ULEGA AAGIZA WATENDAJI KUSIMAMIA MAELEKEZO YA VIONGOZI

  

Na. Edward Kondela

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (Mb) amesema atahakikisha kila maelekezo anayoyatoa anayafuatilia kwa karibu ili kujiridhisha na utekelezaji wake na kufikiwa kwa malengo ya serikali.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akitoa maelekezo kwa uongozi wa machinjio ya Jiji la Dodoma, kukarabati beseni la kuhifadhia damu mara baada ya ng’ombe kuchinjwa wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika machinjio hayo kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ya ukarabati wa machinjio hayo


 

Naibu Waziri Ulega amebainisha hayo wakati alipofanya ziara ya kushtukiza kujionea maendeleo ya ukarabati wa machinjio ya Jiji la Dodoma yaliyoanza Tarehe 15 Mwezi Julai mwaka huu.

 

Mhe. Ulega amesema ameridhishwa na ukarabati unaondelea kufanywa ambapo hadi sasa zimetumika Shilingi Milioni 40 kwa kutumia mapato ya ndani ya machinjio hayo.

 

“Kila maelekezo tunayoyatoa, tunayatoa kwa wakati maalum na kinachofuata ni ufuatiliaji wa karibu, tunatoa maelekezo na kufuatilia utekelezaji wake, tunawapongeza watendaji wetu wizarani maana kila maelekezo tunayoyatoa wanayasimamia na mnafanya kazi nzuri maelekezo tunayoyatoa mnayafanyia kazi.” Amesema Mhe. Ulega

 

Mhe. Ulega amesema alitoa maelekezo ya kuona machinjio ya jiji la Dodoma, yanabadilika na kuwa bora na kwamba ameridhika na ukarabati unaoendelea hadi sasa ambapo awali uongozi wa machinjio ulihitaji Shilingi Bilioni Tatu, lakini aliwaelekeza kuanza kufanya ukarabati kwa kutumia mapato ya ndani.

 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) akikagua baadhi ya vifaa vipya vilivyowekwa katika machinjio ya Jiji la Dodoma, mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ya ukarabati wa machinjio hayo. Kushoto kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko kutoka wizarani Bw. Stephen Michael

Amefafanua kuwa yeye kama kiongozi anatoa maelekezo na kuhakikisha yanasimamiwa usiku na mchana na kuyafuatilia hadi mwisho wake na kutaka maboresho hayo yawe yamekamilika kufikia Tarehe 15 Mwezi Septemba mwaka huu.

 

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Stephen Michael amesema hadi sasa ukarabati wa machinjio ya Jiji la Dodoma yamefikia zaidi ya asilimia 90 ambapo maeneo 13 kati ya 15 yatakuwa yamekamilika mwisho wa mwezi huu na maeneo mawili yaliyobakia yatakamilika ifikapo Tarehe 15 Mwezi Septemba.

 

Bw. Michael amesema ni muhimu kwa wao kama watendaji wanaposimamia maelekezo ya viongozi ni kwamba wanajua athari zinazoweza kujitokeza kutokana na ulaji wa nyama isiyo na usalama na kwamba watasimamia ukarabati huo kwa weledi mkubwa.

 

Mwisho

Comments

Dodoma News
Mwanza City, Mwanza, Tanzania
Dennis G. Harrison, mmiliki mwenza wa Mtandao wa Dodoma News Blog, alizaliwa mkoani Morogoro zaidi ya miaka 40 iliyopita. Dennis ana Taaluma ya Uandishi wa Habari (Proffessional Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT). Mwaka 2009 alimaliza Shahada ya Uzamili katika Mawasiliano ya Umma, ikijikita katika Menejimenti ya Uhusiano kwa Umma na Matangazo katika chuo cha SAUT. Mwaka 2002, Dennis aliajiriwa katika Shirika la Posta Tanzania, Ofisi kuu ya Mwanza. Mwaka 2009 aliajiriwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa nafasi ya Afisa Habari. Akiwa katika ofisi hiyo alifanya kazi kwa juhudu na maarifa na kufanikiwa kuchaguliwa na wafanyakazi wote kuwa mfanya kazi bora. Kufuatia juhudi na utendaji kazi wake, alipanda hadi nafasi ya Afisa Habari Mwandamizi.