Na Eliafile Solla, TEA
Miundombinu bora ya elimu katika Halmashauri nyingi hapa nchini ni changamoto
kubwa ambayo haiwezi kuachiwa Serikali peke yake, bali kuna haja ya kuongeza
ushirikiano wa jamii katika kutatua changamoto hizo.
Mkurugenzi
Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), Bi. Bahati. I. Geuzye akiwasilisha
nasaha zake kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania
(ALAT) jijini Dodoma |
Kauli hii imetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Bi
Bahati. I. Geuzye, alipokuwa akitoa nasaha zake kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa
Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) uliofanyika katika ukumbi wa Jakaya
Kikwete jijini Dodoma.
Awali ya yote Bi. Bahati alibainisha kwamba, Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA)
inatambua umuhimu wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika
kuhamasisha na kuboresha mahusiano yao ya kiutendaji na Halmashauri za Majiji,
Manispaa na Miji kote nchini.
‘‘Kutokana na changamoto hizo za miundombinu bora ya elimu, Mamlaka ya Elimu
Tanzania (TEA) ambayo inaratibu na kusimamia Mfuko wa Elimu wa Taifa kwa
kushirikiana na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI),
imeandaa utaratibu utakaowezesha Halmashauri zetu kuanzisha Mifuko ya Elimu na
kwa zile Halmashauri ambazo tayari zina mifuko hiyo tuna dhamira ya kuihuisha
na kuanza kuitumia kikamilifu’’, alisema Bi. Bahati.
Aliongeza kwamba, katika mwaka 2020 sheria ndogo ya uanzishwaji wa Bodi ya
Mfuko wa Elimu wa Halmashauri iliridhiwa na Mhe. Waziri mwenye dhamana wa Ofisi
ya Rais – TAMISEMI na vile vile mwongozo wa uanzishwaji wa Mifuko
umekwishaandaliwa na kusambazwa kwa wajumbe hao wa mkutano wa ALAT.
‘‘Kazi iliyopo mbele yetu ni kutekeleza lengo kuu la kuanzisha na kuhuisha Mifuko
ya Elimu katika Hamlashauri zote nchini, moja ya mipango inayolenga uboreshaji
wa elimu katika maeneo wanayoishi wananchi’’ alibainisha Bi. Bahati
Zoezi hili la uanzishwaji na uhuishwaji wa Mifuko ya Elimu ya Halmashauri lina
faida nyingi ikiwemo kuwezesha Halmashauri kukuza ushirikiano wa jamii katika
kuchangia miradi ya kipaumbele ya elimu; kuboresha, kuendeleza na kukuza
viwango vya elimu katika Halmashauri husika.
Vile vile mifuko hii itawezesha Halmashauri kutenga sehemu ya mapato yake ya
ndani kwa ajili ya miradi ya elimu ndani ya Halmashauri pamoja na kuratibu
upatikanaji wa michango kutoka kwa mashirika yasiyo ya kiserikali na ya
kiserikali, mashirika ya kidini na watu binafsi kwa ajili ya kusaidia
uendelezaji wa miradi ya elimu ndani ya Halmashauri hiyo.
Comments
Post a Comment