Wizara za Maji, Mifugo na Uvuvi mabingwa wa karata

 




 

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Timu za Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Mifugo na Uvuvi zimeibuka kidedea kwa kutwaa ubingwa wa mchezo wa karata kwa wanaume na wanawake kwenye michuano ya Shirikisho la Michezo kwa Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) uliofanyika leo kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro.

Mchezaji Tuombe Alphonce wa Wizara ya Maji alimshinda Stephano Mjema wa Wizara ya Maliasili na Utalii katika mchezo wa fainali kwa pointi 2-1; huku Sakina Chamshama wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi amemfunga Stella Telengelwa wa Wizara ya Katiba na Sheria kwa pointi 2-0.

Nafasi ya tatu kwa wanaume imechukuliwa na Abdu Chalamande wa RAS Shinyanga aliyemshinda Paschal Banzi wa Wizara ya Katiba na Sheria kwa alama 2-0; wakati kwa wanawake aliyeshika nafasi ya tatu ni Ambiliasia Minja wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) aliyemfunga Mayasa Mlula wa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera. 

Kwa upande wa mchezo wa kuvuta kamba kwa wanawake uliokuwa hatua ya Nane bora timu ya Idara ya Mahakama waliwavuta Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa 2-0; nayo Ofisi ya Waziri Mkuu Sera waliwavuta Hazina kwa 2-0; huku RAS Iringa waliwavuta Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi) kwa 2-0 na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) waliwashinda Wizara ya Mambo ya Ndani kwa 2-0.

Mechi hizo za nusu fainali zitafanyika kesho ambapo kwa wanaume timu zilizofuzu ni  Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi), Idara ya Mahakama, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mh. Martin Shigela jana amesema hakuna sababu kwa mwaka 2022 timu zilizoshiriki mwaka huu kushindwa kushiriki na badala yake ziongezeke Zaidi ili kuleta ushindani mkubwa baina ya timu, ambapo pia watumishi wanaposhiriki wanaongeza ufanisi mahala pa kazi kutokana na kuwa na afya njema.

“Mtumishi wa Umma anapoingia kwenye mashindano anajengewa uwezo wa kufanya kazi kwa makini na bidii, hiyyo wanapokuja kucheza katika mashindano kunawaongezea vitu Fulani akilini na mwilini mwao,” amesema Mh. Shigela. 

 

Wakati huo huo, mchezo wa kuendesha baiskeli itafanyika kesho kwa upande wa wanawake ni kilometa 24.5 zitakazoanzia Njiapanda ya Kilosa na kumalizikia eneo la Mafiga, huku kwa wanaume ni kilometa 35 zinazoanzia Kijiji cha Malecela na kumalizia eneo la Mafiga. 

Mwisho

 

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.