Na Veronica Simba - Kigoma
Imeelezwa
kuwa Mpango Kabambe wa Kupeleka Nishati Vijijini umelenga kuwanufaisha wananchi
kupitia usambazaji umeme pamoja na nishati bora ya kupikia.
Hayo
yalibainishwa mwishoni mwa wiki wakati wa ziara ya viongozi wakuu wa Wakala wa
Nishati Vijijini (REA) mkoani Kigoma.
Wakizungumza
kwa nyakati tofauti, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius
Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa REA Mhandisi Hassan Saidy, walisema kuwa Mpango
huo unahusisha nishati za aina mbalimbali, siyo umeme peke yake.
Wakili Kalolo
alisema kuwa, ni jukumu la REA kuhakikisha wananchi waishio vijijini wanapata
nishati safi na zenye gharama nafuu ili ziwasaidie kuboresha maisha yao, hivyo
Wakala umejiwekea mikakati ya kuhakikisha jukumu hilo linatekelezwa ipasavyo.
Akifafanua, alisema
kuwa REA imefanikiwa kwa kiasi kikubwa na inaendelea kufanya vema katika
utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, hivyo hakuna shaka katika utekelezaji
wa miradi ya aina nyingine za nishati zilizofanyiwa tafiti, utakuwa wenye
ufanisi pia.
Akitoa mfano,
alisema kuwa tafiti zinaonesha eneo jingine muhimu linalopaswa kupewa
kipaumbele ni katika nishati ya kupikia ambapo asilimia kubwa ya waathirika ni
wanawake, ambao kutokana na matumizi ya kuni, wamekuwa wakisumbuliwa na
magonjwa ya macho na kifua.
Alisema, ni
kwa sababu hiyo, Wakala umedhamiria kuondoa adha hiyo katika jamii hususani
wanawake waishio vijijini.
Kwa upande
wake, Mkurugenzi Mkuu akidadavua zaidi kuhusu Mpango huo kabambe, alieleza kuwa
umejikita katika sehemu mbili kubwa ambazo ni usambazaji umeme pamoja na
nishati ya kupikia.
Alieleza
zaidi kuwa, hivi sasa, Wakala unaongeza nguvu zaidi katika nishati ya kupikia
ili kuhakikisha kwamba wananchi hususan wa vijijini, wanatumia nishati bora kwa
shughuli za kupikia na kupunguza au kuachana kabisa na matumizi ya kuni na mkaa
ambao upatikanaji wake ni mgumu, aghali na siyo rafiki kwa mazingira.
Mhandisi
Saidy alisema REA imefanya tafiti kadhaa za majaribio kuhusu nishati ya kupikia
mathalani mradi wa kutumia tungamotaka, ambapo mifumo husika ilipelekwa katika
maeneo 725 yaliyopo sehemu mbalimbali nchini.
Aidha,
aliongeza kuwa, Wakala umeshirikiana na kampuni za usambazaji gesi kufanya
tafiti kuhusu uwezekano wa kuhakikisha nishati ya gesi inafikishwa katika
maeneo ya vijijini kwa gharama nafuu ili wananchi waweze kuitumia kwa shughuli
za kupikia.
Katika hatua
nyingine, viongozi hao waliwahakikishia Wakuu wa Wilaya za Kibondo na Kakonko,
ambao walikutana nao kwa nyakati tofauti, kuwa maeneo yote ya kimkakati, hasa
yanayohusisha masuala ya usalama yatapelekewa huduma ya umeme ili kuwezesha
shughuli hizo kufanyika kwa ufanisi.
Awali, Mkuu
wa Wilaya ya Kakonko Kanali Evance Malassa na Mkuu wa Wilaya ya Kibondo Kanali
Aggrey Magwaza, kwa nyakati tofauti waliomba maeneo ya mpakani ambayo
hayajafikiwa na huduma ya umeme, yapewe kipaumbele katika kufikishiwa nishati
hiyo ili kuimarisha shughuli za kiusalama.
Pia, Wakuu
hao wa Wilaya walipongeza jitihada ambazo zimekuwa zikifanywa na Wakala wa
Nishati Vijijini katika kusambaza umeme vijijini kupitia miradi mbalimbali
inayoendelea kutekelezwa.
Katika ziara
hiyo, Mwenyekiti wa Bodi na Mkurugenzi Mkuu pia walikagua miradi mbalimbali ya
umeme pamoja na kukutana na wakandarasi wanaotekeleza miradi hiyo ambapo
walijadili changamoto zilizopo na kuzipatia ufumbuzi.
Kupitia kikao
hicho, viongozi hao waliipatia ufumbuzi changamoto ya upatikanaji vifaa
iliyokuwa ikimkabili Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa REA Awamu ya Tatu
Mzunguko wa Kwanza, Kampuni Tanzu ya TANESCO (ETDCO) katika wilaya za Kakonko
na Kibondo.
“Utekelezaji
ulikuwa nyuma kidogo kutokana na changamoto ya vifaa. Tumetatua changamoto hiyo
na tumemwelekeza Mkandarasi ndani ya miezi mitatu awe amekamilisha mradi huu,”
alisema Mkurugenzi Mkuu.
Aidha,
Mkandarasi anayetekeleza Mradi huo katika wilaya za Buhigwe, Kasulu, Kigoma
Vijijini na Uvinza, Kampuni ya M/s CCCE Etern Consortium alielekezwa kuongeza
nguvu ili akamilishe kazi hiyo kwa wakati uliopangwa ambao ni mwishoni mwa
mwezi huu wa Desemba, 2021.
Miradi
mingine inayotekelezwa mkoani Kigoma ni pamoja na REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa
Pili unaotarajiwa kuanza hivi karibuni pamoja na Mradi wa Ujazilizi unaolenga
kufikisha umeme katika maeneo yaliyopitiwa na miundombinu ya nishati hiyo
lakini umeme haujashushwa.
Katika ziara
hiyo, viongozi hao wa REA waliambatana na wataalamu mbalimbali kutoka Wakala
hiyo pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO)
Comments
Post a Comment