Na. Veronica Simba - REA
Mkurugenzi
Mkuu mpya wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Said,
amekabidhiwa rasmi Ofisi na Mtangulizi wake, Mhandisi Amos Maganga leo Septemba 29, 2021
ambapo amewaasa watumishi kufanya kazi kwa bidii, maarifa na uadilifu.
Mhandisi Said
amesema matumaini ya Watanzania, hasa wa vijijini, yanategemea dhamana ambayo
REA imepewa.
“Tukitetereka
katika kutimiza majukumu yetu, tutafifisha matumaini ya Watanzania wengi ambao
wanategemea nishati kama nyenzo ya kubadilisha maisha yao,” amesisitiza.
Aidha,
Mkurugenzi huyo mpya wa REA amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kumwamini
kuwatumikia Watanzania katika wadhifa huo na kuahidi kuwa hatamwangusha.
Vilevile,
ametoa pongezi kwa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) chini ya Mwenyekiti Wakili
Julius Kalolo, Mtangulizi wake Mhandisi Maganga pamoja na wafanyakazi wote wa
REA kwa kazi nzuri iliyofanyika na kufikia hatua nzuri katika kusambaza nishati
vijijini.
“REA ni
miongoni mwa Taasisi za Umma ambazo zimefanya kazi kubwa sana na ambazo
zimegusa maisha ya wananchi. Huwezi kupata mafanikio kama haya ikiwa hauna Bodi
imara na yenye weledi mkubwa, Menejimenti nzuri na wafanyakazi wanaojituma,”
amefafanua.
Sambamba na
hayo, Mhandisi Said ameomba ushirikiano kutoka kwa Bodi, Menejimenti na
Watumishi wote wa REA katika kutekeleza majukumu yake.
Awali,
akizungumza baada ya kukabidhi rasmi Ofisi kwa Mkurugenzi mpya, Mtangulizi wake
Mhandisi Maganga amemshukuru Mungu, Bodi na Wafanyakazi wote wa REA kwa
kumpatia ushirikiano katika kipindi chote alichofanya kazi nao.
Mhandisi
Maganga amebainisha kuwa mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya nishati
vijijini, yanatokana na ushirikiano mkubwa alioupata kutoka kwao.
Amewataka
kumpatia ushirikiano wa aina hiyo, Mkurugenzi mpya huku akibainisha kuwa yeye
binafsi anamwamini na anamtambua kama mchapakazi na mwenye uhodari katika
utendaji kazi.
Akizungumza
kwa niaba ya Bodi, Mwenyekiti Wakili Julius Kalolo amempongeza Mhandisi Hassan
kwa kuaminiwa na Rais na kuteuliwa kushika wadhifa huo mkubwa. Amemwahidi kuwa
Bodi itampatia ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yake.
Vilevile,
amempongeza na kumshukuru Mhandisi Maganga kwa ushirikiano alioutoa kwa Bodi
katika kipindi chote alichofanya kazi katika nafasi ya Mkurugenzi Mkuu.
Aidha,
wakizungumza kwa nyakati tofauti kwa niaba ya Menejimenti ya REA na wafanyakazi
wote, Kaimu Mkurugenzi wa Sera, Mipango na Utafiti, Mhandisi Elineema Mkumbo,
Kaimu Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu na Utawala, Grace Sengula pamoja na
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi (TUGHE) Tawi la REA, Swalehe Kibwana,
wameahidi ushirikiano pamoja na kutekeleza yale yote aliyoyasisitiza Mkurugenzi
mpya.
Mhandisi
Hassan Said aliteuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan kushika wadhifa wa
Mkurugenzi Mkuu wa REA kuanzia Septemba 23 mwaka huu akitokea Shirika la Umeme
Tanzania (TANESCO) alikokuwa akifanya kazi kama Meneja Mwandamizi wa Kanda ya
Mashariki.
Comments
Post a Comment