Maafisa
Watendaji wa Kata pamoja na Maafisa Tarafa wa Mkoa wa Rukwa wametakiwa kutambua
kuwa wanalo jukumu la kusimamia ukusanyaji na matumizi ya fedha zitokanazo na
mapato ya ndani kwenye halmashauri.
“Mnatakiwa
kutambua kiasi cha fedha za mapato ya ndani zinazokusanywa kutoka kwenye
vijiji, mitaa na maeneo ndani ya kata na tarafa zenu kwenda kwenye halmashauri
ili mtoe usimamizi wa karibu wa matumizi kwenye miradi ya maendeleo” alisema
Mkirikiti.
Mkuu
wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti ametoa maelekezo hayo jana (28.10.2021)
wakati alipofanya mkutano na Maafisa Tarafa wote wa mkoa wa Rukwa na Maafisa
Watendaji wa Kata mjini Sumbawanga na kuwasisitiza kudhibiti mianya ya upotevu
wa fedha toka kwa vyanzo mbalimbali.
Mkuu
huyo wa Mkoa aliongeza kusema watendeji hao wa serikali wanao wajibu mkubwa wa
kuhakikisha wanafuatilia fedha zinazopelekwa kwenye maeneo yao toka serikali
kuu kutekeleza miradi ya shule,afya,miundombinu,maji hifadhi za mazingira nk.
Aidha,
alitoa maagizo mengine manne kwa
watendaji hao ,kwanza kwenda kutambua miradi yote inayotekelezwa kwenye kata na
tarafa zao ili waisimamie ikamilike kwa wakati na ubora.
Pili,
kutatua migogoro ya wananchi kwa kuwatembelea na kusuluhisha katika ngazi za
vijiji na mitaa badala ya kusubiri viongozi ngazi ya wilaya au mkoa na tatu, kusimamia
utunzaji wa mazingira ikiwemo kuhamasisha wananchi kupanda miti na kudhibiti
uchomaji moto misitu.
“Mkoa
huu wa Rukwa miti inakatwa ovyo, moto kichaa, uchomaji mkaa usiofuata taratibu.
Hili nendeni mkalisimamie kwa karibu” alisisitiza Mkirikiti
Agizo
la nne amewataka watendaji hao wa kata na tarafa kuelimisha wananchi kujitokeza
kupata chanjo ya kinga dhidi ya ugonjwa wa korona na pia kuhamasisha wananchi
kujiandaa kwa zoezi la sensa ya watu na
makazi itakayofanyika mwaka 2022.
Akizungumza
kuhusu umuhimu wa chanjo ya UVIKO-19 Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt. Boniface
Kasululu, aliwataka watendaji hao kuwa mstari wa mbele kwa wao binafsi kuchanja
kisha kuhamasisha wale ambao bado
hajawachanja.
“Nawaomba
sisi watendaji wa serikali tuwe mstari wa mbele kuuunga mkono jitihada za Rais
Samia Suluhu Hassan kwa kujitokeza kuchanja na kuwaelimisha wenzetu, chanjo ni salama na inasaidia kupunguza maambukizi
na pia kuzuia vifo vitokanavyo na ugonjwa wa korona” alisema Dkt. Kasululu.
Dkt.
Kasululu aliongeza kusema mkoa umepokea dozi 24,183 za chanjo ya UVIKO-19 awamu
ya pili aina ya Sinopharm ambapo kazi ya kuhamasisha wananchi imeanza hivyo
amewataka watendaji hao kushiriki kwenye zoezi hilo pamoja na wataalam wa afya
kwenye maeneo yao.
Naye
Afisa Utumishi Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa Sabina Songela akitoa mada kuhusu
majukumu na wajibu wa Maafisa Tarafa na Watendaji wa Kata alisema wanalo jukumu
la kusimamia suala la upatikanaji huduma kwa wananchi ili kuleta ustawi na amani kwenye maeneo yao.
Mkutano
huo wa Maafisa Tarafa toka tarafa zote 19 za Mkoa wa Rukwa na Maafisa Watendaji
Kata toka kata 20 za Manispaa ya Sumbawanga ni kwanza tangu Mkuu huyo wa Mkoa
alipoteuliwa kuongoza mkoa wa Rukwa hapo mwezi Mei mwaka huu na ulilenga
kuwakumbusha wajibu wao kwenye utekelezaji wa majukumu ya serikali.
Mwisho.
Imeandaliwa
na;
Afisa Habari Mkuu,
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa,
SUMBAWANGA
29.10.2021
Comments
Post a Comment