonjwa.

“Kupata ujuzi wa jinsi ya kutoa huduma ya kwanza haimtaki mtu kuwa daktari tu bali kila mtu anapaswa kuwa na ufahamu wa kutoa huduma hiyo kwani kwa kuwa na ujuzi huo humsaidia mtu kuokoa maisha ya mtu mwingine anayehitaji huduma ya dharura mahali popote pale tatizo linapojitokeza”,

“Iliwahi kunikuta mara mbili nikiwa katika safari tofauti nimeweza kuokoa maisha wa watu wawili waliohitaji huduma ya dharura hivyo kuokoa maisha yao, ndio maana nasisitiza watu wote tuwe na ufahamu wa namna ya kutoa huduma ya dharura kwani dharura hizo hazitokei hospitali peke yake”, alisema Prof. Janabi.

Washiriki wa Mafunzo ya siku mbili ya jinsi ya kuwahudumia wagonjwa wa dharura wakifanya mazoezi kwa vitendo jinsi ya kuokoa maisha ya mtu anayehitaji huduma ya dharura wakati wa mafunzo ya siku mbili ya jinsi ya kuwahudumia wagonjwa wa dharura yaliyoandaliwa na kituo cha mafunzo cha tiba na huduma za dharura leo katika ukumbi wa JKCI Jijini Dar es Salaam


Kwa upande wake mkufunzi kutoka kituo cha mafunzo cha tiba na huduma za dharura Dkt. Silvester Faya amesema kuwa wameamua kufanya mafunzo hayo kwa ajili ya kuongeza utaalam kwa watumishi wa afya ili watumishi hao wanapomaliza mafunzo hayo wakabadilishe maono katika kutoa huduma za dharura kwa wagonjwa.

Aidha Dkt. Faya amesema kuwa elimu ya huduma ya dharura bado haijaenea kwa watu ambao sio wataalam wa afya lakini kupitia wataalam wa afya elimu hiyo inaweza kusogea na kuwafikia wananchi wengine ili mtu anapohitaji huduma ya dharura aipate pale shida ilipompata kabla ya kufikishwa hospitalini.  

“Tunaamini yakuwa kama kila mwananchi atapata elimu ya namna ya kumhudumia mtu anayehitaji huduma ya dharura tutapunguza madhara mengi yayaoweza kumpata mgonjwa ikiwemo kupunguza vifo vinavyotokana na kukosa huduma ya dharura kwa wakati” alisema Dkt. Faya

Akizungumzia mafunzo hayo Mratibu wa huduma za dharura Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Paschal Mgaya amesema kuwa nafasi waliyoipata madaktari na wauguzi wachache kutoka katika hospitali za wilaya za Mkoa wa Dar es Salaam iwe chachu kwa watoa huduma wa afya wengine ambao hawakupata nafasi ya kushiriki mafunzo hayo.

“Mafunzo haya yatatusaidia zaidi katika mkoa wetu wa Dar es Salaam kwani wale wachache waliopata mafunzo haya wataenda kutoa elimu hiyo kwa wataalam wengine ambao hawakupata nafasi ya kushiriki hivyo kupunguza changamoto nyingi zilizopo katika kutoa huduma ya dharura na kuokoa maisha ya wagonjwa”, alisema Dkt. Mgaya.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo maalum ya kutoa huduma ya dharura wakifuatilia elimu iliyokuwa ikitolewa na Prof. Janabi (hayupo pichani) wakati wa mafunzo maalum ya siku mbili ya jinsi ya kutoa huduma ya dharura kwa wagonjwa yaliyoandaliwa na kituo cha mafunzo cha tiba na huduma za dharula na kufanyika katika ukumbi wa JKCI leo Jijini Dar es Salaam


Naye afisa Muuguzi kutoka hospitali binafsi ya Sali Judithi Kashe amesema kuwa kupitia mafunzo maalum ya jinsi ya kutoa huduma ya dharura kwa wagonjwa amepata nafasi ya kujifunza vitu vingi vipya ambavyo hakuwa anavijua hivyo mafunzo hayo kwenda kuongeza tija katika utendaji kazi wake wa kila siku.

“Mafunzo tuliyoyapata leo hii yametujenga wataala wa afya kutoa huduma inayofanana na ya usahihi kwa wagonjwa wetu kwani watu wengi hupoiteza maisha pale mwanzoni wanapokosa huduma sahihi ya dharura”, alisema Judith

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.