Na Faustine Kapama na Mary Gwera, Mahakama-Tarime
Mahakama ya Tanzania
imeanza kutekeleza mradi mkubwa wa ujenzi wa Mahakama za Wilaya 19 katika
maeneo mbalimbali nchini ili kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi.
Akizungumza na Wakuu wa
Wilaya za Tarime na Rorya mkoani Mara pamoja na watumishi wa Mahakama katika
ziara yake ya kikazi leo tarehe 28 Oktoba, 2021, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe,
Prof. Ibrahim Hamis Juma alibainisha kuwa Mahakama imetayarisha ramani ya nchi
nzima pamoja na mpango wa miaka mitano wa maendeleo ya miundombinu ambao
umeainisha maeneo yote ya Tanzania ambayo yana changamoto za Mahakama katika
ngazi mbalimbali.
“Tunajaribu kuweka ratiba
ya kutekeleza mpango huo. Kwenye mpango huo utakuta Wilaya ya Rorya haina jengo
na imewekewa ratiba ni lini lazima ipate jengo ndani ya miaka mitano, Wilaya ya
Tarime wanasema jengo ni chakavu, linahitaji ukarabati mkubwa, Serengeti
tumejionea wenyewe, ni chakavu na ni finyu na sio jengo ambalo linakidhi mahitaji
ya Wilaya. Kwa hiyo tumeweza kutayarisha hata gharama za ujenzi. Kwa mfano,
tukipata fedha leo tunajua tunaweza kutumia wapi na kujenga wapi,”
amesema.
Kwa mujibu wa Mhe. Prof.
Juma, malengo ya Mahakama ya Tanzania ni kila Wilaya kuwa na Mahakama ya Wilaya
na kwamba kila Tarafa iwe na Mahakama ya Mwanzo, mpango ambao
watajadiliana na Serikali Kuu ili kuona ni kwa namna gani wanaweza
kusogeza huduma za Mahakama hizo katika maeneo hayo na huenda siku moja miaka
20 au 30 ijayo kila Kata itakuwa na Mahakama ya Mwanzo, lengo hasa ni
kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi.
Akijibu taarifa
iliyowasilishwa kwake na Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Kanali Michael Mntenjele,
Jaji Mkuu alisema kuwa ni kweli Wilaya ya Tarime bado inahudumia Wilaya ya Rorya
katika ngazi ya Mahakama ya Wilaya, lakini taarifa nzuri zilizopo zinaonesha
tayari ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Rorya umeshaanza na sio Wilaya ya Rorya
tu pamoja na Wilaya zingine 18 na kwa mujibu wa ramani iliyopo, ifikapo June
mwaka ujao majengo hayo yawe tayari yamekamilika ili kusiwe na Wilaya ambayo
haina Mahakama za Wilaya.
Kwa hiyo, Mhe. Prof. Juma
aliwahakikishia wananchi wa Rorya alipokutana na Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe. Juma
Chikoka kuwa huduma za Mahakama ya Wilaya zitawafikia hivi karibuni na hali
waliyokuwa nayo haitakuwepo tena. Mkuu wa Wilaya hiyo alimshukuru
Jaji Mkuu na uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa ujumla kwa uamuzi walioufanya
wa kujenga Mahakama ya kisasa, ambayo itasaidia katika kuharakisha utoaji wa
haki kwa wananchi.
Awali, akitoa taarifa fupi
ya Wilaya yake, Mkuu wa Wilaya ya Tarime aliupongeza Mhimili wa Mahakama nchini
kwa juhudi kubwa za kuondosha mashauri na kutoa hukumu kwa wakati, jambo ambalo
limepunguza mlundikano wa mashauri hayo pamoja na malalamiko kwa wananchi. Hata
hivyo, Mhe. Kanali Mntenjele alibainisha baadhi ya changamoto ambazo anaamini
zikipatiwa ufumbuzi zitaharakisha utoaji wa haki kwa haraka kwa wananchi.
Baadhi ya changamoto hizo
ni Mahakama ya Wilaya ya Tarime kuhudumia pia Wilaya ya Rorya, kitendo ambacho
kinaweza kusababisha mlundikano wa mashauri na ucheleweshaji, uchache wa
Mahakama za Mwanzo, jambo ambalo husababisha wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta
huduma ya Mahakama na uwepo wa mlundikano wa mashauri.
Hata hivyo, Mkuu wa Wilaya
hiyo aliwasilisha ombi kwa Jaji Mkuu ili kuona namna ya kuharakisha usikilizaji
wa mashauri yanayohusu ujauzito kwa wananfunzi, ubakaji na ulawiti na kutolewa
uamuzi kwa wakati kwani kuahirishwa mara kwa mara kunaweza kupoteza ushahidi na
mashahidi.
Katika ziara hiyo, Jaji
Mkuu ameambatana na viongozi mbalimbali kutoka Makao Makuu, wakiwemo Msajili
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Mtendaji wa Mahakama ya
Rufani, Bw. Solanus Nyimbi ambaye amemwakilisha Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Mtendaji Mahakama Kuu, Masijala Kuu, Bw.
Samson Mashalla, ambaye amemwakilisha Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Bw.
Leonard Magacha’
Wengine ni Mkurugenzi wa
Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Malalamiko na Maadili, Mhe. Annah Magutu,
Mkurugenzi Msaidizi wa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Machumu Essaba,
Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Adrian Kilimi, Katibu wa Msajili Mkuu, Mhe. Jovin
Constantine na Afisa Utumishi, Mahakama ya Tanzania, Bw. Juni Mdede.
Kwa upande wa Mahakama Kuu
ya Tanzania, Kanda ya Musoma, yupo Jaji Mfawidhi, Mhe. John Kahyoza, Hakimu
Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, Mhe. Frank Moshi ambaye pia ni
Kaimu Naibu Msajili wa Mahakama Kuu katika Kanda hiyo, Mtendaji wa Mahakama Kuu
wa Kanda, Bw. Festo Chonya na Afisa Utumishi, Bi. Francisca Swai.
Jaji Mkuu, Mhe. Prof. Juma
anatarajia kukamilisha ziara yake ya kikazi kesho tarehe 29. 10.2021 ambapo
atafanya ukaguzi katika Mahakama ya Mwanzo Musoma Mjini, Mahakama ya Wilaya,
Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na hatimaye kuhitimisha kwa kufanya
majumuisho ya ziara hiyo.
Comments
Post a Comment