Na Mwandishi Wetu, MWANZA
Shirika la Nyumba la Taifa (NHC)
linatarajia kuanza kuwaondoa wapangaji wa nyumba zake ambao ni wadaiwa
sugu kuanzia mapema mwezi Desemba 2021.
Hayo yalibainishwa mwishoni mwa
wiki na Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline
Mabula wakati akizungumza na wapangaji wa shirika hilo jijini Mwanza ikiwa ni
muendelezo wa ziara zake za kikazi kukagua utekelezaji wa shughuli za sekta ya
ardhi na zile za shirika la Nyumba la Taifa pamoja na kusikiliza na
kuzipatia ufumbuzi changamoto za ardhi.
Kwa mujibu wa Dkt Mabula Shirika
la Nyumba la Taifa (NHC) linadai takriban Bilioni 26 Kwa wapangaji wa nyumba
zake jambo alilolieleza linachangia kuzorotesha kasi ya utendaji kazi wa
shughuli za kila siku za shirika ikiwemo ukarabati
‘’Tutachofanya sasa, yeyote
aliyelimbikiza deni na tushampa notisi lakini bado halipi kodi basi zoezi la
kumuondoa litafanyika bila hata kumtaarifu upya’’ Alisema Dkt Mabula
Aliongeza kuwa, oparesheni a
kuwaondoa wadaiwa sugu wa nyumba za NHC itaenda sambamba na kuwaondoa wapangaji
wote wasio waaminifu waliopangisha nyumba za shirika kwa gharama nafuu huku nao
wakipangisha watu wengine kwa gharama kubwa ambapo alikielezea kitendo hicho
kuwa ni kuiibia Serikali na halikubaliki kwa kuwa ni kosa kisheria.
Aliwahakikishia wapangaji wa
Nyumba za NHC kuwa, Shirika hilo limeanza kufanya ukarabati wa nyumba zake
ikiwa ni mpango wake wa miaka mitano na tayari kiasi cha zaidi ya shilingi
Bilioni hamsini kimetengwa kwa ajili ya shughuli hiyo
Kwa upande wake Mkuu wa wilaya
ya Nyamagana Amina Makilagi mbali na kupongeza shughuli zinazofanywa na Shirika
la Nyumba la Taifa aliliomba shirika hilo kuona namna ya kuzifanyia marekebisho
baadhi ya nyumba zake hasa upakaji upya wa rangi baada ya Serikali kuwapanga
upya wafanya biashara ndogo ndogo maarufu kama wamachinga maeneo ya miji ili
kupendezesha Mji
Naye Meneja wa NHC mkoa wa Mwanza Fadhili Anyegile alisema, kwa mwaka wa 2021/2022 shirika hilo limeweka mikakati ya kuhakikisha linapunguza malimbiko ya madeni ya wapangaji kwa asilimia mia moja, kutoa elimu kwa wapangaji juu utaratibu wa kulipa kodi kwa wakati na kuendelea na zoezi la kufanya matengenezo makubwa na madogo katika nyumba zake Ili kuzifanya kuendelea kuwa imara.
Comments
Post a Comment