Na Mwandishi Wetu,
MWANZA
Serikali ya awamu ya sita chini
Rais Samia Suluhu Hasan imedhamiria kumaliza kero na migogoro ya ardhi nchini
kwa kutatua iliyopo na kuweka mikakati ya kuzuia migogoro mipya ikiwemo utwaaji
maeneo ya wananchi bila kulipa fidia
Hayo yalisemwa na Naibu Waziri
wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula mwishoni mwa jijini
Mwanza wakati wa kutatua migogoro ya muda mrefu ya ardhi iliyopo wilaya ya
Nyamagana ukiwemo mgogoro wa wananchi na Mwekezaji kampuni ya Pamba Engineering
uliopo kata ya Mhandu.
Mgogoro mwingine ni baina ya
Msimamizi wa Mirathi Ndugu Abuu mwana familia ya Marehemu Mzee Seif eneo la
Miembeni mtaa wa Nera kata ya Isamilo kuhusu umilikishwaji eneo lao la urithi
na ulipwaji fidia kwa wananchi wa mtaa wa Kisoko kata ya Luchelele kutokana na
Serikali kutwaa eneo lao kwa ajili ya ujenzi wa shule
Katika kutatua mgogoro kati ya
wananchi na Mwekezaji Pamba Engineering Naibu Waziri Dkt Mabula ameelekeza
wananchi kumilikishwa eneo linalolalamikiwa kati yao na Mwekezaji katika Kata
ya Mhandu kufuatia wananchi hao kukidhi matakwa yote ya kisheria na kulipa
gharama za umilikishaji huku Familia ya Marehemu Mzee Seif ikielekezwa kupatiwa
viwanja Saba vilivyopatikana baada ya kupimwa eneo lao la asili alilolinunua
marehemu baba yao miaka ya themanini kwa aliyeteuliwa kusimamia mirathi baada
ya kujiridhisha
Kuhusu eneo la mtaa wa Kisoko
kata ya Luchelele Mhe Dkt Mabula mbali na kuwataka wananchi wa mtaa huo
kushirikisha viongozi waliopo katika maeneo yao kutatua kero mbalimbali za
ardhi alimtaka Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza Sekiete Yahaya kuhakikisha
anawalipa fidia wananchi wote 20 waliotwaliwa maeneo yao na Serikali kwa ajili
ya ujenzi wa shule mapema kabla ya mwaka wa fedha 2021/2022 kuisha ambapo kiasi
cha shilingi milioni 350 zinadaiwa na wananchi hao
‘’Nikuombe Mkurugenzi wananchi
hawa wamekaa muda mrefu wakisubiri fidia wengine wameshindwa hata kuendeleza
maeneo yao kwa sababu hawajalipwa fidia, naomba wananchi hawa
walipwe wote kabla ya mwaka wa fedha wa sasa kuisha ‘’ Alisema Dkt Mabula
Kwa upande wake mkurugenzi wa
jiji la Mwanza Sekiete Yahaya alisema kuwa, maeneo yanayotwaliwa kwa
ajili ya taasisi za Serikali kama shule na huduma nyengine yatalipwa fidia kwa
awamu mpaka deni lote litakapokwisha.
‘’Mhe Naibu Waziri naahidi
kulipa fidia kwa awamu kuanzia kipindi hiki cha kati kati ya mwaka wa fedha
2021/2022 na kumaliza jumla ya milioni 150 kufikia mwishoni mwaka huu wa
fedha’’ alisema Yahaya.
Naye Diwani wa kata ya Luchelele
Vicent Lusana alifafanua kuwa wanafunzi wanaotoka eneo lake wamekuwa wakitembea
umbali mrefu kwa ajili ya kufuata elimu na kusisitiza kuwa ipo haja kwa
Serikali kuharakisha ulipwaji wa fidia ili waanze ujenzi wa shule kwa lengo la
kuwafanya wanafunzi wa eneo hilo kupata elimu katika umbali mfupi na
kuwaepusha na changamoto mbalimbali ikiwemo mimba za utotoni
Akihitimisha Kamishina wa Ardhi
Msaidizi mkoa wa Mwanza Elia Kamihanda ametaka kuzingatiwa utengwaji maeneo kwa
ajili ya shughuli za Umma katika zoezi la upimaji na upangaji wa mji huku
akiwaasa wananchi kuhakikisha wanayalinda maeneo yote yanayotengwa kwa matumizi
ya jamii ikiwemo malalo na maeneo ya wazi.
Comments
Post a Comment