Naibu Waziri Ofisi ya
Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Chande Desemba 30, 2021
amefanya ziara ya kushtukiza katika Kiwanda cha kurejeleza mifuko cha Hengji
Investment Co. Ltd kilichopo eneo la Ubungo, Dar es Salaam na kushuhudia ukiukwaji
mkubwa wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 kwa wamiliki wa kiwanda hicho
kutiririsha maji taka ambayo hayatibiwa na bila kibali cha Mamlaka ya Bonde la
Wami Ruvu kwenye Mto ng'ombe
Kufuatia ukiukwaji huo
wa Sheria Naibu Waziri Chande ametoa siku 14 kwa Kiwanda hicho kuhakikisha
kinaweka mfumo sahihi wa kutibu maji taka kabla ya kuyatiririsha kwenye
mazingira kama Sheria inavyoelekeza na kupata kibali kutoka Mamlaka ya Bonde la
Wami Ruvu.
"Wataalamu wa NEMC
simamieni hili kikamilifu, nitarudi tena kukagua. Hatuwezi kuweka maisha ya
wananchi rehani kwa kuruhusu ukiukwaji wa Sheria" Alisisitiza Naibu Waziri
Chande.
Pia, amemuagiza Meneja
wa Kiwanda cha Hengji Investment Bw. Calvin Payovela kuhakikisha wafanyakazi wa
kiwanda hicho wanapatiwa vifaa vya usalama mahala pa kazi na kusisitiza kuwa
hilo ni takwa la kisheria na si maamuzi ya mtu binafsi.
“Wafanyakazi hawa wapewe
vifaa vya kujikinga na vumbi na afya zao kwa ujumla maana afya zao ni jambo
muhimu sana, ili tuwe na kizazi endelevu yatupasa kuwa vijana wenye nguvu kazi
ya kutosha” Alisisitiza Naibu Waziri Chande.
Meneja wa Kiwanda hicho
Bw. Calvin Payovela amesema kuwa watahakikisha wanatekeleza maelekezo ya
Serikali ndani ya muda uliotolewa.
Katika hatua nyingine
Naibu Waziri Mhe. Hamad Chande ameuagiza uongozi wa Bonde la Wami Ruvu na
Manispaa ya Kinondoni kuandaa mpango wa muda mrefu wa kunyosha Mto Nyakasanga
ili kupunguza athari za mafuriko kwa wakazi wa eneo hilo.
Naibu Waziri Chande
ametoa rai hiyo baada ya kufanya ziara ya kukagua mwendelezo wa usafishaji mto
huo kwa kuondoa mchanga, tope na taka ngumu katika eneo la Boko.
Amesema Mamlaka ya Bonde
la Wami Ruvu wana wajibu wa kuendelea kusimamia Sheria na kuhakikisha wananchi
hawaweki makazi ya kudumu pembezoni mwa mto huo na kutoa elimu kwa umma juu ya
namna bora ya kujikinga na athari zinazoweza kutokea kutokana na mto kupanuka.
"Lengo la Serikali
ni kuhakiksha watu wako salama na mto unabaki salama" Chande alisisitiza.
Kwa upande wake Kaimu
Meneja wa Kanda ya Mashariki Kaskazini Bi. Lilian Kapakala amesema jamii
inapaswa kupanda miti rafiki kwa mazingira pembezoni mwa mito ili kupunguza
kasi ya mmomonyoko wa udongo.
Nae Mhaidrolojia kutoka
Mamlaka ya Bonde la Wami Ruvu Bw. Jeremia Nestory amesema Mamlaka ya Bonde kwa
kushirikiana na Manispaa ya Kinondoni wanaendelea na utekelezaji wa kusafisha
Mto Nyakasanga kwa kuondoa tope na mchanga ili kurejesha mto katika mkondo
wake.
Kufuatia uchimbaji
holela wa mchanga kwenye mito na mabonde katika Mkoa wa Dar es Salaam
umeandaliwa mwongozo wa usafishaji mchanga, tope na taka ngumu kwenye mito na
mabonde kwa jiji la Dar es Salaam ambao utekelezaji wake umeanza.
Comments
Post a Comment