BARAZA LA WAZEE MKOA WA RUKWA LAZINDULIWA

Na. Revocatus Kassimba, SUMBAWANGA

 

Wazee wa Mkoa wa Rukwa wameiomba serikali kuwasaidia kupata nafasi ya kusikilizwa ili wawe na uwezo wa kuchangia jitihada za maendeleo pamoja na kuhakikisha wanapata huduma muhimu za kijamii.

Mwenyekiti mpya wa Baraza la Wazee Mkoa wa Rukwa Benedict Makosi (kushoto) akiwa na Makamu Mwenyekiti Desderius Sikazwe (katikati) na Katibu wao Amabilis Mpepo jana mara baada ya kumalizika uchaguzi


Hayo yamebainishwa kwenye uzinduzi wa baraza la Wazee wa Mkoa wa Rukwa jana mjini Sumbawanga ambapo pia walifanikiwa kuunda uongozi unaoshirikisha wazee toka halmashauri zote nne za Mkoa wa Rukwa.

Akizungumza mara baada ya kuchaguliwa Mwenyekiti mpya wa Baraza la Wazee Mkoa wa Rukwa, Mzee Benedict Makosi alisema kazi ya uwakilishi inahitaji moyo wa kujitolea na kusikiliza mahitaji ya wanachama.

 “Baraza letu lililokosa muunganiko wa wilaya zingine ikiwemo Nkasi na Kalambo kwani awali lilihusisha wazee wa Manispaa ya Sumbawanga pekee” alisema Mzee Makosi.

Mwenyekiti huyo alitoa rai kwa viongozi wa serikali kote mkoani Rukwa kuwa wastahimilivu na wenye moyo wa kusikiliza shida na kero za wazee muda wote watakapopata nafasi ili maisha ya wazee na wahitaji wengine yawe bora kama serikali inavyoelekeza.

Uzinduzi wa Baraza la Wazee Mkoa wa Rukwa. Pichani Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Sebastian Waryuba (katikati) akiwa na Katibu Tawala Mkoa Denis Bandisa (kulia) na kushoto ni Mwenyekiti wa Wazee Rukwa Benedict Makosi


“Uzee na kuzeeka ni dhana inayoelezea hatua ya mwisho ya makuzi ya binadamu kuanzia utoto, ujana hadi kufika uzee. Hapa Tanzania mtu anaitwa mzee kutokana na ama umri mkubwa, majukumu aliyonayo na pia hadhi yake, kwa mfano mkuu mahali pa kazi au katika ukoo” alisema Mzee Makosi.

Akizindua Baraza hilo la Wazee, Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Sebastian Waryuba aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Mkirikiti alisema kuwepo kwa Taifa la Tanzania ni kielelezo tosha cha mchango wa wazee walioutoa katika nyanja ya kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kijamii.

Waryuba aliongeza kusema pamoja na mchango walioutoa wazee bado ni moja ya kundi lililokuwa limetengwa katika jamii na hivyo nguvu za ziada kutoka Serikalini na wadau kwa ujumla zimeendelea kufanyika ili kuhakikisha wanapatiwa haki zao za msingi.

“Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 Mkoa wa Rukwa kwa mwaka 2021 unakadiriwa kuwa na wazee 73,361 kati yao Wanawake ni 37,509 na Wanaume ni 35,852. Aidha, kufikia Septemba 2021 Mkoa umetambua jumla ya wazee 29,905 kati yao Wanawake ni 15,954 na wanaume ni 13,951” alisema Waryuba.

 

Kuhusu huduma za wazee Mkuu huyo wa Wilaya alisema hadi kufikia Septemba 2021, Mkoa umetoa jumla ya vitambulisho vya matibabu bure kwa Wazee 16,311 sawa na asilimia 55 ya wazee wote waliotambuliwa, kati ya hao wanawake ni 8,515 na wanaume 7,796.

 


Akitoa taarifa ya uchaguzi wa viongozi wapya wa Baraza la Wazee Mkoa wa Rukwa, Katibu Tawala Mkoa Denis Bandisa aliwataja waliochaguliwa na nafasi zao kwenye mabano na halmashauri wanazotoka kuwa ni Benedict Makosi (Mwenyekiti, Manispaa ya Sumbawanga), Desderius Sikazwe (Makamu Mwenyekiti, Kalambo) na Amabilis Mpepo (Katibu, Manispaa).

Bandisa alitaja viongozi wengine kuwa ni Melkio Mwanakatwe (Katibu Msaidizi, Sumbawanga vijijini), Tobias Magazini (Mtunza Hazina, Nkasi), Jenerith Umela (Mwakilishi Baraza la Madiwani, Nkasi) na Nicolaus Lufungilo (Mwakilishi Baraza la Madiwani, Sumbawanga Vijijini).

Uundwaji wa Baraza la Wazee Mkoa ni sehemu ya utekelezaji wa baadhi ya matamko ya Sera ya Wazee ya mwaka 2003 na Azimio la Umoja wa Mataifa Na.46 la 1991 kuhusu haki za Wazee ambazo ni kuwa na uhuru, kushiriki na kushirikishwa, kutunzwa, kukuza utu wao na kuheshimiwa.

 

Mwisho

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.