Na.WAMJW - Dodoma
Wakazi wa Mji wa Dodoma na
vitongoji vyake wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kupata huduma za
afya kutoka kwa madaktari bingwa walioweka kambi kwenye tamasha la ‘Karibu
Dodoma festival ‘ finale endelea kwenye viwanja vya Chinangali jijini hapa.
Wito huo umetolewa jana na
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy
Gwajima wakati akitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali yaliyoshiriki tamasha
hilo ikiwemo taasisi za afya, Hospitali Maalum, Mkoa na Taifa za wizara hiyo.
Dkt. Gwajima alisema wizara yake
imewaletea madaktari bingwa kutoka taasisi na hospitali za Taifa na hivyo
huduma zinapatikana ngazi zote kwani matatizo bado yapo kwenye jamii na watu
wengi wanatembea na magonjwa bila kufahamu kitu ambacho kinasababisha matatizo
Makubwa siku za usoni hivyo akawataka kutumia tamasha hilo kwani huduma
imesogezwa.
Akitolea mfano kwenye tamasha
hilo amesema kati ya wananchi 67 waliojitokeza kupima maambukizi ya kifua kikuu
walipata watu saba wenye kifua kikuu huku mmoja akibainika kuwa na kifua kikuu
sugu. Vilevile, baadhi wamebainishwa kuwa na matatizo ya miguu na uti wa mgongo
na wamepatiwa vipimo ya X-ray hapohapo kwenye tamasha hilo.
"Hapa kwenye tamasha tunalo
gari tembezi la TB ambalo lina Vifaa vyote ikiwemo mashine ya X-ray, wagonjwa
wetu wanaofika hapa wanapata huduma za vipimo hapa hapa na hata kama watafika
banda la MOI basi vipimo wa kiuchunguzi ya magonjwa ya mifupa na uti wa mgongo
watavipata kupitia gari hilo, mie huwa nasema hili gari ni Muhimbili
inayotembea” Aliongeza.
Kwa upande wa Ugonjwa wa
Saratani Dkt. Gwajima, alisema tamasha hilo limekua na faida kubwa kwani
wameweza kuwachunguza akina mama zaidi ya 35 na wanne kati yao wamegundulika na
saratani ya shingo ya kizazi na mmoja aligunduliwa kuwa na viashiria vya saratani
ya shingo ya kizazi,
”Sasa kama huyu mama asingefika
hapa asingejua na baada ya miaka miwili ukute ingekua imeshakomaa na labla
asingeweka kufika Ocean road”.
"Serikali ya awamu ya sita
imedhamiria kufikisha huduma karibu na wananchi, tumeona faida kupitia tamasha
hili ni wakati sasa wa kupanga kila baada ya miezi mitatu kuwasogezea wananchi
huduma hizi huko walipo kwenye mikoa mingine pia watoa huduma wa huko watapata
ujuzi zaidi kupitia wataalamu wetu toka hospitali za Taifa kama, Muhimbili,JKCI,MOI
na Ocean road”, Alisisitiza.
Aliongeza kwa upande wa
maendeleo na ustawi wa jamii Dkt. Gwajima aliwataka wazazi na walezi kuzingatia
suala la malezi bora kwa watoto ili kuondokana na watoto wanaoishi mazingira
magumu na kufanya kazi mitaani ili Taifa kuwa na vijana wenye msingi na maadili
mazuri kwa maendeleo ya nchi.
Hata hivyo aliwaasa wananchi
kuacha maamuzi ya kuwapiga watu na kuwanyanyasa wenye matatizo ya afya ya akili
kwani kwa sasa wanajipanga kusogeza huduma za hospitali hiyo karibu na wananchi
ili kuzuia, kuibua na kupanua huduma za hospitali maalumu ya Mirembe
inayoshughulika na afya ya akili.
-Mwisho
Comments
Post a Comment